Tuesday 3 November 2015

MAANDAMANO YA CHADEMA YAYEYUKA, VIJANA WASEMA WAMECHOKA KUTUMIWA




NA PETER KATULANDA, MWANZA
MAANDAMANO ya uchochezi na uvunjifu wa amani yaliyopangwa  kufanyika jana na CHADEMA mkoani hapa, sambamba na mikoa mingine nchini, ‘yameyeyuka’ baada ya polisi kuimarisha ulinzi kila sehemu.
Kwa mujibu wa baadhi ya wafuasi wa chama hicho waliozungumza na mwandishi wa habari hizi kwa masharti ya kutotajwa majina, mbali na polisi kuyazuia na kuimarisha ulinzi, wameshtuka kutumiwa ovyo na viongozi wao.
“Uchaguzi umemalizika, tunapaswa kuangalia maisha yaliyo mbele yetu, hivyo viongozi wanaotuhamasisha kuandamana tumewaambia waje waongoze maandamano hayo, siyo kututumia kuandamana wakati wao wako majumbani kwao,” alisema kiongozi mmoja wa CHADEMA wa Igoma.
Mfuasi mwingine wa chama hicho aliyekuwa katika kituo cha mabasi yaendayo mikoani cha Nyegezi jijini hapa, alisema viongozi walioandika barua polisi kuomba kuandamana ili kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu uliomweka madarakani Rais Mteule Dk. John Magufuli , wana matatizo ya akili kama si kutaka watoto wa wengine wauawe.
“Kweli tulijaribu kutaka kukusanyana asubuhi maeneo haya ya Nyegezi, lakini kwa hali tuliyoona polisi walivyokuwa wamejipanga, nimewashauri wenzangu tuachane nayo, vinginevyo wanaotaka tuandamane waje mstari wa mbele tufe au kuishia gerezani wote,” alisema mfuasi huyo.
Mwingine aliyedai ni dereva wa daladala ziendazo Igoma-Buhongwa, alisema vijana watakaoandamana wajue kuna kupoteza uhai na viungo iwapo watazua vurugu na kwamba vitendo kama hivyo vinawakera wananchi wengi ndiyo maana chama hicho kimenyimwa kura na kupoteza majimbo ya Nyamagana na Ilemela.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza, Charles Mkumbo, alisema hadi nyakati za mchana hakukuwa na wafuasi wa CHADEMA waliokuwa wameandamana na kwamba jeshi lake lilikuwa limejipanga kukabiliana na maandamano hayo na litaendelea kufanya hivyo.
“Maandamano yoyote lazima yawe na maudhui, haya ni uchochezi, shari na uvunjifu wa amani. Yangekuwa maandamano ya heri, tungeyapa ulinzi, lakini maudhui yake ni kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wakati sheria za uchaguzi zipo na zinapaswa kuchukuliwa, siyo maandamano,” alisema Mkumbo.
Bila kutaja majina, alisema viongozi wa CHADEMA wa wilaya za Nyamagana na Kwimba, walipeleka barua za kuomba kuandamana sambamba na maeneo mengine ya nchi kama ilivyolipotiwa katika vyombo vya habari, lakini waliwakatalia na kuonya wasithubutu kufanya hivyo.
Kamanda huyo amewapongeza wafuasi wa chama hicho, hasa vijana, ambao ndiyo walengwa wa maandamano hayo, kutii amri bila shuruti na kuwataka waendelee kujenga uchumi wa nchi na kuinua vipato vyao kwa amani.
Alisema jeshi lake lipo kwa ajili ya kulinda usalama wa raia wote pamoja na mali zao, hivyo washirikiane na Watanzania wengine kudumisha amani.

No comments:

Post a Comment