Na Is-haka Omar, Zanzibar
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, kimesema hakina
mpango wa kufanya mazungumzo au makubaliano na Chama Cha Wananchi (CUF),
kuhusiana na suala la uchaguzi uliopita.
Msimamo huo ulitolewa jana na Naibu Katibu Mkuu wa (CCM)
Zanzibar, Vuai Ali Vuai, alipokuwa akijibu hoja zilizotolewa na Mkurugenzi wa
Mambo ya Nje wa CUF, Ismail Jussa Ladhu, juzi.
“Uchaguzi umekwisha na kazi iliyopo mbele ya CCM ni
kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Chama ya mwaka 2015/2020, ili kuhakikisha
ahadi zilizotolewa katika kampeni za uchaguzi mkuu na viongozi wa CCM
zinatekelezwa kwa vitendo,” alisema.
Vuai alieleza kupitia gazeti moja kuwa, Jussa
alinukuliwa akisema CUF inaangalia
uwezekano wa kufanya mazungumzo na CCM, kuhusiana na suala la uchaguzi.
Hata hivyo, alisema CCM haipo tayari kukaa meza moja na chama
hicho kujadili jambo, ambalo lilishafanyiwa uamuzi halali kwa mujibu wa kanuni,
taratibu na sheria za nchi.
Alisema CCM inaweza kukikaribisha chama chochote
cha upinzani kufanya mazungumzo juu ya namna gani ya kuimarisha na kusimamia
utekelezaji wa Ilani ya CCM,
siyo suala la uchaguzi mkuu kwa kuwa umeshapita kisheria na serikali zinaendelea
kuwatumikia wananchi kwa uadilifu.
Vuai alisema kitendo cha kujadili serikali zote mbili ya Zanzibar na Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kwa sasa ni kwenda kinyume na sheria za nchi kwa kuwa serikali hizo zimetokana na uamuzi halali wa
wananchi kupitia mfumo wa uchaguzi wa kidemokrasia.
Aliwataka wafuasi wa CUF na wananchi kwa ujumla,
kupuuza madai yaliyotolewa na kiongozi
huyo, hususan kuhusu mantiki ya kuundwa kwa serikali ya mpito Zanzibar, hatua
ambayo haiwezekani na inaashiria kuvunja Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984.
“CCM hatuna mpango wa kukaa meza moja na chama
chochote cha upinzani, siyo CUF tu, kujadili uchaguzi kwa kuwa tayari umeshapita
kwa vigezo vyote vya uhalali wa kisheria.
“Hoja na ajenda
ya kufanyika kwa uchaguzi wa mpito Zanzibar, kwa sasa ni ndoto za mchana
ama kujifurahisha kwa kutafuta umaarufu wa kisiasa usiokuwa na uzani wala mafanikio kwa wafuasi wa chama kinachojenga
hoja hizo hapa nchini,” alisema.
Vuai alisema CCM inaamini uchaguzi umekwisha na
sasa inajipanga na maandalizi ya uchaguzi ujao wa mwaka 2020.
Alisema CUF kwa sasa imekosa mwelekeo ndiyo maana
viongozi wake wanafikia hatua ya kuwadanganya wafuasi wao kwa mambo, ambayo
kiuhalisia wanajua hayawezi kufanyika katika historia ya uwanja wa kisiasa
Zanzibar.
Vuai alisema chama chochote cha siasa pamoja na kuwa na jukumu la kushinda na kusimamisha
dola katika uchaguzi mkuu, bado kinatakiwa kuwa na miongozo imara ya kusimamia
ukweli, haki na uwazi kwa wafuasi na wananchi, vigezo ambavyo vimekosekana
ndani ya CUF tangua kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa 2015.
Alisisitiza kuwa kazi iliyopo mbele ya CCM ni
kujiandaa kwa mambo mbalimbali, yakiwemo uchaguzi wa ndani wa Chama wa mwaka
2017, kwa ajili ya kupata viongozi makini na hodari, ambao watakuwa na jukumu
la kusimamia maandalizi ya uchaguzi wa mwaka 2020.
Naibu Katibu Mkuu alitaja jukumu la msingi
linalotekelezwa na CCM kuwa ni uhakiki
wa mali za Chama, ili kujiridhisha zaidi ikiwa ni mkakati wa uimarishaji wa hali
ya siasa na uchumi ndani ya CCM.
Aliwasihi wafuasi wa chama hicho na wananchi kwa
ujumla, kuendelea kuwa watulivu na kushirikiana kikamilifu na serikali zote
mbili.
Aidha, aliwataka wananchi kuwafichua baadhi ya
wanasiasa wanaojihusisha na vitendo vya kuharibu amani na utulivu wa nchi.
No comments:
Post a Comment