Tuesday 22 September 2015

MAALIM SEIF NI FISADI- SHAKA




Mwandishi Wetu, Zanzibar
KAIMU Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana  wa Chama Cha Mapinduzi  (UVCCM), Shaka Hamdu Shaka, amemtaja ngombea urais wa Zanzibar kupitia CUF, Maalim Seif Sharif Hamad kuhusika na vitendo vya ufisadi na uvufujaji wa fedha za umma wakati akiwa Waziri Kiongozi wa Zanzibar.
Mbali na hilo, amesema Maalim Seif ni kiongozi atakayesumbua Tanzania na kuiondoa katika amani na utulivu wake kwa kuwa kwa muda mrefu amejipika na kuwa kupe wa madaraka.
Shaka, alitoa madai hayo juzi katika mkutano wa kampeni wa kuwanadi wagombea wa CCM, katika jimbo la Mwanakwerekwe mjini Unguja, zilizofanyika kwenye viwanja vya Ijtmai.
Alisema mgombea huyo urais wa CUF ni kupe na king'ang'anizi wa madaraka, asiyetosheka kwa nafasi yoyote na kwamba kutamani kwake urais huenda ana ajenda ya  siri dhidi ya maendeleo ya Zanzibar na mustakabali wake kisiasa , kiuchumi na kiusalama.
"Maalim  Seif ni kupe wa madaraka, hatosheki na hakinai kushika nafasi yoyote hadi awe Rais wa Zanzibar. Mtazameni kwa makini na mtahadhari naye, hana nia njema, pia ni hatari kwa mapinduzi yetu, umoja na Muungano wa Tanganyika na  Zanzibar,” alisema Shaka.
Alisema mwanasiasa huyo akiwa Waziri Kiongozi katika miaka ya 1980, alichukua sh. milioni 100 kwa ajili ya kwenda kujitibu mafindofindo nchini Brunei, lakini hadi sasa hajaonyesha vilelelezo, viambatanisho au mchanganuo wa matumizi ya fedha hizo za umma.
“Huyu ni fisadi na mbadhirifu wa mali za serikali, hastahili  kuwa rais,"alisema Shaka, ambaye Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar.
Alisema uamuzi wa Maalim Seif kwenda kutibiwa nje ya nchi unatofautiana na ahadi aliyoitoa akiwa serikalini kwamba, angekuwa akitibiwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja iliyoko Unguja.
"Maalim Seif amejisahau na kuamua kutia ulimi wake puani kwa kukataa kuheshimu ahadi yake ya kutibiwa nchini, sasa anatumia fedha nyingi za umma nje kila mwaka, ambapo safari yake moja hugharimu mamilioni ya fedha, ambayo yangeweza kutumika kwa shughuli zingine za maendeleo ya Wazanzibari na Watanzania kwa jumla,” alieleza Shaka.
Alisema mwanasiasa huyo anaposema ana uwezo wa kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kuleta maisha bora kwa wananchi wote kwa siku mia moja, anajitafutia umaarufu wa kisiasa na wala hana ubavu wa kutekeleza hayo kama anavyodai kwenye majukwaa ya kisiasa.
"Awamu ya kwanza chini ya Mzee Abeid Karume iliichukua Zanzibar miaka minane kuanzia mwaka 1964 hadi 1972, wapinzani walipompiga risasi, angalau kujenga nyumba za maendeleo, iweje leo Seif anayekwenda kwa mkongojo alete mabadililo kwa siku mia, vijana wenzangu akili za kuambiwa changanyeni na zenu," alisema.
Katibu Mkuu huyo alimtupia lawama Maalim Seif na kudai kuwa mwaka 1995, alitamka kwamba akishinda urais atautambua ufalme uliopinduliwa Zanzibar mwaka 1964, na kwamba atayazamisha Mapinduzi ya Zanzibar katika mkondo wa Nungwi.
Shaka alisema kiongozi huyo hana nia njema ya kujenga umoja na kuleta maelewano, bali anakusudia kushika urais ili kuwagawa wananchi kwa mapande ya unguja na upemba.
Aliwataka wananchi kuamka, kumtazama na kutompigia kura za ndiyo mgombea huyo wa CUF na kumhesbu kama ni adui namba moja wa misingi ya umoja, upendo na mshikamano wa kitaifa, anayepigania kuzorotesha juhudi za vyama  vya  ASP na TANU.
"Nchi yetu imepatikana kwa harubu ya  Mapinduzi yaliyouangusha usultan uliodumu miaka zaidi ya 160, tusikubali kupoteza urithi tulioachiwa na bibi, babu, shangazi na wajomba zetu kwa kukubali ahadi za kusadikika zisizoingia akilini," aliasa.
Aliwaomba wananchi wa Mwanakwerekwe kuwachagua wagombea waliosimamishwa na CCM kuwania nafasi mbalimbali zitakazopigiwa kura Oktoba 25, mwaka huu, wakiongozwa na mgombea urais wa Tanzania Dk. John Magufuli, Dk. Ali Mohamed Shein kwa urais wa Zanzibar, wabunge, wawakilishi na madiwani.

No comments:

Post a Comment