Na Happiness Mtweve, Dodoma
ZAIDI ya Watanzania 450,000 wana tatizo la akili
kwa kujitambua ama kutojitambua.
Aidha, katika mkoa wa Dodoma, kila siku watu 12,
wanapokelewa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Wagonjwa wa Akili ya Mirembe,
kutokana na tatizo hilo.
Hayo yalielezwa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini,
Christina Mndeme, wakati akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya
Jamii, Jinsia na Watoto, katika maadhimisho ya Siku ya Afya ya Akili Duniani, yaliyofanyika
kitaifa mkoani humo.
Alisema tatizo la akili huathiri kufikiri, kuhisi, kutambua
na kutenda na kwamba, limekuwa linaongezeka kwa kasi.
"Kutokana na takwimu hizi, ifikapo mwaka 2050,
idadi ya wagonjwa wa akili duniani itaongezeka kufikia watu milioni 60,"
alisema.
Alisema kwa mujibu wa taarifa ya akili na dawa za
kulevya ya mwaka 2013/2014, mkoa unaoongoza kuwa na wagonjwa wengi wa akili ni
Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mkoa huo una asilimia
mbili ya wagonjwa wa akili, ukifuatiwa na Mwanza wenye asilimia 1.2 huku Rukwa
ukiwa wa mwisho ukiwa na asilimia 0.2.
Christina alisema takwimu hizo ni kwa mujibu wa Shirika
la Afya Duniani (WHO).
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa
Dodoma, Dk. James Kiologwe, alisema kwa Dodoma, wagonjwa 1,256, walipatikana
katika kipindi cha mwaka 2015.
Alisema kila siku wanapokea wagonjwa 12, ambao wana
ugonjwa wa akili, wanaotoka katika maeneo mbalimbali.
Dk. Kiologwe alisema idadi hiyo ya wagonjwa kwa
mkoa wa Dodoma ni kutoka katika vituo 132, vilivyopo mkoani humo.
Naye Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufani ya Wagonjwa
wa Akili Mirembe, Erasmus Mganga, alieleza sababu kuu mbili zinazosababisha
ugonjwa wa akili, kuwa ni ile ya mtu kuzaliwa na vinasaba vya ugonjwa huo,
ambapo vinakuwa ni vya kurithi.
Nyingine inatokana na magonjwa ambayo yanashambulia
ubongo, ikiwemo mtu kuugua ugonjwa wa malaria, uti wa mgongo na mapafu, hivyo huathiri
ubongo.
Alisema mgonjwa huyo akishatibiwa na kupona,
anabaki na tatizo kwenye ubongo, hivyo kupatwa na ugonjwa wa kichaa.
Kupitia wizara, alisema serikali ina mpango wa
kuanzisha kamati ya dawa za kulevya kila mtaa, ili zisaidie kuwatambua
watumiaji wa dawa hizo.
Pia, alisema katika hopitali hiyo, wanapokea
wagonjwa wa akili walioathirika kutokana na uvutaji bangi.
Aliitaja sababu
nyingine inayochangia hali hiyo kuwa ni umasikini, unyanyapaa na unyanyasaji, ambapo
mtu mwenye vinasaba vya ugonjwa huo, akikutana na mambo hayo hujikuta ugonjwa
ukifumuka.
Alisema serikali imeingiza kwenye mitaala ya
mafunzo elimu ya kuhusiana na dawa za kulevya.
Kutoka Zanzibar, Waziri asiyekuwa na Wizara Maalumu,
Juma Ali Khatib, amewataka madaktari wanaoshughulikia wagonjwa wa akili katika
hospitali za Zanzibar, kujenga uzalendo wakati wakitoa huduma zao.
Alisema kwa kufanya hivyo, kutawezesha wagonjwa wa
matatizo hayo kuwa na imani na tiba wanazozitoa.
