Monday 21 September 2015

CUF GEITA WAAHIDI KUMPIGIA KURA MAGUFULI



CHAMA cha CUF mkoani Geita, kimeweka msimamo kwamba kitamchagua mgombea wa CCM, Dk. John Magufuli ili awe Rais wa awamu ya tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kutokana na kutokuridhishwa na jinsi makubaliano ya UKAWA yalivyokiukwa.

Kauli hiyo ilitolewa jana, na mgombea ubunge wa CUF katika Jimbo la Geita Mjini, Michael Peter Malebo, wakati akiomba kura kwa wakazi wa mji wa Geita, mkutano uliofanyika kwenye uwanja wa stendi ya zamani ya mji wa Geita.

Mgombea huyo alisema yeye ndiye alikuwa ameteuliwa na UKAWA kupeperusha bendera ya umoja huo kupitia CUF, lakini alishangaa kuona baadaye anateuliwa mgombea mwingine, Rogers Luhega kutoka CHADEMA na hivyo kuamua kuchukua fomu kugombea kupitia CUF.


Alisema kitendo cha viongozi wa ngazi za juu kukubali kumteua Rogers kuwa mgombea badala yake, ni uhuni na alikataa kukubaliana nao.

Malebo alisema yeye na Chama chake cha CUF mkoani hapa wamekubaliana wamchague Dk. Magufuli aongoze Taifa na kusisitiza kuwa mikutano yao yote ya kampeni watawahimiza wananchi wa Geita kumchagua Dk. Magufuli.

"Ndugu wananchi wote wa Geita mchagueni John Pombe Magufuli kwa maendeleo ya Taifa. Sisi CUF hatumuungi kabisa mkono Lowassa wa CHADEMA, natoa wito wakazi wote wa Geita mchagueni Magufuli tu maana tumefanyiwa uhuni.

"Hapa ni kazi tu, chaguo letu sahihi ni Magufuli, nawasihi sana wananchi msimchague Lowassa na UKAWA yao bali mtu wa kazi na hata mimi mwenyewe kwa upande wa ubunge mkiona kura hazitoshi, basi kura zangu zote mpeni Costantine Kanyasu mgombea wa CCM katika jimbo hili,“
alisema Malebo.

Naye Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya CUF Wilaya ya Geita, Shaban Makunga, kabla ya kumkaribisha mgombea huyo kupanda jukwaani, alisema wao baada ya kutafakari wamebaini viongozi wao ngazi ya Taifa wamewafanyia uhuni.

Kutokana na hilo, alisema hawako tayari kuendelea na umoja huo huku akisema chaguo lao sahihi ni Magufuli na watatumia nguvu zao zote kumnadi kila wanakokwenda.

No comments:

Post a Comment