Wednesday 7 October 2015

NEC YASEMA IMESHATOA ELIMU YA KUPIGA KURA KWA ASILIMIA 90




NA RACHEL KYALA
TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imesema hadi sasa imetoa elimu ya mpigakura kwa zaidi ya asilimia 90, tofauti na lawama kwamba haijaifikia jamii ipasavyo.
Aidha NEC, imesema imeshaendesha vipindi vya televisheni 22, na  24 vya redio mbalimbali, huku elimu hiyo ikiendelea kutolewa kwenye redio ya mtandao wa tume kwa saa 24 hadi sasa na kutoa kibali kwa asasi 447 kutoa elimu hiyo kwa jamii tangu Agosti 19, mwaka huu.
Vile vile imesema imeshatoa taarifa mbalimbali magazetini, kuchachapisha majarida ya elimu kwa mpigakura, ambapo wiki iliyopita ilikutana na wawakilishi wa makundi mbalimbali, ikiwemo walemavu, vijana na wanawake.
Kaimu Mkurugenzi, Idara ya Habari na Elimu kwa Mpigakura, Giveness Aswile, alisema hayo jana, jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa  NEC inawashangaa wanaoibeza kwamba haijatoa elimu ya kutosha.
Alizishangaa taasisi kama vile Mtandao wa Asasi za Kiraia wa Kuangalia Uchaguzi Tanzania (TACCEO).
Mtandao huo katika mkutano wake na waandishi wa habari jana, uliitupia lawama NEC  kuwa imetoa elimu ya mpigakura kwa asilimia 8.6 tu, jambo ambalo ulidai utawakosesha watu wengi haki ya kupiga kura.
“Tatizo watu wanachanganya elimu ya uraia na elimu ya mpigakura na kuipa NEC, majukumu yasiyo yake, NECc imeshafanya sehemu yake kwa kiasi kikubwa na bado inaendelea, madai hayo hayana tija yoyote,” alisema Giveness.
Alisema, elimu ya mpigakura inapaswa kuelimisha namna mpigakura anavyotakiwa kushiriki katika uchaguzi, maeneo ya kupgia kura, huku elimu ya uraia inaelimisha wajibu, sababu na haki za kupiga kura.
“Elimu ya mpigakura ni kipengele kidogo tu ndani ya elimu ya uraia, ambapo serikali hadi sasa bado haijaunda chombo maalumu cha kutoa elimu hiyo, hivyo suala hili ni mtambuka ni wajibu wa wadau wote, ikiwemo vyama vya siasa,” alisema.
Katika hatua nyingine, alisisitiza kuwa vituo vya kupigia kura ni vile vile ambavyo vilitumika kuandikisha wapiga kura na kusema watu wote wanapaswa kurudi nyumbani wanapomaliza kupiga kura.

No comments:

Post a Comment