Waziri Khatib, aliyasema hayo jana, wakati akitoa
salamu zake katika maadhimisho ya Siku ya Wagonjwa wa Akili Duniani,
zilizofanyika katika Hospitali Kuu ya Kidongo Chekundu mjini Unguja, ambapo aliwafariji
kwa kuwapatia matunda na vinywaji.
Waziri huyo alisema kazi ya kuwahudumia wagonjwa wa
akili inahitaji kujitolea zaidi kwa vile wagonjwa wanaowahudumia tayari huwa ni
wenye matatizo.
“Ni vyema kwa madaktari ambao wamechagua fani ya
kutoa huduma katika eneo hilo, kuona wanakuwa wazalendo zaidi,” alisema.
Alisema tatizo la wagonjwa wa akili hapa nchini
bado lipo na limekuwa likiongezeka siku hadi siku, hivyo serikali imeamua
kuimarisha utoaji wa huduma katika sekta ya afya kwa kusomesha watoa huduma
zaidi, ikiwa ni hatua itakayosaidia kupatikana wataalamu wenye uwezo mzuri wa
fani ya tiba kwa visiwa vya Unguja na Pemba.
Akitoa mfano wa hilo, alisema mpango wa serikali ya
Zanzibar kusomesha madaktari wa fani mbalimbali hapa nchini na kuja kwa ujenzi
wa Hospitali Kuu ya Abdalla Mzee, Kisiwani Pemba na Hospitali ya Mnazi Mmoja na
kuongeza vitengo vyake, ni ushahidi tosha wa dhamira ya serikali kukuza ustawi
wa sekta hiyo ya afya.
Kutokana na hatua hizo za serikali, Waziri Khatib,
aliwataka wanafunzi wanaochukua fani mbalimbali katika sekta ya afya,
kuzingatia miiko ya utumishi wao watapomaliza masomo yao kwa kuacha kuwa na
tabia ya kuwatolea matusi wagonjwa.
Aidha, aliwataka wanafunzi hao, kuwaona wagonjwa wa
akili ni sawa na wagonjwa wengine wanaohitaji kupatiwa matibabu yaliyo sahihi.
Alisema serikali itajitahidi kuhakikisha inawaangalia
katika maslahi yao kwa kuwapatia vifaa vya kufanyia kazi.
Waziri Khatib aliwaonya wafanyakazi hao kujiandaa
kuvitunza vifaa na majengo mapya ya Hospitali ya Kwa Abdalla Mzee na Mnazi Mmoja.
Awali, akitoa salamu zake kwa niaba ya Katibu Mkuu
wa Wizara ya Afya, Abdumalik Akili, Mkurugenzi wa Huduma za Hospitali Kuu ya
Mnazi Mmoja, Mohammed Dahoma, alisema serikali imeshajipanga kuona
inashughulikia tatizo la wagonjwa wa akili.
Alisema hatua hiyo inatokana na idadi inayowapa
huduma imeongezeka kutoka mwaka 2006, kwa kufikia zaidi ya wagonjwa 100,000.
Alitaja miongoni mwa changamoto zinazoikabili hospitali hiyo kuwa ni uwepo wa dawa
zisizotosheleza kwa mahitaji halisi ya wagonjwa wanaotibiwa katika taasisi hiyo.
Alitoa wito kwa jamii kutoa ushirikiano, ili
kusaidia tiba za wagonjwa hao kwa kuwa ni sehemu ya matibabu yao.
Dk. Akili aliwataka wahudumu wa sekta hiyo, kukaa
pamoja kuziangalia changamoto zilizomo katika matibabu ya afya ya akili, hususan
sera na sheria zinazosimamia taasisi hiyo.
Mshauri wa Rais Habari, Utalii, Utamaduni na
Michezo, Abdalla Mwinyi Khamis, aliwataka wanafunzi wanaojifunza fani ya kutoa
huduma kwa wagonjwa wa akili, kuifahamu vyema historia ya kazi hiyo, ikiwa ni
hatua itayowasaidia kutoa tiba bora kwa wanaougua maradhi hayo.
No comments:
Post a Comment