Wednesday 7 October 2015

DK. MAGUFULI AFUNGA KAZI, AVUNJA NGOME ZA UKAWA K'NJARO



 
Mgombea urais wa CCM, Dk. John Magufuli akihutubia wananchi katika mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye uwanja wa Mashujaa mjini Moshi.
Dk. Magufuli akimpongeza mama huyo aliyeamua kujiondoa CHADEMA na kujiunga na CCM wakati wa mkutanowa kampeni
Hii ni sehemu ya umati wa wananchi waliohudhuria mkutano wa kampeni wa DK. Magufuli mjini Moshi
 
Maelfu ya wananchi wa mji wa Moshi wakimsikiliza Dk. Magufuli alipokuwa aiwahutubia
Moshi sasa ni ya CCM. Hivi ndivyo hali ilivyokuwa jana

MGOMBEA urais wa CCM, Dk. John Magufuli, amezisambaratisha ngome za kundi la UKAWA katika mikoa ya Arusha na Kilimanjaro, huku akiahidi kuongoza serikali yenye watendaji waadilifu na wachapakazi.

Aidha, amesema atawachukulia hatua kali watendaji wa serikali, watakaowahamisha wafanyabiashara wa soko la Memorial katika Manispaa ya Moshi kuwapeleka eneo lingine ambalo linamilikiwa na kigogo wa CHADEMA.

Aidha, Dk. Magufuli amekiri kuwa Watanzania wapo tayari na wanaunga mkono dhamira yake ya kuleta mabadiliko ya kweli nchini, ambapo umati uliofurika kwenye mkutano wake wa kampeni mjini Moshi ni ishara tosha.

Pia, amesema kwa hali ilivyo, anachosubiri kwa sasa ni kuapishwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano kwani, tayari watu wameshafanya uamuzi sahihi na kuwaahidi kuwa atatatua kero zote zinazowakabili wakazi wa Moshi.

“Nasema kama ni mkuu wa mkoa, wilaya au viongozi wengine wa Halmashauri, natoa tamko leo kwa sababu mimi ndiye Rais nitakayefuata, wafanyabiashara wa soko la Memorial, wasiondolewe. Atakayekiuka agizo hili, nitamtimua mapema kabisa,” alisema Magufuli.

Aidha, katika mkutano huo Mjumbe wa Kamati ya Ushindi ya CCM, Christopher Ole Sendeka, aliwataka watanzania kuwa makini na mgombea urais wa CHADEMA, Edward Lowassa, kwani ni laghai na amelikana kabila lake kwa ajili ya kupata madaraka.

Kwa mujibu wa Ole Sendeka, Lowassa anatoka kwenye kabila la Wameru, lakini aliamua kulikana na kujipachika umasai ili kuweza kupata fursa ya kupata madaraka, jambo alilosema ni hatari na usaliti mkubwa.

VIWANDA
Akizungumzia suala la viwanda vingi kushindwa kuzalisha, Dk. Magufuli ametoa siku zilizobaki kuvifufua ili viweze kufanya kazi kama ilivyokuwa awali.

Alivitaja viwanda hivyo kuwa ni kile cha magunia, ngozi na kile cha Kilimanjaro Machineries Tools ambavyo kwa sasa havifanyi kazi.

Alisema kusimama huko kunaufanya uchumi wa Moshi kushindwa kusonga mbele kwa vijana kukosa ajira na serikali kupoteza mapato ambayo yangesaidia kufanya maendeleo.

“Kwa siku hizi zilizobaki, wawekezaji wahakikishe viwanda walivyopewa wanavifufua, vianze kufanya kazi kabla sijaapishwa. Wasipofanya hivyo, nitawanyang’anya na kuvirejesha serikalini,” alisema Dk. Magufuli.]

Alisema kitendo cha jimbo la Moshi Mjini kuongozwa na upinzani kwa miaka 20, ndiyo sababu kubwa ya maendeleo kuchelewa ikilinganishwa na maeneo mengine yenye wabunge wa CCM.

Dk. Magufuli alisema Halmashauri ya Moshi Mjini inayoongozwa na Chadema, imekuwa ikishindwa kutoa mikopo kwa kinamama na vijana licha ya kukusanya mapato ya sh. bilioni tatu kwa mwaka.

