Thursday 8 October 2015

KWANINI DK. SHEIN ATAPATA USHINDI WA KIMBUNGA ZANZIBAR




Na Hamis Shimye, Zanzibar
WAKATI Uchaguzi Mkuu ukitarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu, mgombea urais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein anazidi kuonekana kuwa ataibuka na ushindi wa kishindo katika uchaguzi huo.

Uchunguzi uliofanywa na UHURU, katika visiwani vya Unguja na Pemba wiki hii, umebaini sababu kubwa inayomfanya Dk. Shein kuibuka na ushindi ni utekelezaji mkubwa wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa zaidi ya asilimia 90.

Taarifa zaidi zilizopatikana katika uchunguzi huo, zilieleza kuwa utekelezaji huo wa Ilani, unawafanya hata wapinzani washindwe kueleza mambo watakayowafanyia Wazanzibar endapo watapewa ridhaa kwenye uchaguzi huo, badala yake wanadai wakichaguliwa wataleta mamlaka kamili.

UHURU lilibahatika kuweka kambi katika maeneo mengi ya Pemba, hasa katika wilaya za Wete, Mkoani na Chakechake na kubaini kuwa kuna uwezekano mkubwa nguvu ya CUF ikaondoka kwenye uchaguzi huu, kutokana na utekelezaji wa mambo katika sekta zote kuanzia elimu, afya, jamii hadi michezo kufanikiwa.

Katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2010, CUF ilishinda majimbo yote 18, lakini  wabunge na wawakilishi wa Chama hicho wameshindwa kutekeleza mambo mengi katika majimbo yao, badala yake wamekuwa ni watu kueneza chuki kati ya Wapemba na Waunguja.

Akizungumzia tatizo la wabunge hao kushindwa kutekeleza lolote licha ya  wabunge kwenye maeneo hayo kwa muda mwingi, mmoja wa wananchi wa Pemba, Ahmada Saidy Ussi alisema CCM itapata ushindi na nguvu CUF itaondoka.

Alisema tatizo kubwa la watu wa Pemba ni uoga wa kukipigia kura CCM, kwani hivi sasa kuna propaganda zinatembea kuwa Pemba hawahitaji barabara bali wanachotaka ni mamlaka kamili, ambayo yatapatikana chini ya Maalim Seif Sharif Hamad.

"Awali tulikuwa tunalalamika kuhusiana na kuwa nyuma kwa maendeleo. Dk. Shein ametekeleza mambo mengi kwa kiasi kikubwa kuliko ilivyokuwa awali. Na hilo halifichiki na ndio maana tuna msemo kuwa CCM wameleta maendeleo ili tuwapende,''alisema.

Kwa mujibu wa Ussi, ambaye ni mmoja wa wanachama wa CUF, alisema hivi sasa Pemba hakuna kero yeyote kama ilivyokuwa awali na ndio maana sera zao zimebakia kwenye mamlaka kamili na sio vinginevyo.

UHURU ilishuhudia kupoteza nguvu kwa Maalim Seif, ambaye ni mgombea urais wa CUF toka 1995, hivyo kutoa nafasi kubwa kwa Dk. Shein kuibuka na ushindi kwenye uchaguzi huo kutokana na muda mwingi kuongelea suala la maendeleo kwa Zanzibar na sio vinginevyo.

Hilo limebainika hata kwenye maskani za CUF, ikiwemo Radio One iliyoko eneo la Daraja Bovu, mjini Magharibi, Unguja, ambao wanaamini huu ni wakati wa Maalim Seif kupumzika na kwamba anapoteza muda ndani ya CUF.

Said Abdallah Said, alisema Seif anapaswa kupumzika kwa kuwa hana jipya kwa siasa za hivi sasa ndani ya Zanzibar, ambayo kwa kiasi kikubwa vijana ndio wameamka na wameonekana kuiunga mkono CCM.

"Mimi ni CUF, lakini Maalim tayari ameshapoteza mwelekeo, uchaguzi huu hatushindi na Dk. Shein atashinda, amefanya mambo mengi sana hasa katika elimu, usambazaji wa nishati ya umeme na upatikanaji wa maji safi na salama,'' alisema.

Alisema anampa nafasi kubwa Dk. Shein kutokana na uwezo wake wa kushinda kwa kuwa moja ya kitu wanachokipigania hivi sasa ni suala la mamlaka kamili pekee, ambayo kwa kiasi kikubwa linatolewa ufafanuzi kila siku.

