Wednesday 4 November 2015

SITTA AJITOSA TENA KUWANIA USPIKA




HATIMAYE Spika wa zamani wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samuel Sitta, amevunja ukimya na kutangaza rasmi kuwa wakati wa mchakato wa kinyang’anyiro cha Spika wa Bunge la 11, atawania nafasi hiyo.
Sitta, amekuwa kada wa kwanza wa CCM kutangaza rasmi kuingia katika mchuano wa kuwania nafasi hiyo nyeti.
Habari kutoka miongoni mwa wasaidizi wa Sitta, zimesema spika huyo wa zamani ameamua kuwania nafasi hiyo kutokana na uwezo na uzoefu alionao wa kuendesha Bunge.
Msaidizi huyo alisema Sitta anaamini kuwa uwezo wake aliouonyesha katika kuendesha Bunge la Tisa (mwaka 2005 hadi 2010), akitumia kauli mbiu yake ya 'Spika wa kasi na viwango’, itamfanya aendane na kasi ya utendaji wa Rais Mteule, Dk John Magufuli.
Alisema Sitta ameahidi akichaguliwa kuwa Spika wa Bunge la 11, atasimamia suala la Muungano na Umoja wa Taifa bila kuyumba.
Kuhusu Katiba mpya, alisema ameahidi atasimamia na kuukamilisha mchakato wa Katiba Inayopendekezwa  kwa ufanisi na atasimamia ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi kwa ajili ya uchumi bora wa viwanda, kilimo, huduma na mauzo nje.
Sitta alijizolea sifa nyingi wakati akiwa Spika wa Bunge la Tisa, ikiwamo Bunge hilo kufanyia marekebisho ya kanuni mbalimbali zilizolifanya liwe na makali na kuibua kashfa nzito, ikiwamo ya Richmond, ambayo ilisababisha Waziri Mkuu, Edward Lowassa,  kujiuzulu na alilirejeshea makali.
Tayari Bunge la Jamhuri ya Muungano limetangaza kuanza kwa mchakato wa kumpata Spika mpya wa Bunge, atakayerithi mikoba ya Spika Anne Makinda.
Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel, akizungumza na vyombo vya habari mapema wiki hii, alivitaka vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu, kuandaa watu wao watakaowania nafasi hiyo.
Alisema vyama hivyo havina budi kuzingatia kuwa mgombea wa nafasi ya Spika, anaweza kuwa mbunge au mwanachama yeyote wa chama hicho kwa masharti kwamba kama si mbunge, jina lake lazima liwasilishwe kwanza Tume ya Uchaguzi siku tano kabla ya uchaguzi, kujiridhisha kuwa mgombea huyo ana sifa za kuwa mbunge.
Mbali na kutangaza kuanza kwa mchakato wa uspika, Joel pia aliwataka wabunge waliopo majimboni kuwasili Dar es Salaam, kuanzia  jana, ili washiriki hafla ya kuapishwa kwa Rais Mteule, Dk. John Magufuli, kesho kwenye Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam.
Ripoti ya tathmini juu ya utendaji kazi wa Bunge la tisa chini ya Spika Sitta, iliyofanywa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), inaonyesha kuwa Bunge hilo lilikuwa na ufanisi na ubunifu.
Ilisema Bunge hilo la tisa lilipata ufanisi na mafanikio kadhaa, kutokana na ubunifu na ujasiri wa baadhi ya wabunge, wakiongozwa na utayari wa Sitta, ambaye wakati akishika nafasi hiyo aliahidi kuwa 'spika wa kasi na viwango.'
Mafanikio yaliyopatikana katika Bunge hilo, kwa mujibu wa ripoti hiyo ni pamoja na kutungwa kwa kanuni mpya za Bunge za mwaka 2007, ambazo zimeelezwa kuwa zilisaidia kwa kiasi kikubwa kuliwezesha lifanyekazi kwa ufanisi, kama vile kuondoa ukiritimba wa serikali kuwa ndiyo pekee inayoweza kupeleka muswada bungeni.
Kanuni hizo mpya za mwaka 2007, ambazo zilitokana na kufanyia marekebisho makubwa kanuni za Bunge za mwaka 2004, zilitoa mamlaka kwa Kamati za Kudumu za Bunge kuwa na uwezo wa kupeleka miswada kwa ajili ya kujadiliwa bungeni na hatimaye kuwa sheria.
Mambo mengine yaliyolipatia sifa Bunge la tisa chini ya Sitta ni kubadili kanuni za Bunge, ambazo ziliruhusu uwasilishwaji wa hoja binafsi bungeni na ulazima wa kamati za kudumu za Bunge kushirikisha umma katika kujadili mapendekezo ya miswada mbalimbali.
Masuala mengine ni Kamati za Kudumu za Bunge kuwa na uwezo wa kujadili na kuwasilisha mapendekezo yao bungeni kwa ajili ya kujadiliwa, Bunge kuwa na uwezo wa kuanzisha kamati maalumu zilizo na uwezo wa kuchunguza mambo kama ile iliyochunguza kashfa ya Richmond na uvunjifu wa haki za binadamu kwa kuchafua maji ya Mto Tigiti huko Mara.
Ripoti hiyo inasema katika kutimiza moja ya majukumu yake ya msingi ya kikatiba, Bunge hilo lilibadili na kutunga sheria kadhaa kwa maslahi ya jamii, zilizokuwa na mtazamo wa haki za binadamu, kama vile Sheria ya Mtoto ya 2009, Sheria ya Gharama za Uchaguzi na Sheria ya Watu wenye Ulemavu (2010).
Mbali ya uspika, Sitta ameshika nyadhifa mbalimbali kuanzia katika serikali ya awamu ya kwanza hadi awamu ya nne inayomaliza muda wake ya Rais Jakaya Kikwete.
Nyadhifa hizo ni pamoja na kuwa Waziri wa Uchukuzi, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Waziri wa Katiba na Sheria, Mkurugenzi Mkuu Kituo cha Uwekezaji (TIC) na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba

No comments:

Post a Comment