Wednesday 4 November 2015

BALOZI SEIF AKUTANA NA VIONGOZI WA DINI ZANZIBAR




Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa katika picha ya pamoja na Vongozi wa Dini mbali mbali Nchi mara baada ya kufanya mazungumzo nao Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar. Kushoto ya Balozi Seif ni Kiongozi wa Timu ya Waislamu Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Kabi na Kulia ya Balozi ni Kiongozi wa Wakristo Askofu Augustino Mweleli Shao.

Picha na – OMPR – ZNZ.
                                   
Othman Khamis Ame, OMPR

 Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inakamilisha taratibu zilizobakia na tayari inajiandaa kuwachukulia hatua za Kisheria watu wote waliohusika kuharibu kwa makusudi zoezi zima la Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar uliofanyika Tarehe 25 Mwezi Oktoba mwaka huu.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akizungumza na Viongozi wa Dini mbali mbali Nchini aliokutana nao Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar kutafakari na kutafuta mbinu za kuendelea kujaribu kudumisha amani ya Nchi iliyotetereka  na kuleta mtafaruku katika kipindi hicho cha Uchaguzi.

Balozi Seif alisema ina uthibitisho kamili wa vielelezo vya ushahidi wa udanganyifu kwa maeneo yote ya Zanzibar hasa katika Majimbo ya Uchaguzi ya Kisiwa cha Pemba.

Alisema Afisa  wa Tume ya Uchaguzi au Mtu yoyote aliyehusika na udanganyifu huo aelewe kwamba mkondo  wa sheria utamkumba kwa vile vitendo walivyofanya wameisababishia hasara kubwa Serikali pamoja wa washirika wa maendeleo walioamua kusaidia uchaguzi huo.

Balozi Seif alibainisha kwamba  wakati wahusika hao wanapandishwa katika vyombo vya kisheria kujibu shutuma zinazowakabili Serikali kwa upande wake  itaweka hadharani uthibitisho kamili wa vielelezo vya ushahidi wa udanganyifu huo ili Wananchi wapate fursa ya kuelewa dhambi hiyo mbaya waliyofanyiwa na watu wachache kwa tamaa binafsi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwahakikishia Viongozi hao wa Dini kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejipanga vizuri kupitia vyombo vyake vya ulinzi kwa kupiga Doria maeneo yote katika kuona amani ya nchi inaendelea kudumu.


Aliwapongeza Viongozi hao wa Dini kwa jitihada zao wanazochukuwa za kutumia busara zao kwa kukutana na Viongozi  wa pande mbali mbali za Kisiasa wakilenga kusaidia kutuliza mumkari na machungu ya waumini wao ambao takriban wote ni  wafuasi wa vyama vya Kisiasa vilivyopo hapa Nchini.

Alivilaumu baadhi ya vyombo vya Habari hasa vile vya Nchi za Magharibi jinsi vilivyoonyesha wazi Taarifa zao nyingi  wanazotowa za zoezi zima la uchaguzi Mkuu wa Zanzibar zikionyesha  kuegemea upande mmoja tu.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alielezea masikitiko yake juu ya wangalizi wa Kimataifa walioamua kufuatilia uchaguzi Mkuu wa Zanzibar kwamba hawakwenda Kisiwani Pemba muda wote wa zoezi la kupiga kura kufuatilia changamoto zilizojitokeza katika majimbo ya Pemba.

" Nimesikitishwa na waangalizi wa Kimataifa waliokuwepo Zanzibar kwa karibu mwezi mmoja kufuatilia kampeni na uchaguzi wake wameshindwa kwenda Pemba wakati wa zoezi la kupiga kura na kuonekana  zaidi katika majimbo ya Kisiwa cha Unguja.

Balozi Seif aliishauri Idara ya Habari Maelezo kuendelea kufuatilia Taarifa zinazotolewa na vyombo mbali mbali vya Habari ndani na nje ya Nchini na kukemea au kutoa Taarifa dhidi ya uchochezi unaotolewa na vyombo hivyo.

Nao Viongozi hao wa Dini mbali mbali Nchini wameishukuru na kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ile ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua iliyochukuwa katika kusimamia amani ya Nchi.

Wananchi wa Zanzibar  wamerejea katika harakati zao za kawaida  za kimaisha  baada ya kutokea hitilafu tofauti ndani ya zoezi zima la upigaji kura kwenye  uchaguzi Mkuu wa Tarehe 25 Mwezi uliopita na kupelekea kuibuka kwa mtafaruku uliotikisa  amani ya Taifa.

No comments:

Post a Comment