Saturday 10 October 2015

BANDARI KUBWA KUJENGWA MWAKANI ZANZIBAR




Na Hamis Shimye, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema ujenzi wa bandari mpya eneo la Mpigaduri, Unguja, utaanza mapema mwakani.
Amesema fedha za ujenzi wa bandari hiyo ziko mbioni kupatikana kutoka Benki ya Exim ya China, ambayo imeonyesha nia ya kuikopesha serikali dola milioni 222 (takriban sh. bilioni 490).
Mbali na kuanzwa kujengwa kwa bandari hiyo, Dk. Shein pia amesema atajenga bandari ya Wete, Pemba na kuiboresha bandari ya Mkoani iliyoko pia kisiwani humo.
Dk. Shein aliyasema hayo kwenye uwekaji wa jiwe la msingi katika  Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amaan Karume. Uwanja  huo unajengwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) kwa mkopo kutoka China.
Alisema serikali yake imepanga mambo mbalimbali kuhakikisha inaboresha miundombinu kwa kuwa bila miundombinu imara hakuna maendeleo bora.
"Ujenzi wa bandari hiyo si suala la jana au leo, bali lilianza toka kwa Mzee wetu Dk. Salmin Amour ambaye alitaka kujenga bandari eneo hilo. Sasa ndoto hiyo imekamilika na ujenzi utaanza mwakani,''alisema.
Alisema alipokutana na Rais wa China, Xi Jinping, alimwomba kujenga bandari hiyo na kukubali na tayari kuna kampuni ilishafanya upembuzi yakinifu.
Dk. Shein alisema anaamini bandari hiyo itakapokamilika itasaidia kuongeza mapato ya Zanzibar kwa kuwa itakuwa na uwezo mkubwa wa kubeba watu na itaendana na ushindani wa kimataifa.
"Tumenuia pia kujenga bandari ya Wete kupitia mwekezaji wa ndani, ambaye tayari ameshapatikana na muda ukifika ataanza ujenzi huo huku pia bandari ya Mkoani nayo ikiendelea kuboreshwa,” alisema.
Kwa mujibu wa Dk. Shein, ujenzi wa bandari hiyo unatokana na bandari iliyoko Malindi kuwa ndogo na kunahitajika kujengwa kubwa yenye uwezo wa kupokea na kusafirisha wageni pamoja na mizigo.

Usafiri wa ndege Pemba
sasa kufanyika pia usiku

WANANCHI wa Pemba na Unguja wataanza kusafiri kwa ndege usiku katika kiwanja cha ndege cha Pemba, baada ya miezi miwili kukamilika kwa uwekaji wa taa kwenye kiwanja hicho.
Pia uwanja huo ndani ya muda mfupi utajengwa zaidi na kuwa wa kisasa kwa kuboresha na kupanua njia za kurukia ndege na utuaji ili kusaidia ndege nyingi kutua kwa wakati.
Ahadi hiyo ilitolewa jana na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, ambaye pia ni mgombea wa Urais wa CCM Zanzibar, ambapo alisema amenuia kukoboresha kiwanja hicho na kuwa na cha kisasa.
Alisema hivi sasa ndege nyingi haziwezi kutua usiku kwenye kiwanja hicho, hivyo ukarabati na uwekaji wa taa umeshaanza na kuahidi kuwa  ndani ya miezi miwili kila kitu kitakuwa vizuri.
"Nawaambia ndugu zangu wa Pemba na Unguja, sasa mtaweza kutua na kusafiri kwa ndege hata usiku kwenye kiwanja chetu cha ndege cha  Pemba kwa kuwa ujenzi wake unakaribia kwisha,” alisema.
Dk. Shein alisema licha ya kuweka kwa taa hizo kwenye kiwanja hicho, pia ujenzi wa kiwanja cha kisasa cha ndege cha Pemba nao utafanyika.

No comments:

Post a Comment