“Niambieni wenyewe kinamama mmeshawahi kupata mikopo kutoka katika Halmashauri au nyie vijana. Huu ni wakati wa mabadiliko, vizuri kufikia uamuzi wa kusema yatosha,”alisema.

ARDHI
Kama alivyoahidi katika maeneo mengine, Dk Magufuli alisema atahakikisha serikali yake inasimamia haki za ardhi na kuzuia mianya ya rushwa kwa wanaotoa maeneo.

“Watu wakitaka viwanja, hawapati mpaka kutoa rushwa, hili nitalisimamia kikamilifu kwa kuzingatia sheria ya ardhi na mipango miji kwa maana hata waliobomolewa kufuatia upanuzi wa barabara, fidia yao watapewa,”alisema.

KAHAWA
Dk. Magufuli alisema serikali yake itakuwa rafiki kwa
wakulima na wafugaji ili waweze kujipatia vipato vyao.

Alisema anafahamu kuwepo kwa kodi zisizo na msingi katika zao la kahawa, atazifanyia kazi kuziondoa au kuhakikisha zinapungua ili bei ya zao hilo imnufaishe mkulima.

“Mimi ni rafiki wa wakulima na wafugaji, nataka walime na kufuga kweli. Hivi vikwazo vinavyosababisha bei ya kahawa inakuwa chini, serikali yangu itaviangalia,” alisema.

OLE SENDEKA
Ole Sendeka amewataka wakazi wa Moshi na Watanzania kwa ujumla, kumpa kura za ushindi Dk. Magufuli kwa sababu ni kielelezo cha uadilifu na uchapakazi.
Alifichua kuwa Lowassa alikana kabila lake halisi ili aweze kuchaguliwa kuwa mbunge wa Monduli.

Alisema anamfahamu Lowassa kwamba amezaliwa kutoka katika kabila la Wameru, lakini aliamua kuwadanganya Wamasai kwamba, naye ni kabila hilo ili aweze kupata ubunge.

Alisema Dk. Magufuli ndiye rais anayefaa kwa sababu, tayari mikoa 21 aliyofanya kampeni, watanzania wameamua hivyo.

NCHIMBI
Naye mlezi wa mkoa wa Kilimanjaro, Dk. Emmanuel Nchimbi,  aliwahakikishia watanzania kwamba kamwe hawezi kuihama CCM na wanaomzushia wanamkera sana.

“Nazushiwa ninataka kuihama CCM, nataka kuwaambia wanaovumisha hivyo, wananikera. Siwezi kushuka kwenye gari la kisasa nikaenda kupanda kigari kibovu,” alisema Dk. Nchimbi.

OLE SILANGA
Aliyekuwa mjumbe wa Baraza Kuu la Chadema aliyehamia CCM, Ole Silanga, alisema chama hicho cha upinzani ni cha kinafiki kwa sababu anakifahamu usanii wake mwanzo mwisho.
Alisema kwa sababu ya usanii wao, anaamini mwisho wa Lowassa na Chadema kwa ujumla umefika, watanzania watakapomchagua Magufuli kuwa rais wa Tanzania.
“Chadema ni wanafiki, unajua hata siri ya kutumia helkopta kwenye kampeni ni kuwakwepa akina mama wajawazito, wasiwaombe msaada barabarani,” alisema.

Alisema Lowasa amekuwa chanzo cha matatizo mengi katika jimbo la Monduli, mojawapo ni mradi wa malambo na majosho ambayo yalikuwa yakitumiwa na ng’ombe zake tu.

Alisema hata mradi wa maji Monduli Juu, uliogharimu kiasi cha sh. bilioni tatu, haupo na kwamba, kuna mengi ambayo hayana faida wala manufaa yoyote kwa watanzania.

WANACHAMA WARUDISHA KADI
Kama ilivyokuwa kwa Arusha na Monduli, baada ya Dk. Magufuli kumaliza kuhutubia, mafuriko ya wanachama na wafuasi wa CHADEMA kurudisha kadi na kupewa na CCM yalianza.
Miongoni mwa waliorudisha kadi hizo, wapo Katibu na Mwenyekiti wa Vijana wa wilaya, pamoja na wanachama wa vyama vingine.

Magufuli ambaye muda mwingi alikuwa akishangiliwa Rais… Rais.. Rais… aliwaomba wananchi kutofanya makosa, wamchague aliongoze Taifa kwa awamu ya tano.



