Thursday 7 April 2016

DK SHEIN AWAONYA WAFANYAKAZI WAZEMBE




SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imeahidi kuimarisha maslahi ya wafanyakazi, lakini imeonya kuwachukulia hatua wale wote ambao ni wazembe.

Ahadi hiyo ilitolewa jana, mjini Zanzibar na Rais  Dk. Ali Mohamed Shein, katika hotuba yake wakati wa kuzindua rasmi Baraza la Wawakilishi.

Dk. Shein alisema SMZ itaendelea kuimarisha miundo ya utumishi ili wafanyakazi waendelee kufaidika na elimu, uwezo na uzoefu walioupata wakiwa kazini na viwango vya elimu walivyonavyo.

Hata hivyo, alisema wafanyakazi wote wanafahamu kuwa mshahara ni matunda na tunzo mtu anayopata kutokana na juhudi aliyoifanya katika uzalishaji.

“Kuna baadhi ya watu wamejenga tabia ya kudai mishahara mikubwa na kuilaumu serikali kuwa haipandishi mishahara bila ya wao kuwa na ari na dhamira ya kweli ya kujitahidi kufanya kazi na kuzalisha,” alisema Dk. Shein.

Alisema watu wa aina hiyo wanapaswa kuacha tabia hiyo, ambayo haina manufaa kwa maendeleo.

Badala yake, Dk. Shein alisema kwa pamoja wanapaswa kulitekeleza kwa vitendo agizo alilolitoa mwaka 2011, mara tu baada ya kuingia madarakani kuwa ‘tubadilike na tusifanye kazi kwa mazoea’.

“Tulijitahidi kubadilika na kuyaondoa mazoea.  Lakini ni ukweli usiopingika matatizo bado yapo, viwango vya utendaji na nidhamu kazini bado havijaongezeka sana. Ni jukumu letu tufanye kazi kwa bidii na tuipende kazi,” alisema. 

Aliongeza: “Wapo baadhi ya wafanyakazi, ambao hawapendi kufanyakazi (kwa vitendo vyao), na wengine hawataki kufanyakazi, lakini wao ndio wa mwanzo wanaotaka mishahara mikubwa, posho nzuri, safari za kila wakati na kuhudhuria kwenye semina na mikutano kila mara.”

Pia, alisena wapo baadhi ya wafanyakazi kwenye taasisi muhimu zinazotoa huduma kwa wananchi, ambao hawajali kazi zao na wanakwepa wajibu wao. 

“Upo ushahidi kutoka kwa baadhi ya wananchi kwamba wanapokwenda kutaka huduma wanadharauliwa, wanapuuzwa, wananyanyaswa na wengine hutakiwa watoe kitu chochote,” alisema.

Dk. Shein alionya: “Wapo baadhi ya watumishi wenye tabia ya kutoroka, kuchelewa na hawajali kanuni. Wao hujifanya wababe mbele ya viongozi wao. Wenye sifa mbaya tutawachukulia hatua, kama hapana budi, tutawafukuza kazini. Hatuwezi kuwa na wafanyakazi waliokuwa na nidhamu.
Sasa basi, imetosha.” 

Aliongeza kuwa waliopewa dhamana ya kuongoza idara mbalimbali za serikali, watapaswa watekeleze wajibu kwa kuwasimamia wafanyakazi walio chini yao. 

Viongozi hao nao wameonywa kuwa kama hawatawawajibisha wafanyakazi wao, watawajibishwa wao. 

Pia, Dk. Shein aliwahakikishia wananchi kuwa atatekeleza ahadi alizozitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka 2015, za kuimarisha maslahi ya wafanyakazi katika sekta mbalimbali, ukiwemo utoaji wa kima cha chini cha mshahara cha sh. 300,000 kwa mwezi ndani ya kipindi cha mwaka mmoja baada ya kuingia madarakani.

Alisema katika kipindi cha uongozi wake, serikali itaimarisha huduma za hifadhi ya jamii kwa wanachama wake, kwa kubuni utoaji wa mafao mapya na kuongeza kiwango cha malipo ya kiinua mgongo na pensheni. 

“Madeni ya viinua mgongo vya wafanyakazi waliostaafu tutayalipa, tunawaomba wastaafu wawe na subira,” alisema Dk. Shein.

Kuhusu ajira, alisema suala hilo bado ni changamoto kama ilivyo katika mataifa mengine na kwamba, ana matumaini makubwa ya kupata mafanikio katika ongezeko la nafasi za kazi katika kipindi kijacho kutokana na mikakati iliyopo.

“Tutahakikisha jitihada za serikali za kutekeleza mageuzi ya uchumi zinafanikiwa katika sekta ya utalii na viwanda kwa kuwashajiisha wawekezaji,” aliahidi na kuongeza kuwa, sekta binafsi itaimarishwa na kuwa chanzo kikuu cha ajira.

No comments:

Post a Comment