Sunday 6 September 2015

SAMIA AFUNGA KAZI JIMBO LA UKONGA, ASEMA MAFURIKO YA MVUA NI NDOTO

Mgombea mwenza wa urais Samia Suluhu Hassan akihutubia umati wa wananchi katika mkutano wa kampeni uliofanyika Majohe, Jimbo la Ukonga, Dar es Salaam
Wananchi wakinyoosha mikono juu kufurahia hotuba iliyotolewa na mgombea mwenza wa urais, Samia Suluhu Hassan
Mgombea ubunge wa jimbo la Ukonga, Jerry Silaa akiomba kura kwa wananchi wakati wa mkutano huo
Umati wa wananchi uliofurika kwenye mkutano huo uliofanyika Majohe, Ukonga, Dar es Salaam.
Baadhi ya wasanii wa filamu na muziki wa kizazi kipya wakiwa kwenye mkutano huo
Msanii maarufu wa filamu nchini Wema Sepetu akisalimiana na mgombea mwenza wa urais, Samia Suluhu Hassan
Mgombea mwenza wa urais Samia Suluhu Hassan akiteta jambo na mgombea ubunge wa Jimbo la Ukonga, Jerry Silaa
Mgombea ubunge wa jimbo la Segerea akiomba kura kwa wananchi wakati wa mkutano huo


EPSON LUHWAGO NA MARIAM MZIWANDA
TATIZO la mafuriko katika Jiji la Dar es Salaam, litapatiwa ufumbuzi wa kudumu kutokana na kuwepo kwa mpango kamambe ulioandaliwa wa kuzibua mitaro kuelekea baharini.
Sambamba na mpango huo, serikali ijayo ya CCM itajenga hospitali kubwa Kibamba, ili kutoa huduma bora. Pia inatarajia kupanua Hospitali ya Palestina iliyoko Sinza, ambayo itakuwa ya wilaya mpya ya Ubungo.
Hayo yalisemwa juzi na mgombea mwenza wa urais wa CCM, Samia Suluhu Hassan, katika mikutano ya kampeni iliyofanyika Mbezi Mwisho na Mburahati Barafu, jijini Dar es Salaam.
Alisema jiji la Dar es Salaam limekuwa likikumbwa na mafuriko mara kwa mara kutokana na kuziba kwa mitaro ya maji kwenye maeneo mbalimbali, hivyo serikali imeliona na italifanyia kazi.
“Wananchi wamekuwa wakiathiriwa na mafuriko mara kwa mara ambayo husababisha pia magonjwa ya mlipuko. Sasa kuna mpango kamambe wa kuzibua mitaro yote na kuelekeza maji kwenye Mto Ng’ombe hadi baharini.
Pia mitaro yote itazibuliwa kwa ajili ya kupeleka maji kwenye mito na kuielekeza baharini,” alisema.
Aliongeza kuwa: “Dar es Salaam ni jiji la pili kwa ukubwa Afrika kwa maendeleo, lakini sifa yake kubwa ni uchafu. Tutalisimamia kwa karibu suala hili na kuhakikisha uchafu ndani ya jiji hili unabaki historia,” alisema. 
Kuhusu afya, alisema serikali ijayo ya CCM itajenga hospitali kubwa na ya kisasa ambayo itatoa huduma kwa saa 24 na kupunguza adha kwa wakazi wengi wa jimbo la Kibamba kwenda kufuata huduma kwenye hospitali ya Tumbi, Kibaha.
Alisema hospitali hiyo kubwa na kisasa itawezesha watu kupata huduma bora na za uhakika pindi itakapokamilika na pia kupunguza adha za kufuata huduma Tumbi na hata Muhimbili.
“Ndugu zangu, nawahakikishia kuwa hospitali hii kubwa na ya kisasa itajengwa. Tuchagueni ili tuingie madarakani tuifanye kazi hii,”alisema katika mkutano uliofanyika Mbezi Mwisho.
Naye mgombea ubunge wa jimbo la Kibamba, kupitia CCM, Dk. Fenella Mukangara, alisema kuna mpango pia wa kujenga vituo vitatu vya afya ambavyo vitachangia kutoa huduma na kupunguza tatizo hilo.
Akiwa katika mkutano wa jimbo la Ubungo, eneo la  Mburahati, Samia alisema serikali ya awamu ya tano ya CCM inatarajia kupanua hospitali ya Sinza Palestina ili kuwa ya ngazi ya wilaya, baada ya kuanzishwa kwa wilaya mpya ya Ubungo.
Sambamba na hilo, alisema vituo vya afya vilivyoko katika wilaya nzima ya ubungo vitaboreshwa kuhakikisha huduma za uhakika zinapatikana kwa saa 24.
“Kituo cha afya cha Mburahati kinafanyiwa ukarabati mkubwa kwa ushirikiano baina ya Manispaa ya Kinondoni na JICA (Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan). Kazi hii ikikamilika huduma bora na za kisasa zitapatikana,” alisema.

AWAZODOA WAPINZANI
Samia alisema wapinzani wamekuwa wakidai kuwa CCM haijafanya chochote wakati wanapita kwenye barabara za lami za CCM na kupata huduma ambazo zimepatikana kutokana na  utekelezaji wa Ilani za Uchaguzi za CCM.
“Hawa wanaosema hatujafanya kitu tunawashangaa sana. Magari yao yanapita kwenye barabara zilizojengwa na CCM. Wanatibiwa kwenye hospitali zilizo chini ya serikali za CCM. Wao wamefanya nini? Wapuuzeni watu hawa,”alisema.
Akiwa katika jimbo la Kibamba, alimtumia salamu mgombea wa CHADEMA, John Mnyika, kuwa ajiandae kufungasha virago kwa sababu hana chake tena.
Alisema Mnyika atapigwa na mwanamke (Dk. Fenella) kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu, kwa kuwa CCM imejipanga kuwaletea wananchi wa Kibamba maendeleo.
Kuhusu barabara, Samia alisema Ilani ya Uchaguzi wa CCM imeweka bayana mpango wa kujenga barabara kadhaa kwa kiwango cha lami, ili kurahisisha usafiri na kupunguza msongamano.
Kwa mujibu wa Ilani, baadhi ya barabara kuwa ni Mbezi-Malamba Mawili- Kinyerezi hadi Banana (likomita 14); Tegeta Kibaoni- Wazo- Goba- Mbezi Mwisho (kilomita 20); Tangi Bovu hadi Goba (kilomita 5.2 kati ya tisa); Kimara Baruti- Msewe- Changanyikeni (kilomita 2.6); na Kimara Kilungule hadi External (kilomita 8.8 kati ya tisa).
Zingine ni Kigogo round abaout- Bonde la Msimbazi- kona ya Twiga/Msimbazi (kilomita 0.5 kati ya 2.7); Tabata dampo hadi Kigogo (kilimota 1.6 kati ya kilomita 2.25); na Kibamba- Mlonganzila (kilomita nane kati ya 12).         

No comments:

Post a Comment