Friday 9 October 2015

LOWASSA ASIYUMBISHE FAMILIA YA SOKOINE





Na Tito Msemakweli
“NI kweli nilimshawishi Namelock agombee ubunge kwa tiketi ya CCM, lakini mambo yalipobadilika nilimshauri ajitoe. Kama CCM hainitaki kwqa nini yeye abaki?” Hiyo ni kauli ya mgombea urais kwa tiketi ya Chadema chini ya mwavuli wa Ukawa, Edward Lowassa.

Ni kauli aliyoitoa kwa wananchi wa Monduli alipowahutubia juzi akiwaomba kura ili apate ridhaa ya kuingia Ikulu na kuwa rais wa tano wa Tanzania; akijieleza pia kwa wana chi hao baada ya Namelock kumkatalia ombi lake hilo akimsifu kuwa ni binti msikivu.

Namelock ambaye ni binti wa Waziri Mkuu wa zamani, marehemu Edward Sokoine aliamua kushikilia msimamo wake wa kutaka kumrithi Lowassa kwenye kiti cha ubunge wa Monduli kwa tiketi ya CCM, ingawa kwa sasa Waziri Mkuu huyo aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond ameonekana kumkasirikia.

“Kama mtu amebaki CCM mimi nifanye nini?” Alihoji na kusema sasa atamwombea kura Julius Karanga ambaye anagombea nafasi hiyo kwa tiketi ya Chadema, chama kilichompokea Lowassa na kumpachika kugombea urais bila kufuata utaratibu wa kidemokrasia.

Ni dhahiri, kuwa Lowassa ameumbuka kwa Namelock, binti ambaye awali alimheshimu na kumsikiliza kwa mambo mengi akiwa kada wa CCM na mbunge wa Monduli, Waziri na Waziri Mkuu, lakini alipomwona mzee huyo amekengeuka akamwacha aende zake.

Lowassa ambaye anajiona kuwa mlezi wa familia ya Sokoine, amekuwa akijipa madaraka makubwa ya kutaka kuiendesha familia hiyo ikiwa ni pamoja na kuwachagulia wanafamilia maisha ya kufuata, mojawapo likiwa hilo la Namelock ambaye amemshitukia.

Inasikitisha kuwa Waziri Mkuu mwingine mstaafu, Frederick Sumaye, anamuunga mkono mgombea wake huyo ambaye anampigia debe usiku na mchana kwa kutoa kauli sawa na hiyo iliyojaa ubaguzi kwamba:

“Wale watu wa Monduli ambao walikuwa wanamfuata Lowassa na sasa hivi hawako naye, hawawezi kuwa watu wake. Kama mtu amebaki CCM si mtu wa Lowassa hata kama alikuwa anamsaidia kisiasa.”

Mpiga debe huyu anafanya kila juhudi kuhakikisha Lowassa anakosana na hata ndugu zake na wafadhili wake, kwa sababu tu hawako pamoja ndani ya Chadema au Ukawa, huku akihanikiza kuwa walioko CCM wabaki na Magufuli (Dk John) kwa kuwa Lowassa hana mtu CCM! Hivi ni kweli?

Ingekuwa kweli mbona wanaendelea kurubuni watu kwa kauli za kimtaani za ‘Toroka Uje’ wakimtumia mwanasiasa mwingine mchovu, Hamis Mgeja ambaye anaamini kwamba CCM ilikuwa mali ya ‘mkata pumzi’ Kingunge Ngombale-Mwiru ambaye ametoroka na kwenda Chadema.

Wakati Magufuli anahubiri kuwa atakuwa kiongozi wa watu wote bila kujali tofauti za kiitikadi, kidini na kikabila, Lowassa na Sumaye wanaamini kwamba wasio Chadema na Ukawa si watu wao na hivyo hawatawaongoza. Huku ni kufilisika kifikra na kisiasa.

