Monday 9 November 2015

SITTA: TUNAHITAJI BUNGE LENYE HOJA, SI KUPIGA KELELE




ALIYEKUWA Spika wa Bunge la Tisa, Samwel Sitta, amesema bunge lijalo, linalotarajiwa kuanza vikao vyake Novemba 17, mwaka huu, linapaswa kutawaliwa na hoja za msingi na si wabunge kupiga kelele.
Kutokana na changamoto zinazotarajiwa kulikabili bunge hilo, Sitta amesema anahitajika mtu mwenye uzoefu na anayezifahamu vyema kanuni za bunge ili kutenda haki baina ya Chama tawala na upinzani.
“Wakati umefika wa bunge lijalo kuwa la kujenga hoja na sio wabunge kupiga kelele,”amesema.
Sitta, alisema hayo jana, katika mahojiano maalumu na kipindi cha Hello TZ, kinachorushwa hewani na kituo cha Radio Uhuru FM cha Dar es Salaam.
Katika mahojiano hayo, Sitta aliweka wazi nia yake ya kugombea nafasi ya uspika katika Bunge la 11 na kuongeza kuwa, ameamua kuwania nafasi hiyo baada ya kuona changamoto zilizopo baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu.
 “Kuna mambo ambayo huwezi kuyafanya ukiwa pembeni, bali ujuzi wako mahususi unahitajika hata kama unakwenda unaachia pole pole. Kama suala ni kurithisha uzoefu, litapatikana humo humo,” alisema
Aidha, alisema umakini unahitajika katika bunge la 11 kutokana na kiporo cha Katiba Inayopendekezwa na kuongeza kuwa, anafahamu vizuri kuhusu mapendekezo yaliyomo kwenye katiba hiyo.
“Katiba ya nchi huangusha nchi,  ni suala ambalo lisipowekwa vizuri,
lisipotengenezewa mazingira mazuri ya kwenda mbele, linaweza kutugawa tukafika mahali ambapo mambo mengine yasikae vizuri,” alisema.
Alisema anazielewa hisia za pande zote mbili kuhusu Katiba Inayopendekezwa na kwamba, anaamini ana uwezo na sifa za kupata nafasi hiyo ya uspika na ataifanya vizuri atakapopata nafasi ya kuliongoza Bunge la 11.
Alisema kuna mambo mengi ndani ya Katiba Inayopendekezwa yanayohitaji umakini wa hali ya juu na kutolea mfano wa suala la mgombea binafsi, linalohitaji kuwekewa sheria ili kutoa mwongozo katika nafasi hiyo.
“Suala la mgombea binafsi linahitaji kuwekewa sheria. Kama ni chama mnaambiwa kabisa mkileta ukabila, udini na ukanda, chama kinafutwa je, kwa mgombea binafsi inakuwaje?”  Alihoji.
Aliongeza kuwa iwapo atapata nafasi hiyo, atahakikisha anamaliza vizuri jambo hilo ili kila Mtanzania aridhike na maamuzi yatakayotolewa na bunge.
Sitta alisema ndani ya miaka mitano, watu wanategemea maendeleo na  mabadiliko ya katiba ili nchi iendelee kubaki na umoja na amani na waridhike kwamba haki itatendeka ndani ya katiba mpya.
Alisema kinachohitajika katika bunge lijalo ni uvumilivu na kuyakusanya makundi yote yafanye kazi kwa pamoja na kujenga bunge la kizalendo.
“Tunahitaji bunge litakalotanguliza maslahi ya nchi kwani uchaguzi umeshamalizika, tusijenge hisia miongoni mwa majirani zetu katika Afrika kwamba kila tunachokifanya tunakidharau, tujenge taifa moja la kizalendo,” alisema.
Sitta alisema anachosubiri ni taratibu za Chama ili aweze kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea nafasi hiyo.
Kwa upande wake, Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema mpaka sasa Chama hakijapanga ratiba ya uchukuaji fomu za kuomba kuteuliwa na chama hicho kwa ajili ya nafasi hiyo ya uspika.
Sitta, aliongoza bunge la tisa kwa kipindi cha miaka mitano, kuanzia 2005 hadi 2010, na kupewa jina la ‘Mzee wa Kasi na Viwango.’

No comments:

Post a Comment