ATIKISA NGOME YA MBOWE
Wakati UKAWA wilayani Monduli wakiendelea kuuguza majeraha ya kuondokewa na vigogo wake waliohamia CCM, bado mambo yamekuwa mabaya zaidi katika Jimbo la Hai, ambako ni ngome ya Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe.

Jana, Dk. Magufuli alifanya mkutano mkubwa wa kampeni katika jimbo hilo uliofanyika viwanja vya Boma Ng'ombe, ambako alilakiwa na maelfu ya watu waliokuwa wakimsubiri wakati akitoka Siha.
 
Hata baada ya kuingia katika viwanja hivyo, watu walizidi kumiminika bila kujali kama hakuna nafasi ya kuweza hata kunyanyua mguu huku Dk. Magufuli akishangazwa na umati huo na kuahidi kuwatumikia kwa uadilifu mkubwa.

Mbali ya mapokezi hayo makubwa ya kutisha, wanachama zaidi ya 100 walirudisha kadi za CHADEMA na kujiunga na CCM, akiwemo aliyekuwa Katibu wa CHADEMA wa Wilaya ya Hai, Goodluck Lema.

"Kwa akili zangu timamu, nimeamua kujiunga na CCM, baada ya kufuatilia kwa karibu kampeni za Dk. Magufuli. Nimetumika sana bila faida, nimeamua kwa ridhaa yangu,” alisema Lema.

Akiizungumzia Hai, Dk. Magufuli alisema wilaya hiyo imechelewa kwa maendeleo ikilinganishwa na Siha kutokana na kuongozwa na wanasiasa wasiopenda maendeleo ya watu bali kujali yao binafsi.
 
"Hai ni wilaya ya zamani zaidi kuliko Siha kwa sababu ni kiungo kwa kila aendae Arusha na maeneo mengine. Wilaya hii haikupaswi kuwa hivi,” alisema.

Alisema Mbowe, ambaye ameliongoza jimbo hilo, muda mwingi amekuwa akisafiri na kuishi Dar na kutalii maeneo mengine huku akisahau majukumu yake.

"Mambo mengine mmeyasababisha wenyewe. Mlifanya makosa kumchagua mtu ambaye hajui namna ya kutatua kero zenu, muda wote anatalii tu.

"Mbowe ni rafiki yangu kweli, lakini katika masuala ya maendeleo sina mchezo kabisa, hafahamu kero na shida zinazowakabili yule. Nawaomba mfanye mabadiliko sasa kwa kuwachagua wagombea wa CCM,” alisema.

Dk. Magufuli amemshauri Mbowe abaki na wadhifa wa Uenyekiti wa CHADEMA pekee yake, aachane na ubunge kwani ni majukumu ambayo kimsingi, hawezi kuyatekeleza kwa ufanisi.  Alisema kwa kuendelea kubaki kuwa Mwenyekiti wa CHADEMA, ataweza kukijenga chama hicho.

Akizungumzia changamoto zilizopo Hai, Dk. Magufuli alisema anataka kiwanda cha Kilimanjaro Machines Tools, mwekezaji wake akifufue kianze uzalishaji kwani, kusimama kunaathiri soko la ajira kwa vijana katika sekta mbalimbali.

"Huyo mwekezaji ahakikishe kiwanda hicho kinaanza kazi mara moja, akishindwa kitarudi serikalini haraka,” aliongea Dk. Magufuli.

Kuhusu ardhi, Dk. Magufuli alisema anafahamu yapo matatizo ya mashamba, ameahidi kuyashughulikia kwa majibu wa sheria za ardhi.

Pia, alisema matatizo ya maji, umeme na barabara za mitaani atazitatua kwa sababu anaamini akiziba mianya ya mafisadi, Watanzania wanyonge watanufaika.

Akiwa jimboni Siha, mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Emmanuel Nchimbi alisema serikali ya awamu ya tano, haitaki rais nyoronyoro.

Alisema anayefaa ni Dk. Magufuli, ambaye atasimamia rushwa na kuondoa mfumo mbaya wa kupiga dili.

"Hatutaki uzembe, serikali ya Magufuli wananchi wana imani nayo, tusubiri mabadiliko yenye manufaa kwa Watanzania,” alisema Nchimbi.

No comments:

Post a Comment