Sunday 13 September 2015

DK. MAGUFULI: DAWA ZA MIFUGO KUSHUKA BEI



 Mgombea wa Urais kupitia CCM Dk. John Pombe Magufuli akihutubia wakazi wa Igunga kwenye mkutano wa kampeni za CCM zilizofanyika kwenye uwanja wa Barafu
 Wakazi wa Igunga wakimsikiliza mgombea wa urais kupitia CCM Dk. John Pombe Magufuli kwenye mkutano wa kampeni ulioanyika kwenye viwanja vya Barafu.

 Mgombea wa Urais kupitia CCM Dk. John Pombe Magufuli akiwanadi wagombea ubunge wa CCM wanaogombea katika majimbo ya Igunga Dk. Dalally Kafumu na jimbo la Manonga Seif Hamis Gulamali  katika mkutano wa kampeni za CCM zilizofanyika kwenye uwanja wa Barafu
Mgombea wa Urais kupitia CCM Dk. John Pombe Magufuli akimnadi mgombea udiwani wa kata ya Maganzo
 Mgombea wa Urais kupitia CCM Dk. John Pombe Magufuli akimnadi mgombea ubunge jimbo la Kishapu Ndugu Suleiman Masoud Nchambi kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika Kishapu
NA SELINA WILSON, KISHAPU
MGOMBEA Urais wa CCM, Dk. John Magufuli, amesema serikali yake itatoa kipaumbele kikubwa kwa wafugaji na wakulima, ikiwemo kushusha bei za pembejeo na dawa za mifugo ili kuondokana na umasikini.
Alitoa ahadi hizo zenye neema kwa wakulima na wafugaji kwa nyakati tofauti jana, wakati akihutubia mikutano ya kampeni katika wilaya za Kishapu, Maswa na Igunga.
Alisema anatambua changamoto zinazowakabili wafugaji na wakulima kutokana na bei kubwa za dawa za mifugo na pembejeo pamoja na malisho.
“Tunataka mifugo itunufaishe kiuchumi, serikali yangu itaweka mazingira mazuri kwa kuboresha upatikanaji wa dawa za mifugo ili wafugaji nao wanufaike,” alisema.
Alisema pia anakusudia kuwekeza katika viwanda vya mazao ya mifugo, ikiwemo viwanda vikubwa vya nyama, ngozi, viatu, mikoba na mikanda itengenezwe hapa nchini kwa ngozi.
“Tukitengeneza viatu vya wanafunzi, viatu vya askari na kuviuza hapa nchini na nje, tutapiga hatua kubwa kimaendeleo. Ethiopia imepiga hatua kubwa kwa viwanda vya ngozi,  kwa nini sisi tushindwe,” alisema.
Dk. Magufuli alisema pia kupitia ufugaji , serikali yake itashirikiana na wawekezaji wa ndani kuanzisha viwanda vya kusindika maziwa ili yauzwe nje ya nchi.
Akiwa Igunga mkoani Tabora, Dk. Magufuli alihutubia maelfu ya wananchi waliofurika katika uwanja wa Barafu mjini Igunga, ambapo aliwatangazia neema ya kutatua kero kubwa ya maji.
Alisema wanapotengeneza barabara, wanajenga madaraja, serikali yake itakachofanya ni kuchimba mabwawa makubwa na kuhifadhi maji kwa ajili ya matumizi ya wananchi.
Dk. Magufuli alisema miradi ya barabara na madaraja ndio inayotumia fedha nyingi zaidi kuliko miradi ya maji, hivyo kama aliweza kutengeneza mtandao wa barabara za lami kilomita 17,666, hawezi kushindwa.
“Kama niliahidi kujenga daraja la Mbutu hapa Igunga na likajengwa na hili la maji niacheni, sitashindwa, ni mambo rahisi yanayohitaji mtu kama Dk. Magufuli, nichagueni niwe rais ili niwafanyie kazi. Mimi Magufuli ni kazi tu,” alisema.
Katika hatua nyingine, Dk. Magufuli aliahidi kujenga kilometa nne za barabara za lami katika mji wa Igunga, ili kuuweka katika hali bora zaidi.
Aliwataka wananchi wa Igunga wamchague Dk. Peter Kafumu, awe mbunge  kwa kuwa yapo mambo mengi kwenye ilani yanayotakiwa kutekelezwa kwenye jimbo hilo, hivyo wakimpatia Kafumu yatatekelezwa kirahisi.
Msichague wabunge wasusaji
Katika hatua nyingine, Dk. Magufuli aliwataka wananchi kutochagua wabunge wenye tabia ya kususia vikao vya Bunge wakati mipango muhimu kuhusiana na maendeleo ikijadiliwa.
Alikuwa akizungumza na wananchi wa majimbo ya Maswa Mashariki na Magharibi, katika mikutano ya kampeni za uchaguzi mkuu.
Alisema kutokana na kuchagua wabunge wenye tabia hiyo, ndio maana Wilaya ya Maswa licha ya kuwa kongwe, bado imeendelea kubaki nyuma kimaendeleo.
Alisema wabunge wa upinzani mara nyingi ndio wamekuwa wakisusia vikao vya Bunge na kutoka nje wakati wenzao wakijadili mipango muhimu ya maendeleo.
“Kwenye vikao vya bajeti ndio mahali ambapo wabunge wanawabana mawaziri ili wapitishe miradi ya maendeleo katika maeneo yao. Lakini wao wanatoka nje na kuacha wenzao wanapigania majimbo yao,” alisema.
Alisema Maswa inapitwa na Wilaya ya Chato, ambayo ni mpya na haijafikisha hata miaka 10, lakini imepiga hatua kubwa kimaendeleo, hivyo kuwataka wananchi kutumia uchaguzi huu kufanya marekebisho kwa kuchagua wabunge bora wa CCM.
Dk Magufuli alisema maendeleo yanakuja kwa mipango inayoanzia kwenye vikao mbalimbali, ikiwemo vikao vya Bunge la Bajeti, ambavyo ndivyo vinapitisha bajeti za  miradi yote ya maendeleo.
Awali, mgombea ubunge wa Maswa Mashariki kwa tiketi ya CCM, Stanslaus Nyongo, alimuomba Dk. Magufuli awasaidie kutatua changamoto kubwa za jimbo hilo, ambazo ni maji, barabara,umeme na elimu.
Nyongo alisema Mwaswa ndio wilaya iliyozaa Wilaya za  Bariadi na Meatu, lakini yenyewe imeendelea kubaki nyuma kimaendeleo hivyo alimuomba Dk Magufuli akiingia Ikulu, aingalie wilaya hiyo kwa namna tofauti.
Akizungumza katika jimbo la Maswa Magharibi, Mjumbe wa NEC, Stephen Wassira, aliwataka wananchi wasikubali kufanya majaribio wakachagua viongozi kwa ushabiki.
“Mmewachagua wapinzani mmeona wanachofanya bungeni, msifanye ushabiki, angalieni viongozi watakaowaletea maendeleo. Awamu ya tano itaongozwa na Rais Dk. Magufuli, anataka watu wachapa kazi mtapata maendeleo,” alisema. 
Msafara wa Dk. Magufuli, ukitokea Maswa kwenda Igunga mkoa wa Tabora, ulilazimika kusimama katika maeneo ya Kishapu, Kolandoto na Maganzo mkoani Shinyanga, kabla ya kuingia katika eneo la Igurubi, Igunga mkoani Tabora.

No comments:

Post a Comment