Monday 21 September 2015

UKAWA WAZIDI KUTIFUANA, MAHANGA, SUMAYE WAJIKAANGA




UGOMVI wa kugombea majimbo na kata baina ya wanachama wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), umezidi kushika kasi na kutishia kupasua umoja huo.
Hali hiyo ilidhihirika katika mkutano wa kampeni za UKAWA jimbo la Ukonga, Chanika, Magengeni, Dar es Salaam jana, ambapo mgombea urais wa CHADEMA, Edward Lowassa, alikuwa akihutubia sambamba na kutambulisha wagombea udiwani na ubunge wa jimbo hilo.
Awali, wakizungumza na Uhuru, wafuasi wa CHADEMA wa eneo hilo, walisema kumekuwa na mvutano mkali kuhusu nafasi za wagombea udiwani, hali iliyowalazimu kuwaacha wagombea wenye mvutano wasimame wote.
"Kutokana na hali hiyo CCM (Chama Cha Mapinduzi), hakitakuwa na kazi kubwa katika kata zote 12 za jimbo, maana tumeshagawanyika hivyo ushindi kwao ni mweupe.
"Lakini sisi (CHADEMA), ndio tuliohangaika sana kujenga chama katika jimbo hili, wenzetu CUF walikuwa wamelala tu, hata uhamasishaji kujiandikisha BVR ni sisi ndio tulifanya, mimi peke yangu nilitoa 80,000, ila wenzetu wanataka kutumia nguvu yetu,"alisema Joyce Chacha, ambaye ni mama lishe katika eneo hilo la Chanika Magengeni.
Mpasuko huo uliwalazimu viongozi wa CHADEMA kuugeuza ajenda badala ya sera za uchaguzi.
Alipopata nafasi ya kupanda jukwaani, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alimtaka mgombea ubunge wa jimbo la Ukonga, Mwita Waitara, kulishughulikia tatizo hilo ndani ya siku moja na kuwafukuza wote watakaokaidi maagizo.
Katika kauli zake za vitisho, Mbowe alisema wameshafanya maamuzi kila eneo la ubunge na udiwani asimame mtu mmoja, hivyo ni marufuku kujitokeza wawili.
Katika mkutano huo, ambao ulijaa wafuasi wa CHADEMA bila kuhusisha vyama vingine, kauli hiyo ya Mbowe ilizua minong'ono ya chini  kwa chini na kuanza kudhihakiana wenyewe kwa wenyewe.
"Kila nafasi mtu mmoja, tatizo la kugombea nafasi ya ubunge au udiwani haliruhusiwi, jimbo hili tulishasema atasimama Waitara na katika nafasi za udiwani viongozi wenu wa jimbo watatoa majina ya wanaostahili kusimama kwenye kata.
"Kama kuna wagombea wengine, ajue kabisa hawakilishi Ukawa, asimame mwenyewe, na atakayekaidi afukuzwe tu,"alisema Mbowe katika kauli zake za kujihami.
Katika hali ya kushangaza na kutapatapa, aliyekuwa Waziri Mkuu, Frederick Sumaye na Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Makongoro Mahanga walitoa kauli za kujikaanga wenyewe.
Kwa upande wake, Mahanga alisema aliwahi kuwa mbunge wa jimbo la Ukonga kabla ya kugawanywa na kupatikana jimbo la Segerea, na kwamba tangu alipoondoka jimboni humo, hakuna maendeleo.
Alisema alikuwa Naibu wa Waziri wa Kazi, lakini hakuna kazi kwa vijana, kauli ambayo inamfunga kwamba utendaji wake ulikuwa ni mbovu.
Hata hivyo, Ukonga na Segerea zinaelezwa zilikuwa kwenye vipindi vigumu vya ukosefu wa maendeleo wakati Mahanga akiwa mbunge katika majimbo hayo, hali iliyowalazimu wananchi kumuengua kwenye kura za maoni za CCM jimbo la Segerea, na yeye kukimbilia CHADEMA.
Sumaye, ambaye alikuwa Waziri Mkuu kwa miaka 10, aliwashangaza watu alipodai hakuna maendeleo yaliyofanyika na viongozi ni wazembe.
Alisema kwa sasa hakuna matumaini labda mtu awe mwizi ama mpenda magendo na kuwataka wananchi kufanya mabadiliko ama waiache CCM madarakani.
Akimalizia mkutano huo, Lowassa alitoa kauli ambazo zinaonyesha dhahiri akiingia madarakani, nchi itakuwa kama jalala.
Alisema ataruhusu shughuli nyingi zifanyike popote wakiwemo wamachinga, bodaboda na mama lishe,  hali inayotishia ustawi wa taifa kutoweka, kwa sababu kila kitu lazima kifanyike kwa utaratibu na si holela kama alivyotangaza yeye.

No comments:

Post a Comment