Monday 7 September 2015

MSUKUMA AMWANIKA LOWASSA



 
Na Mwandishi Wetu, Geita

MWENYEKITI wa CCM Mkoa wa Geita, Joseph Musukuma, amesema ataziweka hadharani siri zote za mgombea urais wa CHADEMA, Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond, Edward Lowassa.

Amesema ana ufahamu uozo mwingi wa Lowassa, kwani alikuwa miongoni mwa washauri wake 10, muhimu wakati akitafuta wadhamini ndani ya chama na kwamba mgombea huyo hana sifa na hafai kuongoza nchi.

Mbali na hilo, amewashukia waliokuwa wenyeviti wa chama wa mikoa, Mgana Msindai (Singida) na Hamis Mgeja (Shinyanga), kwamba anawafahamu vilivyo na wanasumbuliwa na maslahi  binafsi na si ya Watanzania.

Musukuma alisema hayo katika mkutano wa hadhara, wakati akimnadi mgombea ubunge Jimbo la Geita, Costantine Kanyasu (CCM), kwenye ufunguzi wa kampeni uliofanyika katika uwanja wa Nyankumbu, mjini hapa.
“Napenda niwaeleze Watanzania, hasa wale waliokuwa hawajui, nilikuwa miongoni mwa washauri 10 muhimu wa Lowassa wakati akitafuta wadhamini ndani ya chama ili  ateuliwe kuwa mgombea urais, namjua na siri zake zote nazijua, wala hakuna kitu ambacho anaweza kukificha,”  alisema huku akishangiliwa na umati mkubwa wa wananchi waliohudhuria mkutano huo.

Alisema miongoni mwa siri anazotarajia kuzitoa hadharani ni pamoja na mpango mkakati uliokuwepo baada ya chama kukata jina la Lowassa kuwa ni kuhakikisha Balozi Amina Salum Ali, anapitishwa kuwa mgombea urais wa CCM.

Msukuma alisema mkakati huo ulipangwa, ili Lowassa ashinde kirahisi akiwa CHADEMA.

“Ni kweli wafuasi wa Lowassa walikuwa wakinihusisha kuwa ni miongoni mwa wenyeviti wa mikoa wa CCM waliotarajiwa kuhama kwenda CHADEMA, najua hata wao walijua mie ningehama kwenda huko,  lakini nimewaambia sihami CCM.

‘’Kwa sababu namfahamu vilivyo Lowassa, hivyo nawasubiri wafuasi wake waropoke, ili niweke siri zake zote hadharani kwa Watanzania wasiojua ukweli, kwani nimekuwa nikihudhuria vikao vyote muhimu vya kimkakati nyumbani kwake kabla hajahama kwenda huko aliko,’’ alisema.

Alisema kiu ya Watanzania katika uchaguzi wa mwaka huu ni kumpata mgombea wa CCM ambaye ni Dk. John Magufuli na kwamba muda wa wapinzani kupewa ridhaa ya kuongoza dola haujafika.

Akizungumzia makada waliohama chama na kujiunga na CHADEMA, Musukuma, ambaye pia ni mgombea ubunge Jimbo la Geita Vijijini, alisema anawasubiri kwa hamu Msindai na Mgeja wafike Geita kuwalaghai wananchi.

Musukuma alisema atajitolea kurusha helikopta angani na kuueleza umma namna Msindai alivyokuwa mzigo ndani ya chama.

“Huyu bwana ni mzigo kweli kweli, wala asiwadanganye Watanzania na kisa cha Mgeja kuhama ni kuwa baada ya binti yake kukosa ubunge, huku akiwa ametumia zaidi ya sh. milioni 30, alizotoa kama rushwa kwa wajumbe”, alisisitiza.

Alisema ana vielelezo vyote, ikiwemo ujumbe mfupi wa maneno aliokuwa akitumiwa na Mgeja na baadhi ya nyaraka zingine muhimu alizokuwa akitumia kuwarekodi pasipo wao kujua.

“Ninazo sms alizokuwa akinitumia na pia ushahidi niliokuwa nawarekodi bila wao kujua,” alisema.

