Tuesday 11 October 2016

VIFAA VYA KUHAKIKI VYETI VYAIBWA




Na Chibura Makorongo, Shinyanga
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, vifaa vinavyotumika kuhakiki vyeti kwa watumishi wa umma na kuandikisha vitambulisho vya  taifa (NIDA), vinadaiwa kuibwa na watu wasiojulikana kwenye jengo la ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, mkoani Shinyanga.
Vifaa hivyo, zikiwemo kamera mbili na viegesho vyake,  vimebainika kupotea jana, asubuhi wakati wa kujiandaa kuendelea na uhakiki wa vyeti na kuandikisha vitambulisho vya taifa.
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani, Nyabaganga Talaba, alithibitisha upotevu wa kamera mbili za NIDA.
“Leo asubuhi (jana), ofisa wa NIDA alibaini kamera  mbili na viegesha vyake havionekani. Tunaendelea kufanya uchunguzi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kuwabaini wahusika na kupata vifaa hivyo,” alisema.
 Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Stephen Magoiga, alikiri kupotea kwa kamera mbili na viegesha vyake vilivyokuwa vimehifadhiwa kwenye ofisi ya halmashauri yake kwa ajili ya kupigia picha za NIDA.
Hata hivyo, alisema bado hajawapata taarifa zaidi kuhusu upotevu wa vifaa hivyo na kuahidi kutoa taarifa zaidi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Muliro Muliro, alithibitisha kutokea kwa tukio la upotevu wa vifaa hivyo na kusema kuwa uchunguzi unaendelea.
“Vifaa hivyo vilikuwa vimehifadhiwa katika jengo la halmashauri, ambalo lina ulinzi, lakini vimekutwa havipo.
Nilichoagiza uchunguzi ufanyike ili tujue kamera mbili na viegesha vyake viko wapi,” alisema.
Alisema vifaa hivyo vinatumika kwa kuandikisha vitambulisho vya taifa, sambamba na uhakiki wa yeti kwa watumishi wa umma.
Alisema wanaendelea na uchunguzi kuhusu tukio hilo ili kujua kama kuna wizi au la na kwamba, mpaka sasa kuna baadhi ya watu wanahojiwa.

No comments:

Post a Comment