Wednesday 7 October 2015

SAMIA AZITETEMESHA NGOME ZA WAPINZANI KIGOMA, ASEMA KAFULILA NI MZIGO

Wananchi wakiwa wamesimamisha gari la mgombea mwenza wa urais, Samia Suluhu Hassan alipofika katika kitongoji cha Mwandiga mkoani Kigoma
Samia akiwapungia mkono wananchi baada ya kuwasili katika eneo la mkutano
Wananchi wakimshangilia mgombea mwenza wa CCM, Samia baada ya msafara wake kuwasili Mwandiga
Samia akiteta jambo na mmoja wa wagombea ubunge wa CCM katika mkoa wa Kigoma, Husna Mwilima
Samia akisalimiana na mgombea ubunge wa CCM wa jimbo la Kigoma Mjini, Peter Serukamba
Wananchi wakimshangilia mgombea mwenza, Samia alipokuwa akiwahutubia
Dada huyo akiwa na bango wakati wa mkutano wa kampeni wa mgombea mwenza wa urais wa CCM, Samia


NA KHADIJA MUSSA, UVINZA
WANANCHI wa Jimbo la Kigoma Kusini wamesema wamechoshwa na utapeli unaofanywa na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, David Kafulila na kwamba ni mzigo uliosababisha kudorora kwa maendeleo jimboni humo.
Malalamiko hayo yamekuja  baada ya Kafulila kushindwa kutekeleza ahadi alizozitoa miaka mitano iliyopita, ikiwemo ya kufuatilia mafao ya wafanyakazi wa kiwanda cha chumvi cha Nyanza, ambao hadi sasa hawajalipwa na wanaendelea kuteseka.
Katika kuhakikisha hawamtaki Kafulila, jumla ya wanachama 70 kutoka NCCR-MAGEUZI katika Kata ya Uvinza, walijiunga na CCM, ambapo walisema sababu kubwa ni kwa mbunge huyo kutoa ahadi za uongo na kuwasababishia matatizo ya kukosa maendeleo kwa miaka mitano.
Wananchi hao waliyasema hayo katika mkutano wa kampeni wa mgombea mwenza wa urais kupitia CCM, Samia Suluhu Hassan, uliofanyika katika viwanja vya Kuchilingulu, wilayani hapa na kuhudhuriwa na umati mkubwa wa wananchi.
Mmoja wa wananchi hao Juma Mkosa (80), alisema hawamhitaji Kafulila katika jimbo lao, kwa sababu ameshindwa kuwasaidia hata wazee na badala yake amekuwa akiwaongopea kila mara wanapomfuata.
Alisema haoni sababu ya kuendelea kuchagua viongozi wa upinzani kutokana na kukosa ukweli na kuwafanya wao kama daraja la kufikia malengo yao binafsi na si kuwatumikia wananchi waliowachagua.
Naye Fundi Kajwabi (60), alisema wamejifunza kutokana na makosa, hivyo hawatarudia tena na sasa wamejipanga kuhakikisha mgombea wa CCM anaibuka na ushindi, ili washirikiane  naye  katika kuboresha maendeleo yao.
"Kafulila ni tatizo na mzigo, kwani ukweli mdogo ametudanganya sisi vijana kuwa atatujengea gereji ili tujiajiri, nasi tukampa kura, baada ya kupata akaingia mitini na mbaya zaidi ni pale alipowaahidi wazee wetu waliokuwa wanafanyakazi katika kiwanda cha chumvi kuwa akishinda ubunge atahakikisha wanalipwa mafao naolo hakulitekeleza, hivyo hatuwezi kumchagua," alisema Rashid Kisoma.
Naye Kalunde Juma alisema licha ya kuahidi wanawake kuwawezesha kiuchumi kwa kuwapatia mikopo ili waendeleze vikundi vyao vya ujasiriamali, alishindwa na kuwaacha wakihangaika bila msaada, ambapo alisema hawataki tena kutawaliwa na upinzani na badala yake wanaichagua CCM kwa kuwa inatekeleza ahadi zake kwa wananchi.
Mgombea ubunge wa jimbo hilo  kupitia CCM, Hasna Mwilima,  alisema Kata ya Uvinza inakabiliwa na changamoto mbalimbali, zikiwemo za upatikanaji wa maji safi na salama, hospitali ya wilaya na mafao kwa waliokuwa wanafanyavkazi katika kiwanda cha chumvi, hivyo alimwomba Samia atakapoingia madarakani kushughulikia kero hizo.
Naye Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Kigoma, Dk. Amani Kabouru, aliomba serikali ijayo ya awamu ya tano, iangalie mkoa huo kama lulu ya utalii kwa sababu kuna vivutio vingi vya utalii  lakini  havijapewa kipaumbele.
Akizungumza katika mkutano huo, Samia alisema suala la kulipwa fidia kwa waliokuwa wanafanyakazi wa kiwanda cha chumvi atafanyia kazi, ambapo serikali itakutana na kufanya mazungumzo na mwekezaji, hivyo kila muhusika atalipwa stahiki zake.
Kuhusu kuwepo kwa tishio la kufungwa kwa kiwanda cha chumvi kwa sababu masuala ya mazingira, alisema atahakikisha jambo hilo litafanyiwa kazi kwa kuboresha maeneo yenye matatizo na hakitafungwa, kwani kitendo hicho kitarudusha nyuma maendeleo ya wananchi.
Pia aliwataka wananchi hao kutodanganyika na wapinzani wanaopita katika maeneo na kudai kuwa wao ndio waliojenga barabara na kufikisha umeme si kweli kwa sababu vyote vimefanywa na serikali kwa kupitia ilani ya uchaguzi.
Aliwaomba  wamchague Dk. John Magufuli ili  awe rais na kuwaletea maendeleo.

No comments:

Post a Comment