Monday 16 November 2015

CCM YASHINDA UBUNGE LULINDI, BWANAUSI AIGALAGAZA UKAWA




Na Clarence Chilumba, Masasi
WANANCHI wa Jimbo la Lulindi, Masasi mkoani Mtwara, wamemchagua Jerome Bwanausi (CCM), kuwa mbunge wa jimbo hilo baada ya kupata kura 17,715, sawa na asilimia 87.04.
Katika uchaguzi huo, Bwanausi amemshinda kwa mbali Modesta Makaidi wa chama cha NLD, aliyepata kura 1,638, sawa na asilimia 8.05.
Akitangaza matokeo hayo jana, Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo hilo, Beatrice Dominick, alisema jumla ya wananchi 59,027, walijiandikisha katika daftari la kudumu la wapigakura huku watu 20,580, sawa na asilimia 34.87, walijitokeza kupiga kura.
Beatrice alisema kura halali katika uchaguzi huo zilikuwa 20,552, kura zilizoharibika ni 228, huku idadi ya wapigakura ikipungua kutokana na wananchi wengi kutojitokeza kwenye zoezi hilo la upigaji kura.
Alisema Bwanausi alipata kura 17,715, sawa na asilimia 87.04, Modesta Makaidi wa chama cha NLD, alipata kura 1,638, sawa na asilimia 8.05.
Wagombea wengine ni Amina Mshamu wa CUF aliyepata kura 714, sawa asilimia 3.51 na Francis Ngaweje wa ACT- Wazalendo, akiambulia kura 285, sawa na asilimia 1.40.
Akizungumzia kuhusu matokeo ya udiwani katika jimbo hilo, alisema kata zote zilinyakuliwa na CCM na kwamba Rais Dk. John Magufuli, alipata kura 31,603 sawa na asilimia 71.28.

No comments:

Post a Comment