Wednesday 23 March 2016

DIWANI WA CHADEMA ATUPWA JELA MIEZI SITA




DIWANI wa Kata ya Siuyu, Tarafa ya Mungaa, Jimbo la Singida Mashariki, Jared Justin (CHADEMA), amehukumiwa kwenda jela miezi sita, baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kuzuia wakala wa kukusanya mapato ya Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi.

Imedaiwa kuwa jimbo hilo pekee mkoani Singida, ambalo lipo mikononi mwa upinzani (CHADEMA), lina sera ya kuzuia wananchi wake kuchangia maendeleo kwa madai kuwa hilo ni jukumu la serikali.

Mahakama ya Mwanzo ya Ikungi, chini ya Hakimu Simon Kiyinga, ilimuhukumu diwani huyo kijana kwenda jela juzi, baada ya kuridhishwa na upande wa Jamhuri.

Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa Februari 13, mwaka huu, saa tatu asubuhi, katika mnada wa Njiapanda, mshitakiwa alimzuia Ofisa Mwidhiniwa, Amina Abdallah wa Kampuni ya Abada  Care Investment, kufanyakazi ya kukusanya ushuru wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi.

Kwa mujibu wa hati ya upande wa mashitaka, siku ya tukio, mshitakiwa alitenda makosa mawili,  ikiwa ni pamoja na kumuzuia Amina kufanyakazi yake ya kukusanya mapato ya halmashauri, kitendo ambacho ni kinyume na kifungu cha 12 (e), sheria ndogo ya Halmashauri ya Ikungi.

Aidha, mshitakiwa pia alituhumiwa kutenda kosa la kushawishi wananchi waache kuchangia mapato kwa halmashauri yao, kinyume na sheria ndogo kifungu cha 12 (1) (c).


Hata hivyo, Hakimu Simon Kiyinga alitupilia mbali tuhuma za kosa la pili kwa kuwa ushahidi uliotolewa hautoshi kumtia hatiani mshitakiwa.

Hakimu Kayinga alisema kwa kosa la kwanza la kumuzuia ofisa kukusanya mapato yaliyobainishwa na Halmashauri ya wilaya ya Ikungi, ushahidi wa upande wa mlalamikaji, umethibitisha bila kuacha shaka yoyote kwamba ana hatia kama alivyoshitakiwa.

Kwa hali hiyo, alisema mshitakiwa atakwenda  jela miezi sita, ili iwe fundisho kwake na kwa madiwani wengine wanaotarajia kufanya kosa kama hilo.

No comments:

Post a Comment