Thursday 18 May 2017

TRL YAWAONYA WANAODANDIA TRENI BAADA YA KUANZA SAFARI





KAMPUNI ya Reli Tanzania (TRL), imewaonya wananchi, hususan wenye tabia ya kudandia treni baada ya milango kufungwa.
Imesema mtu yeyote atakayetiwa hatiani kwa kosa hilo, adhabu yake ni kifungo cha miezi sita jela.
TRL imesema tayari jeshi la polisi limeanza operesheni ya kuwasaka abiria wasiotaka kufuata sheria za kuingia kwenye usafiri huo, badala yake wamekuwa wakidandia  mabehewa baada  ya milango kufungwa.
Aidha, kampuni hiyo  imetangaza neema kwa wasafiri wa treni ya Dar es Salaam, kuwa imepanga kununua treni mpya ndani ya mwaka ujao wa fedha, ambayo itatoa huduma hiyo kwenye maeneo mbalimbali.
Akizungumza jana, Dar es Salaam, Meneja Usafirishaji Abiria wa TRL, Iddi Mzungu, alisema katika siku za hivi karibuni, kumeibuka tabia ya baadhi ya abiria kudandia kwenye mabehewa baada ya milango ya treni kufungwa na kusisitiza kuwa, atakayebainika atapelekwa mahakamani na kufungwa miezi sita jela.
''Tunaomba abiria wafuate sheria za matumizi ya treni. Agosti 3, mwaka jana,  aina hii ya uvunjaji wa sheria ilisababisha mtu mmoja kupoteza maisha baada ya kuning’inia na kugongwa na geti la kuingilia stesheni,''alisema.
Wakati huo huo, Mzungu amesema tayari mamlaka hiyo imekwishaandaa mpango wa kuletwa treni nyingine mpya, ambayo itasaidia kupunguza adha ya usafiri katika jiji la Dar es salaam.
Alisema treni hiyo ya kisasa itakuwa na uwezo wa kutumia mafuta kidogo pamoja na kuwa na uwezo wa kutembea haraka zaidi.
“Tulishaandaa mpango, tunaagiza treni  mpya, ambayo itaondoa changamoto ya usafiri  Dar es salaam, itakuwa ya kasi na isiyo na matumizi makubwa ya mafuta,” alisema.
Akielezea mkakati wa jeshi la polisi reli juu ya  kudhibiti matukio hayo, mwakilishi wa jeshi hilo, Kamanda Frank Gadau, alisema tayari operesheni imekwishaanza, ambapo abiria atakayebainika  kukiuka sheria  ya usafiri huo, atakamatwa na kufikishwa mbele ya sheria .

No comments:

Post a Comment