Wednesday 9 September 2015

DK: MAGUFULI: NITAREJESHA HESHIMA YA JIJI LA TANGA




Mgombea wa Urais kupitia CCM Dk. John Pombe Magufuli akihutubia wakazi wa mji wa tanga kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye viwanja vya Tangamano ambapo aliahidi kuboresha Bandari ya Tanga, kujenga Viwanda vya matunda na samaki ili kuweza kupunguza tatizo kubwa la ajira
Wananchi wakimsikiliza mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Magufuli alipowahutubia kwenye viwanja vya Tangamano
 Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia  ambaye pia ni mgombea Ubunge wa Jimbo la Bumbuli Mhe. January Makamba akihutubia wakazi wa mji wa Tanga kwenye mkutano wa kampeni za CCM
 Naibu Waziri wa Fedha na mgombea ubunge wa Jimbo la Iramba  Magharibi Mheshimiwa Mwigulu Nchemba akihutubia wakazi wa Tanga mjini kwenye mkutano uliofanyika kwenye uwanja wa Tangamano
Umati wa wananchi (picha ya juu na chini) uliofurika kumsikiliza Dk Magufuli alipokuwa akiwahutubia mjini Tanga juzi

NA SELINA WILSON, TANGA
MGOMBEA urais wa CCM, Dk. John Magufuli, amesema akipata ridhaa ya wananchi atarejesha heshima ya Jiji la Tanga kwa kufufua na kujenga viwanda ili kufungua fursa za kiuchumi.
Amesema miaka iliyopita watu wa mikoa mbalimbali walikua wanakimbilia Tanga kutafuta ajira kutokana na kuwepo viwanda vingi vya uzalishaji wa bidhaa mbalimbali.
Dk. Magufuli alisema hayo jana kwa nyakati tofauti katika mikutano ya kampeni za uchaguzi mkuu aliyoifanya katika Wilaya za Muheza, Pangani na Tanga Mjini katika mkutano mkubwa uliofanyika Uwanja wa Tangamano.
Alisema serikali yake itajenga viwanda vya samaki katika maeneo ya ukanda wa Pwani ili kuhakikisha rasimali hiyo inawanufaisha Watanzania hususan wananchi wa maeneo hayo.
“Tutajenga viwanda ili tudhibiti hata wezi wanaokuja kwenye bahari yetu kuvua samaki. Tutashusha bei ya vifaa vya uvuvi ili wanaofanya shughuli hizo wanufaike na rasilimali za nchi yao,” alisema Dk. Magufuli.
Dk. Magufuli aliwataka wanaotaka kuja kuwekeza hapa nchini wajitokeze kwa kuwa milango ipo wazi kwa ajili ya viwanda ikwemo vya matunda vitakavyowezesha wananchi kusafirisha juisi kwenda kwenye masoko badala ya kusafirisha machungwa.
“Tutavifufua viwanda vyote vilivyofungwa ili vifanye kazi ya uzalishaji na Watanzania hususan vijana wapate ajira. Tanzania ni nchi tajiri, tutatumia utajiri huo kuwanufaisha Watanzania wote,”alisema Dk. Magufuli.
Akiwa Pangani, Dk. Magufuli alisema serikali yake kuanzia mwakani itaanza ujenzi wa Daraja ya Mto Pangani ili kuhakikisha wananchi wanarahisishiwa usafiri kati ya Pangani na wilaya zingine ikiwemo Bagamoyo mkoani Pwani.
Pia, alisema serikali itanunua kivuko kipya ambacho kitakuwa kinafanya kazi wakati wa ujenzi wa daraja na kwamba tayari wataalamu wameshanza kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi wa daraja hilo.
“Nikiwa Waziri wa Ujenzi nilinunua Kivuko cha MV Pangani ambacho kinaendelea kutumika mpaka sasa na kinatumiwa na wananchi wote bila kujali itikadi zao, hivyo nawaomba wananchi mniamini ili niwatumikie,” alisema.
Dk. Magufuli aliahidi ujenzi wa barabara ya lami kilometa 178 kutoka Tanga/Pangani/Saadan hadi Bagamoyo.
Katika hatua nyingine, alisema chini ya utawala wake wazee hawatalipa nauli kwenye Kivuko cha MV. Pangani kwa kuwa ni watu wazima wanaohitaji kuendelea na shughuli zao bila kuhangaika.
Dk. Magufuli alisema watu wanaweza kuona ni siasa, lakini msimamo wake ni kutekeleza miradi yote na kwamba fedha zipo isipokuwa kuna mafisadi ambao wanatumia fedha za serikali vibaya na kuwa akiingia Ikulu atapambana nao na kufikisha huduma kwa wananchi.
Akiwa Muheza, Dk. Magufuli alisema ana dhamira ya kutatua tatizo la muda mrefu la maji katika mji huo na kwamba atatatua kero hiyo katika kipindi kifupi baada ya kuingia madarakani.
Akimnadi, Mgombea ubunge wa jimbo hilo , Balozi Adadi Rajabu, Dk. Magufuli alisema anamfahamu ni mtu mfuatiliaji ambaye atahakikisha anafanya naye kazi bega kwa bega.
“Adadi ni rafiki yangu ambaye ninakwenda kwake usiku na mchana…ni mfuatiliaji wa mambo kama mimi…alikuwa mchapakazi hodari alipokuwa katika majeshi na hata kama balozi,” alisema Dk. Magufuli na kuwa CCM imefanya jambo jema kuteua jembe hilo.
Awali, akizungumza katika mkutano wa kampeni wa Muheza, Katibu Mkuu Mstaafu wa CCM, Yusuf Makamba, alisema Dk. Magufuli ni mgombea mwenye sifa kuzidi wagombea wote wanaowania urais mwaka huu.
Makamba alisema , Dk. Magufuli ana sifa za elimu, anao uwezo wa kuongoza nchi kwa kuwa ni mchapa kazi na hana kashfa katika utendaji wake.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara, Mgombea Ubunge wa Viti Maalumu na Mujumbe wa Baraza Kuu la UWT, Ummy Mwalimu, alisema Wanawake wa Mkoa wa Tanga wana kila sababu ya kumpigia kura Dk. Magufuli  kwa kuwa ni muadilifu na mchapa kazi.
“Wanawake tunafahamu unao uwezo wa kutuvusha Watanzania. Kubwa zaidi ni kwamba umetupa heshima wanawake kwa kumteua Samia Suluhu kuwa mgombea mwenza na kuandika historia ya Tanzania kupata Makamu wa Rais mwanamke,” alisema.
Katika mikutano ya kampeni, Dk. Magufuli aliwapokea wanachama zaidi 20 kutoka CHADEMA walioamua kukihama chama hicho huku wakieleza kukerwa na utaratibu wa kuwatumia vijana bila kuwanufaisha.
Akizungumza mjini Muheza kwa niaba ya wenzake, kijana maarufu, Rashid Nassor Rashid , alisema alikuwa mpiga debe maarufu wa CHADEMA na ana kundi kubwa la vijana wenzake wameamua kuhama kwa kuwa wanahitaji mabadiliko ya kiuchumi ambayo wanaamini watayapata kwa Dk. Magufuli.
Kabla ya kuhutubia mikutano ya Muheza, Pangani na Tanga Mjini, Dk. Magufuli akitokea Handeni alilazimika kusiamama na kuzungumza na wananchi katika maeneo mbalimbali ikiwemo  Mkata, Kabuku, Michungwani, Hale, kutokana na hamasa ya wananchi kutaka kumsikiliza.

No comments:

Post a Comment