"Sisi tuna ushabiki tu, lakini hoja ya msingi hivi sasa hatuna. Hebu niambie wewe (mwandishi wa habari) hoja yetu nini? Kama nchi tayari tunayo tena tuna katiba yetu na yenye kueleza kila kitu. Sasa mamlaka kamili tunayoyataka ni yapi?'' alihoji.

Licha ya kauli za watu hao, UHURU ilibaini sababu kubwa zinazomfanya Dk. Shein kuibuka na ushindi, mbali na wingi wa wanachama wa CCM ni kupandisha uchumi wa Zanzibar kutoka asilimia sita mwaka 2010 hadi asilimia 7.4 mwaka huu.

Pia, ameweza kuinua kiwango cha ukusanyaji mapato ya ndani ambayo yameongezeka kutoka sh. bilioni 184.4 hadi kufikia sh. bilioni 360.4, sawa na ukuaji wa asilimia 98.7.

UHURU pia ilibahatika kupata taarifa kuwa chini ya uongozi wa Dk. Shein wa miaka mitano iliyopita, mgombea huyo, ambaye pia ni Rais wa Zanzibar,  amepunguza mfumuko wa bei, ambao ulikuwa unakwamisha maendeleo ya haraka visiwani humo.

Taarifa zinaeleza kuwa mfumuho huo, umepungua kutoka asilimia 14.7 mwaka 2010 hadi asilimia 5.6 mwaka 2014, huku pia akiimarisha pato la Zanzibar kufikia dola za Kimarekani 939, ambazo ni zaidi ya sh. milioni moja kwa mwaka 2015.

Katika suala la kilimo, ambalo kwa Pemba ndio kama kitega uchumi kikuu, wakulima wameonekana kunufaika na sera mbalimbali za Dk. Shein ikiwemo kuwapatia ruzuku za pembejeo za kilimo.

Inaelezwa kuwa kuwepo kwa ruzuku hiyo ya pembejeo, kumesaidia kuongezeka kwa mazao hasa mpunga, mbogamboga na mifugo, ambapo zaidi ya wakulima 360,000 wamefaidika na hata kuamini mtu sahihi ni Dk. Shein.

Katika visiwa vya Pemba, jambo linalompa heshima zaidi Dk. Shein na hata kusifiwa na aliyekuwa Waziri Kiongozi wa Zanzibar, awamu ya sita (2000 hadi 2010), Shamsi Vuai Nahodha ni kupandisha zao la karafuu.

Nahodha alisema wiki hii katika mkutano wa kampeni uliofanyika katika Uwanja Gando, uliopo Wilaya ya Wete, Kaskazini Pemba kuwa Dk. Shein ndio mtu sahihi kutokana na kupandisha zao la karafuu, ambalo walikuwa wanahangaika nalo na hivi sasa limekuwa juu.

Inaelezwa kuwa huko nyuma, pishi moja ya zao la karafuu ilikuwa inauzwa kwa kiasi kisichozidi sh. 8,000, lakini Dk. Shein amepandisha zao hilo hadi kuwa sh. 25,000 na kusababisha wafanyabiashara kunufaika na zao hilo.

Pia, hivi sasa karafuu inaelezwa kuwa inauzwa kwa sh. 22,000 kwa daraja la pili na makonyo ni sh. 15,000. Jambo hilo ndio linalotoa mwangaza kuwa ushindi wa Dk. Shein ndani ya Pemba ni mweupe.

Mbali na kuboresha zao hilo, pia ameboresha idara ya kilimo Zanzibar na ameweza kuwagawia wananchi miche ya karafuu bure ili kulifanya zao hilo kuimarika zaidi na kila mwananchi ameonekana kufurahia wazo hilo la Dk. Shein katika kukipa hadhi kilimo.

Aidha, imeelezwa kuwa kupanda kwa bei hiyo maradufu kumeondoa uuzwaji wa zao hilo kwa njia ya magendo kupitia Mombasa nchini Kenya, ambao ulikuwa unawakosesha wananchi wa Pemba na Unguja kunufaika na zao hilo.

Dk. Shein katika miaka yake mitano, ameweza kuongeza usambazaji wa maji safi na salama kutoka asilimia 75 (2010) hadi asilimia 90 kwa mwaka 2015, ambapo maeneo yote ya mjini na vijijini yanapata maji safi na salama.

Kufanikiwa kwa Dk. Shein katika uongozi wake wa miaka mitano ndiko kunakompa nguvu zaidi ya kuibuka na ushindi wa zaidi ya asilimia 60, kama utafiti wa CCM uliotolewa hivi karibuni unavyoeleza.

No comments:

Post a Comment