Sunday 11 October 2015

DK SHEIN AAHIDI KUSAMBAZA ZAIDI UMEME PEMBA




Na Hamis Shimye, Pemba

MGOMBEA urais wa Zanzibar kupitia CCM, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema serikali yake inaendelea na jitihada za kufikisha umeme katika baadhi ya maeneo katika Jimbo la Mtambwe, Kaskazini Pemba.

Amesema yako baadhi ya maeneo ambayo umeme bado haujafika, hivyo atahakikisha unafika katika maeneo yote jimboni humo.

Akizungumza katika viwanja vya Shule ya Makoongeni, Dk. Shein alisema pamoja na kufikisha umeme katika maeneo hayo, pia atajenga barabara zenye hadhi ya kimataifa.

"Umeme ni lazima na nitahakikisha unafika  Mtambwe yote, lakini pia tegemeeni barabara zenye hadhi ya miji mikuu kama vile Dar es Salaam, Nairobi na Kampala.

“Nilipotembelea kituo kimoja cha karafuu mwaka 2011, niliahidi kujenga barabara inayokuja Mtambwe, lakini nimeambiwa barabara ile haikujengwa ipasavyo," alisema.

Kuhusu zao la karafuu, aliwaambia wakazi hao wa Mtambwe kuwa serikali italisimamia ingawa wenzao wa Chama cha Wananchi (CUF) sera yao ilikuwa ni kulibinafsisha.

Naye Balozi Ali Karume alisema CCM haitoi ahadi za uongo ndiyo maana Dk. Shein alipoahidi gharama za kujifungua ni bure, limetekelezwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja.

"Wanawatisha CCM ikishinda watachoma nyumba za CCM moto, wataanzia wapi, kwani wao wanalala nje?" Alihoji Balozi Karume.

No comments:

Post a Comment