Friday, 11 March 2016

TRA YAFUTA RASMI MSAMAHA WA KODI






MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA), imetangaza kufuta msamaha wa kodi kwa wafanyabiashara wanaoingiza bidhaa kutoka nchini China.

Awali, TRA iliweka kodi elekezi kwa bidhaa kutoka China, ambapo sasa wafanyabiashara watatakiwa kulipa kulipa kodi halisi inayotakiwa ili kuweka uwiano sawa na bidhaa zingine zinazoingizwa nchini.

Pia, TRA imetangaza kukusanya mapato ya sh. trilioni 8.6, ikiwa ni asilimia 99 ya malengo iliyojiwekea kwa mwezi Februari, mwaka huu, na kwamba itaongeza kasi zaidi katika ukusanyaji wa mapato ya serikali.

Kaimu Kamishina wa TRA, Alphayo Kidata, alisema jijini Dar es Salaam, jana, kuwa serikali kupitia mamlaka hiyo, imefuta kodi elekezi hiyo, ambayo ilikuwa ikiwapa punguzo la kodi wafanyabiashara wanaoagiza na kuingiza bidhaa kutoka China kwa kupunguziwa sehemu ya kodi.

“Tumeamua kuondoa kodi elekezi kwa sababu haina faida kwa taifa na inawanyima wafanyabiashara wengine, ambao hawaagizi bidhaa kutoka China, fursa ya kushindana sokoni.

“Serikali yetu si ya kibaguzi na ndio sababu tumeamua kufuta kodi hii ili kuleta usawa kwa wafanyabiashara wote,” alisema Kidata.

Aliongeza: “Suala lililopo kwa sasa ni kwa kila mwananchi anayepaswa kulipa kodi katika kitu anachokifanya, alipe kodi na hatutafumbia macho ukwepaji wa kodi na hakuna kitu kinachoitwa kodi elekezi wala msamaha wa kodi katika serikali hii, tulipe kodi kwa maendeleo ya taifa letu.”

Alisema hakuna sheria yoyote inayosema kuwa kutakuwa na kodi elekezi ama msamaha wa kodi kwa mfanyabiashara, bali ule ulikuwa ni utaratibu uliowekwa na TRA na haukuwa na tija.

Katika hatua nyingine, Kidata alisema serikali ipo kwenye mpango wa kuunda Mamlaka ya Mapato Kuu ya Taifa nje ya TRA, iliyopo kwa sasa ili kuondokana na malalamiko ya kero za kodi kwa wananchi wenye kipato cha chini.

Alisema hiyo ni sehemu ya mikakati ya serikali ya kuwasaidia wananchi wa kipato cha chini, kumudu kulipa viwango vya kodi vinavyowekwa na mamlaka hiyo.

“Serikali inawajali watu wake na ndio sababu tumeona kuna haja ya kuunda mamlaka moja ya utozaji wa kodi, itakayojumuisha taasisi zote zinazohusika na ukusanyaji wa mapato nje ya kodi na ushuru ili kuondoa malalamiko ya wananchi,” alisema.

Kidata alisema mamlaka hiyo itasaidia kuweka viwango vya kodi, ambavyo wananchi wa hali ya chini watamudu kulipa kutokana na biashara au kazi wanazozifanya.

TRA imekuwa na rekodi nzuri ya ukusanyaji wa kodi ila kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu kodi, ambazo zimekuwa kero na hazina tija.

Kaimu Kamishna wa Kodi za Ndani wa TRA, Salum Yusuf, alisema watalisimamia suala la ulipaji kodi na yeyote atakayekaidi kulipa, atachukuliwa hatua za kisheria.

No comments:

Post a Comment