Monday 21 September 2015

MSUKUMA AMCHANA MGOMBEA WA CHADEMA





Na Charles Mganga, Chato

MWENYEKITI wa CCM Mkoa wa Geita, Joseph Kasheku ‘Msukuma’, amemponda mgombea wa UKAWA, Edward Lowassa kwamba hafai, hana sifa.
Aidha, Msukuma alisema hata mikutano yake ya kampeni ambayo amekuwa akiihutubia, hutanguliza fedha kwa ajili ya kuwaandaa wanachama wao.
 "Naomba niwaambie mimi ndiye najua siri kubwa za Lowassa, huwa wanatanguliza fedha kabla ya kuanza kuhutubia," alisema Msukuma.
Msukuma aliwataka wananchi kupokea fedha zao, kwa sababu ni za wananchi wanaolipa kodi, lakini akawasihi kufanya uamuzi makini kwa kumchagua Dk. John Magufuli kwani anastahili kutokana na uchapakazi wake.
Msukuma aliwaponda waliohama CCM, kwamba wamefuata mkumbo na kuwataja wenyeviti wa zamani wa CCM, Khamis Mgeja wa Shinyanga na Mgana Msindai wa Singida, kuwa ni makapi na mizigo.
Pia, alimtaja waziri wa zamani wa mambo ya ndani, Lawrence Masha kwamba naye hana uwezo wowote.
"Amegombea sehemu mbalimbali na kushindwa hakuwa na msaada, "alisema Msukuma huku akishangiliwa na wananchi waliofurika katika mkutano huo.
Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Abdallah Bulembo, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuia ya Wazazi, aliendelea kuwachana UKAWA kwamba kamwe hawawezi kwenda Ikulu.
"Haiwezekani UKAWA kwenda Ikulu kwa sababu siyo wodi ya wagonjwa,"alisema Bulembo.
 Naye mke wa Dk Magufuli, Janeth, kwa mara ya kwanza, alisimama kuwaomba Watanzania kumchagua mgombea huyo wa urais.
 Pia, aliwataka kumchagua Dk. Merdad Kalemani kuwa mbunge wa Jimbo la Chato.
Wakati huo huo, mgombea urais wa CCM, Dk. John Magufuli jana aliwaaga rasmi na kuwaomba kura wananchi wa Chato, alipohutubia umati wa watu uliofurika kwenye viwanja vya sekondari ya Chato.
Dk. Magufuli, ambaye ameongoza jimbo la Chato kwa miaka 20 mfululizo, alisema anagombea urais kwa kuwa anazo sifa, anatosha na dhamira yake ni kuwatumikia watanzania na kuwaletea maendeleo ya kweli.
Aidha, amesema mtu pekee mwenye uwezo wa kuleta mabadiliko ya kweli na si bora mabadiliko ni yeye kwa kuwa amepikwa vyema na marais waliotangulia wa awamu ya tatu na ya nne.
Dk. Magufuli aliwataka wananchi kudumisha amani huku akisema awamu zilizotangulia, zimefanya makubwa hivyo, anahitaji urais ili kuyaendeleza mazuri yaliyofanywa na watangulizi wake.
Kwa mujibu wa Dk. Magufuli, kumekuwa na maendeleo mengi, na wanaobeza wanashangaza mbele ya umma wa Watanzania kwani mengi yanaonekana.


No comments:

Post a Comment