WAZIRI MKUU Kassim
Majaliwa ameiagiza Bodi ya Soko la Kimataifa la Samaki la Feri, kukutana na
kampuni mbalimbali zinazouza gesi ili kupata inayouza kwa bei nafuu zaidi,
lengo likiwa kuwapunguzia gharama wakaangaji wa samaki sokoni hapo.
Aidha, Waziri Mkuu
Majaliwa amemtaka Meneja wa soko hilo, Solomon Mushi, kuhakikisha wanakuwa na
kifaa maalumu cha kupimia ujazo wa mitungi ya gesi sokoni hapo ili kubaini kama
ni sahihi.
Alitoa agizo hilo jana,
wakati alipofanya ziara ya ghafla katika Soko la Kimataifa la Samaki la Feri,
iliyokuwa na lengo la kuangalia mfumo wa majiko ya gesi sokoni hapo, ambapo
aliridhishwa na unavyofanya kazi.
Waziri Mkuu, ambaye
alitumia dakika 44, kulitembea soko hilo, alitoa maagizo hayo baada ya kupokea
malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara, ambao wamesema wamekuwa wakiuziwa gesi
kwa bei kubwa na imekuwa ikiongezeka mara kwa mara.
Akizungumza kwa
niaba ya wafanyabiashara hao, Ally Iddi, alisema awali walikuwa wanauziwa
mtungi wa gesi wenye ujazo wa kilo 32, kwa sh. 70,000, lakini sasa umeongezeka
hadi sh. 98,000, kiasi ambacho ni kikubwa ikilinganishwa na uzalishaji wao.
“Nimeulizia kwenye
baadhi ya maduka na kukuta mtungi wenye ujazo kama huo unauzwa sh. 75,000,”
alisema.
Kijana mwingine,
ambaye ni mkaangaji wa samaki, Mwanya Selemeni, alisema hivi sasa hali ya soko
la feri ni nzuri, tofauti na walivyokuwa wakitumia kuni kwa sababu hakuna
moshi. Alimuomba Waziri Mkuu ahakikishe wanafikishiwa gesi ya kutoka Mtwara ili
gharama ziweze kupungua.
Naye Mariam Samweli,
alimuomba Waziri Mkuu wapatiwe umeme kwenye mabanda yao ili watafute biashara
zingine za kufanya.
Katika ziara hiyo, Waziri
Mkuu pia alitembelea eneo la mnada wa kuuza samaki sokoni hapo, ambako
alielezwa matatizo ya umeme na uzibaji wa mitaro ya maji machafu, hali ambayo
inatishia usalama wa afya zao.
“Kuna jipu la umeme
hapa, tunachangishwa hela na kumpa mtu ambaye hatumjui, lakini hatujawahi kuona
risiti, wao wanaweka umeme juu kwa juu na umeme wenyewe wala haukai. Mita
tunayo hapa, lakini hata namba hatujapewa,” alisema Omari Masoud kwa niaba ya
wenzake.
Kuhusu tatizo la
uzibaji mitaro na kutiririsha majitaka, kiongozi wa mama lishe sokoni hapo,
Fatma Ally, aliomba watatuliwe tatizo hilo, ambalo limedumu kwa zaidi miezi
miwili.
Akijibu kero hizo,
Waziri Mkuu alimwagiza Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Raymond Mushi, asimamie suala
la kuweka umeme kwenye banda na kuhakikisha mama lishe wa soko hilo upande wa
mnadani, waanze kutumia majiko ya gesi badala ya mkaa.
Kuhusu mitaro,
alimwagiza meneja wa soko hilo, Solomon
Mushi aimarishe uzibuaji wa mitaro.
“Mwambie mkandarasi
azibue mitaro kila siku jioni na watumiaji wa soko waache kutumia mifuko ya
plastiki kwa sababu inapoingia kule, inaziba na wala haiozi,” alisema.
Aliwataka
wafanyabiashara waimarishe usafi kwa sababu ni sehemu ya chakula. “Lengo letu
ni kufanya soko hili liwe kwenye viwango vya kimataiafa ili mteja anapokuja
kununua samaki wabichi ama wa kukaanga, awe na chaguo,” alisema.
Kwa upande wake,
Mushi alisema bodi ya soko hilo, ambayo imeundwa hivi karibuni, itakutana kesho
kwa mara ya kwanza na miongoni mwa mambo yatakayojadiliwa ni maelekezo
yaliyotolewa na Waziri Mkuu.
Katika hatua
nyingine, Majaliwa amesema mabasi yaendayo kasi (DART), yataanza kufanyiwa
majaribio ndani ya wiki moja kuanzia sasa, ili madereva waanze kuzoea njia na
taa za kuongozea magari.
“Wataanza na mabasi
kati ya 30 – 50, ambayo yatapita kwenye njia zote za mradi huo. Zoezi hilo
litafanyika ili watumiaji wengine, wakiwemo waendesha daladala, bodaboda na
watembea kwa miguu waweze kutambua kuwa njia ya mabasi yaendayo kasi si ya
kwao, hivyo waanze kuzoea,” alisema.
Alitoa kauli hiyo jana,
wakati alipofanya ziara ya ghafla katika Soko la Kimataifa la Samaki la Feri,
iliyokuwa na lengo la kuangalia mfumo wa majiko ya gesi sokoni hapo na kukagua
ujenzi wa ukuta unaotenganisha soko hilo na mabasi yaendayo kasi.
Waziri Mkuu, ambaye
alitembelea soko hilo kuanzia saa 5:10 hadi saa 5:54, alitoa jibu hilo wakati
akijibu maombi ya mfanyabiashara, Sharifu Ramadhani, ambaye alisema wanatumia
fedha nyingi kwa ajili ya usafiri kwa vile mabasi mengi yanaishia Mnazi Mmoja.
“Mabasi yanaishia
Mnazi Mmoja na huku ni mbali kwa hiyo tunalazimika kutembea kwa miguu kwa
sababu kukodi taksi ni gharama kubwa,” alisema.
Akifafanua kuhusu
hatua iliyofikiwa kwenye utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu alisema: “Hivi
sasa wanakamilisha ufungaji wa mitambo ya kukatia tiketi, ambapo abiria atakuwa
na kadi kama za benki, ambayo anaijaza fedha halafu anapita kwenye mashine,
kiasi cha nauli kinakatwa halafu anaingia kwenye basi, hakutakuwa na muda wa
kukata tiketi.”
Alisema tatizo la
usafiri kwa wafanyabiasha wa feri litakwisha hivi karibuni baada ya mabasi hayo
kuanza kazi.
No comments:
Post a Comment