Thursday 12 November 2015

MASHINE YA MRIA YAANZA KUFANYAKAZI MUHIMBILI




HATIMAYE Hospitali ya Taifa Muhimbili imelazimika kutumia saa mbili kukarabati mashine ya kuchunguzia magonjwa ya MRI, baada ya Rais Dk. John Magufuli, kutoa siku 14 kwa uongozi wa hospitali hiyo kuhakikisha mashine hiyo na ya CT-SCAN zinakarabatiwa.
Rais Magufuli, hivi karibuni alifanya ziara ya kushitukiza kwenye hospitali hiyo na kuwataka watumishi wake kufanyakazi na kuonya kuwa hatamuonea huruma yeyote atakayeshindwa kuwahudumia wananchi.
Mashine hiyo ilianza kufanyakazi jana alasiri, baada ya mafundi kutoka Kampuni ya Philips, kufanya matengenezo kuanzia mchana.
Aidha, mafundi hao wanaendelea kuifanyia matengenezo mashine ya CT- SCAN, ambayo nayo wakati wowote inatarajiwa kutengemaa na kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa.
Taarifa iliyotolewa jana na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Huduma kwa Wateja wa hospitali hiyo, Aminiel Aligaesha, ilisema leo watatoa taarifa kuhusu hatua za ukarabati za mashine hiyo zilipofikia.
Kurejea kwa huduma za vipimo vya MRI katika hospitali hiyo ya taifa, kutawawezesha wagonjwa kufanyiwa vipimo vya picha kwa ubora bila kutumia mionzi.
Ziara ya Rais Magufuli, imekuwa mkombozi kwa wagonjwa hususan waliokuwa wakihitaji huduma za vipimo hivyo, iliyokosekana kwa zaidi ya miezi miwili.
Baada ya ziara hiyo aliyoifanya Novemba 9, mwaka huu,Rais Magufuli alivunja bodi ya hospitali hiyo, ambayo ilishamaliza muda wake, na kumrudisha Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hussein Kidanto, aliyekuwa anakaimu nafasi ya mkurugenzi mkuu.
Rais huyo wa awamu ya tano, alionyesha kukerwa na vitendo vinavyofanywa kwa makusudi na baadhi ya madaktari, kuharibu vifaa tiba kisha kuwaelekeza wagonjwa kufuata huduma hizo kwenye hospitali binafsi.

No comments:

Post a Comment