Katika hatua nyingine, Meneja kampeni wa mgombea ubunge jimbo hilo, Ahmed Mbarak, alisema Dk. Wilbroad Slaa ni mcha Mungu anayesimamia ukweli kutokana na hatua yake ya kuamua kujitenga na mafisadi.

Akizungumza katika mkutano huo, aliyekuwa Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, wilayani Geita, ambaye alitangaza rasmi kuhama chama hicho kupitia mkutano huo, Bashiru Ally,alisema vyama vya upinzani hapa nchini, ni mfano wa kampuni za watu binafsi, kwa kuwa Lowassa amevamia kichaka asichokijua.

Kwa upande wake, mgombea ubunge jimbo hilo, Constantine Kanyasu, akiomba kura, alisema anazijua kero nyingi zinazowakabili wananchi wa jimbo hilo, ikiwemo maji na shida wanazopata wachimbaji wadogo wa dhahabu na kwamba baadhi ameanza kuzishughulikia.

Njau amdadavua Sumaye
KADA wa CCM, Victor Njau, ameshangazwa na kitendo cha Waziri Mkuu Mstaafu Fredrick Sumaye, kuungana na Edward Lowassa, wakati alikuwa mstari wa mbele kuhakikisha Lowasa haingii Ikulu kwa njia yoyote ile.
Amesema Sumaye alimtafuta mara kadhaa akitaka kukutana naye ili wapange mpango mkakati wa kuhakikisha Lowassa hafanikiwi katika harakati zake za urais na baada ya mazungumzo ya muda mrefu walikubaliana kukutana jijini Arusha
Njau alitoa kauli hiyo jana katika uzinduzi wa kampeni za Jimbo la Arusha Mjini, zilizofanyika katika viwanja vya Soko Kuu, jijini hapa.
Alisema Sumaye alifunga safari kutoka Dar es Salaam na kuja Arusha kwa ajili ya kuonana naye pamoja na watu wengine ambao hakuwataja.
Kwa mujibu wa Njau, mapema mwaka huu, walikutana na Sumaye katika hoteli ya kitalii ya Naura Spring, iliyopo jijini hapa, chumba namba 206, kupanga mpango mkakati wa kuhakikisha Lowassa haingii Ikulu, lakini cha kushangaza hivi sasa anamkumbatia na kumpamba kwa kila sifa kuwa ni kiongozi anayefaa kuwaongoza Watanzania.
“Nina ushahidi wa kutosha wa maandishi na sauti niliyomrekodi Sumaye akisistiza mambo kadhaa tutakayoyafanya na wenzangu, ili kukamilisha mpango huu kwa namana yoyote ile, lakini leo hii anaambatana naye. Hivi kweli huyu ni mzima au anataka kucheza na akili za Watanzania?” alihoji.
Alisema mara kadhaa Sumaye amekuwa akikaririwa na vyombo vya habari kuwa endapo CCM, ingemteua Lowassa kugombea urais, angehama kwa sababu si msafi na ana tuhuma nyingi.
Njau ambaye ni mwanasheria wa kujitegemea, aliwataka Watanzania kutodanganywa na mafisadi wala rushwa, wenye uroho wa kwenda Ikulu, kwani wakiwachagua watajutia na kuwataka wananchi kumchagua Dk. John Magufuli kuwa rais wa awamu ya tano.
“Ndugu zangu, tusimchague Lowassa, ana uroho wa madaraka… tumchague Dk. Magufuli kwa kuwa ni mchapa kazi na kazi zake alizozifanya zinaonekana kwa macho. Mafisadi wala rushwa wenye uchu wa madaraka tusiwape nafasi ya kwenda Ikulu kwa kuwa hatujui lengo lao nini,” alisema.
Kuhusu Godbless Lema, aliwataka wananchi wa Arusha kutomchagua kwa kuwa ni tapeli na anatafuta nafasi hiyo kwa ajili ya maslahi binafsi.
Alisema aliahidi kujenga machinga Complex, lakini mpaka sasa hakujenga wala hakuna hata kiwanja alichonunua kwa ajili ya ujenzi huo.
Njau alisema watamwuunga mkono mgombea wa CCM, watafanya kampeni kila kona usiku na mchana, kuhakikisha mgombea huyo anapata ushindi mkubwa.

No comments:

Post a Comment