Namelock ambaye alikuwa karibu sana na familia ya Lowassa, ameonesha msimamo wa marehemu baba yake wa kukataa kurubuniwa na kushawishiwa kwa ‘Big G za kuazima’ na kuamua kubaki ndani ya chama kilichomlea baba yake mpaka akapoteza maisha kwa ajali ya gari akiwa mtu maarufu ndani na nje ya nchi.

Heshima kama hiyo wameikataa akina Kingunge, Lowassa na Sumaye, ambao wameamua kujitoa mhanga kutafuta madaraka kwa njia yoyote ile, ili mradi wahakikishe mwisho wa siku wanaingia Ikulu kuendeleza ufisadi waliokuwa wakiufanya.

Namelock amekataa kuingia kwenye tandabui la makandokando yasiyoeleweka yaliyogubikwa na uporaji ardhi za wakulima, uingizaji nchini kampuni hewa za kuzalisha umeme, uporaji zabuni za maeneo ya maegesho na stendi Dar es Salaam na kujinasibu kusaidia wananchi kuondokana na umasikini huku wakiwaibia.

Wapo wengi wanaorubuniwa na wapambe wa Lowassa na Ukawa kwa jumla ili wavihame vyama vyao na kujiunga na Ukawa, ili eti wasaidie kuing’oa CCM madarakani kama ambavyo amekuwa akijinasibu Sumaye katika mikutano ya hadhara ya kumzungumzia Lowassa ambaye anaonekana kuanza kupoteza kauli.

Sumaye ambaye amekuwa kama fisi anayenyemelea mkono wa binadamu udondoke aukwapue, anafanya jitihada za makusudi za kuhakikisha walioko karibu na Lowassa hawaendelei kuwa pale, ili likitokea la kutokea hata kama ni baada ya miaka mitano neema iwe kwake. 

Ndiyo maana ya kauli ya : “Kama mtu amebaki CCM si mtu wa Lowassa hata kama alikuwa anamsaidia kisiasa,” ambayo ilipaswa kutolewa na Lowassa mwenyewe na si mpambe, mpiga debe au mshenga awayeyote.

Lowassa alitaka kumfanya Namelock awe kama Fred mwanawe ambaye alimwamuru siku ya kwanza alipojiunga anChadema naye apewe kadi sambamba na wanawe wengine na mkewe ambaye inasemekana alimkubalia kwa shingo upande.

Wapo wana CCM wengi ambao walifuatwa na kundi la Lowassa kushauriwa kumfuata, lakini wengi wao walikataa baada ya kumeona Lowassa wa sasa si yule aliyekuwa CCM, ambaye alikuwa na fikra na uamuzi binafsi tofauti na sasa ambapo fikra na uamuzi anaazima kutoka kwa akina Sumaye na Freeman Mbowe.

Kutokana na hali hiyo, si rahisi kwa mtu timamu anayejitambua na kuelewa analolifanya, kukubali kurubuniwa au kushawishiwa kujiunga na kambi ya mtu ambaye hana mwelekeo wa kisiasa, achilia nmbali uwezo wa kuongoza Taifa kutokana na udhaifu alionao kiafya.

Wengi wanaojiunga kwa Lowassa ni wanaokumbwa na upepo na mawimbi bila kujua yanawafikisha wapi, lakini ni hao ambao hata wanapoondoka CCM  hawaachi pengo na hata huko waendako hawasaidii chochote na ndiyo sababu wamebaki kuwa maboya na mavuvuzela wa mgombea.

Wako wapi akina John Guninita, Lawrence Masha, Mgana Msindai, Tambwe Hiza, Makongoro Mahanga,  James Lembeli, Goodluck ole Medeye?  Wameongeza nini kwenye Ukawa? Walirubuniwa na kuahidiwa nafasi lakini hakuna lolote ingawa baadhi yao wanawania ubunge ambao hawataupata kwa ridhaa ya wananchi. 

Walidhani wanafuata nyuki kupata asali lakini wataambulia manundu.

No comments:

Post a Comment