Monday 16 November 2015

UKAWA WAZIDI KUWEWESEKA





WAKATI Rais Dk. John Magufuli akianza kazi kwa kishindo kwa kufanya ziara za kushtukiza kwenye baadhi ya taasisi za serikali huku akihimiza uwajibikaji na kutowaonea huruma watendaji wazembe, kundi la  Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) limezidi kuweweseka.
Dk. Magufuli alichaguliwa na wananchi kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 25, mwaka huu, kwa asilimia 58.46 huku jumuia za kimataifa na wasimamizi wa uchaguzi huo wakikiri kuwa ulifanyika kwa mazingira huru na haki.
Wasimamizi kutoka Jumuia ya Ulaya, Jumuia ya Nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara (SADEC) na wale wa ndani,  walisema wananchi walipata fursa ya kuchagua viongozi kwa haki.
Licha ya ukweli huo, aliyekuwa mgombea urais wa CHADEMA, anayeungwa mkono na UKAWA, Edward Lowassa, ameendelea kuweweseka kwa kudai uchaguzi huo haukuwa wa haki hivyo hawatashirikiana na serikali.
Taarifa ya Lowassa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari, imedai kushangazwa na namna ambavyo ulinzi ulivyoimarishwa katika kipindi cha uchaguzi mkuu.
Amedai kuwa licha ya uchaguzi mkuu kumalizika, amani na utulivu nchini vimetoweka na kuhoji kile alichodai hofu ya kuzuiliwa kwa mikutano ya kisiasa.
Lowassa, ambaye aliwahi kuwa waziri mkuu kisha kujiuzulu kwa kashfa ya kampuni tata ya kufua umeme ya Richmond, alidai kuendelea kuipinga serikali kwa madai ya kuibiwa kura.
Kufuatia madai yao ya Lowassa, wananchi mbalimbali waliozungumza na gazeti hili, wameonyesha kushangazwa na tuhuma hizo kwa kuziita ni za kutaka kuwapotezea muda wananchi.
Alphonce Mawazo, mkazi wa Dar es Salaam, alisema madai ya Lowassa kuwa amani imetoweka yameonyesha namna ambavyo UKAWA walivyokuwa na dhamira ya kutaka utulivu uliopo utoweke.
“Hawezi kusema amani haipa wakati wananchi tunaendelea na shughuli zetu za ujenzi wa taifa kama kawaida. Huyu alichokuwa akihitaji ni kushuhudia Watanzania wakitangatanga kwa kukosa utulivu,” alisisitiza.
Mkazi wa Kimara Suka, Mwanaidi Msuya, alisema tuhuma za Lowassa ni za kushangaza na zenye lengo la kuwapotezea wananchi muda wa kufanyakazi.
Alisema kwenye kipindi cha upigaji kur, kulikuwa na mpango wa baadhi ya wafuasi wa UKAWA waliopanga kuwazuia wanawake na wazee wasiende kupigakura.
“Walikuwa hawataki wanawake wakapige kura hivyo usalama ulivyoimarishwa ulivuruga mipango yao isiyokuwa na tija,” alisema.
Tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu, UKAWA wamekuwa wakiendeleza propaganda zenye lengo la kutaka kuvuruga amani na mshikamano wa wananchi.

No comments:

Post a Comment