Wednesday 4 November 2015

VIONGOZI WA DINI WAWAONYA WANASIASA



VIONGOZI wa dini wametakiwa kukemea watu ambao wanataka kuendeleza migogoro ya kisiasa kwa kuhamasisha vijana kufanya maandamano ambayo ni kiashiria cha uvunjifu wa amani.
Imeelezwa kuwa vijana wengi wanakubali kurubuniwa kutokana na kutopenda kujishughulisha, hivyo kulaghaiwa kwa maslahi ya watu fulani.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Sadiki aliyasema hayo jana, kwenye mkutano wa kuishukuru Kamati ya Amani ya Viongozi wa Dini mkoani hapa, kwa kuliombea Taifa kufanya uchaguzi ulio huru na wa amani.
Alisema kuna watu ambao wanataka kuendeleza migogoro ya kisiasa mara baada ya uchaguzi, badala ya kuwaza ni namna gani washirikiane na viongozi wateule kwa ajili ya kuleta maendeleo ya nchi.
Sadiki alisema inapotokea mtu anachukua majukumu ya tume ya kumtangaza mshindi, ni usaliti na ukiukwaji wa sheria ambao hauwatakii wananchi heri.
“Watu hao hao ndio ambao wamekuwa wakisambaza ujumbe kwa wananchi, hasa vijana wakiwataka kuandamana huku familia zao zikiwa nje ya nchi.
“Vijana wamekuwa wakitumika na baadhi ya wanasiasa kwa sababu hawataki kufanyakazi, wanataka kupata maisha kiraisi ndiyo maana baadhi ya watu hutumia fursa hiyo kuwarubuni,”alisema.
Aidha, alitoa wito kwa vijana kupenda kufanya kazi, hasa mwaka ujao ambao kauli mbiu yake ni ‘Hapa kazi tu’ ili kuepuka kurubuniwa au kutumika na wanasiasa wenye nia ovu.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Shekhe wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum, alisema kampeni na shughuli za uchaguzi zimeisha kwa amani na salama tofauti na ilivyokuwa inategemewa na wengi.
Alisema hayo yote ni kutokana na maombi yao pamoja na bidiii za mkuu wa mkoa kwa kushirikiana na kamati yake ya ulinzi kutoa elimu kwa wananchi kuhusu amani.
Alisema kama kuna mgombea yeyote ambaye hakubaliani na matokeo, anapaswa kufuata utaratibu na sheria za nchi kwakuzingatia katiba inavyosema.
Alhad Salum alisema wagombea wote walioshinda au kushindwa wanatakiwa kuheshimu damu za wananachi wasije kutaka kuzitumia kwa maslahi yao ya kutaka kufika wanapotaka.
“Mimi niwaombe waliokuwa washindani wote, iwe washindi au washindwa, kujiepusha na mambo ambayo yanaweza kusababisha umwagikaji wa damu za wananchi.
“Kila mmoja anatakiwa kufahamu kuwa katika kushindana, kuna kushinda na kushindwa, hivyo wakubaliane na matokeo kwa sababu tume ilikuwa huru,” alisema.
Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kubaki kama Watanzania kwa kuheshimiana bila kuona kuwa huyu ni mshindi au mshindwa.

No comments:

Post a Comment