Friday 8 April 2016

HAMAD RASHID, ALI KARUME WAULA




RAIS wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein, ameteua wajumbe saba kuwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi huku akiwajumuisha viongozi watatu wa vyama vilivyoshiriki uchaguzi wa marudio wa Machi 20, mwaka huu.

Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, iliwataja wajumbe hao kuwa ni Balozi Ali Karume, Amina Salum Ali na Mohamed Aboud.

Wengine ni aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha ADC, Hamad Rashid Mohammed, Said Soud Said, ambaye aliwania nafasi ya urais kupitia chama cha AFP Wakulima na Juma Ali Khatib wa Chama cha TADEA.

Taarifa hiyo ilisema wajumbe wengine walioteuliwa ni Moulin Castico, ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Ilisema Dk. Shein amefanya uteuzi huo kwa mujibu wa Katiba kifungu cha 66 cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, ambayo inampa uwezo kufanya uteuzi wa wajumbe kumi kuingia katika baraza la wawakilishi.

Katika hotuba yake ya uzinduzi wa Baraza la Wawakilishi, Rais Dk. Shein aliahidi kuunda serikali itakayovishirikisha vyama vya siasa kwa ajili ya kuleta maendeleo ya wananchi wote bila ya kujali itikadi za kisiasa.

No comments:

Post a Comment