Wednesday 9 September 2015

POLISI YAWAONYA WANANCHI KUTOVURUGA AMANI





Na Mwandishi Wetu

JESHI la Polisi limewataka wananchi kufuata sheria na kuweka uzalendo mbele ili kuhakikisha kampeni za uchaguzi mkuu zinafanyika kwa amani bila misuguano baina ya polisi na raia.

Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Bulimba, alisema jana kuwa Watanzania wote wanaoshiriki kwenye kampeni wanapaswa kuweka mbele utaifa badala ya ushabiki wa kisiasa unaoweza kuvuruga amani.

“Wote tunapaswa kushirikiana kulinda amani yetu. Hivyo wafuasi wa vyama mbalimbali vya siasa wanapaswa kutambua kwamba kulinda amani ni jambo la msingi zaidi,” alisema. 

Aliwatahadharisha wanasiasa na wafuasi wa vyama kuepuka kujiingiza kwenye makosa ya jinai, kutokana na siasa kwa vile sheria zinazosimamia uchaguzi hazitoi mwanya kwa wanasiasa kufanya mambo yanayopitiliza na kuivuruga jamii.

Alisema jeshi la polisi limejipanga vizuri kwa muda wote wa kampeni, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi na litamshughulikia yeyote atakayevunja sheria bila kuangalia anatoka kwenye chama gani cha siasa ili kulinda amani ya nchi.

Kwa mujibu wa Advera,watu kadhaa wamekamatwa na wanaendelea kuhojiwa kutokana na kujihusisha na vitendo vya uvunjifu wa amani.

Akifunga mafunzo ya wiki mbili kwa polisi wa kada mbalimbali kuhusu haki za binadamu na matumizi ya nguvu kwa kiasi wakati wa uchaguzi yaliyofanyika hivi karibuni Dar es Salaam, Naibu Kamishna wa Polisi, Mary Nzuki, alisema jeshi hilo limechukua tahadhari zote kuhakikisha kuwa kampeni na uchaguzi unafanyika kwa amani.

No comments:

Post a Comment