Monday 16 November 2015

UVCCM: WASALITI WAWEKWE HADHARANI




UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), umesema muda wa kuoneana haya ndani ya Chama sasa umekwisha na kwamba viongozi wote wasaliti wanapaswa kuwekwa hadharani.

Umesema wana-CCM wanatambua kuwepo kwa wenzao, wakiwemo waliowahi kushika nafasi za juu za Chama na serikali, ambao wamekuwa wakikihujumu Chama na kukisababishia kufanya vibaya kwenye baadhi ya uchaguzi.

Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Shaka Hamdu Shaka, alitoa kauli hiyo jana, alipongumza na viongzi wa UVCCM na CCM, katika ukumbi wa CCM  kata ya Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja, ambapo alisema vijana watasimama imara kuhakikisha wanalinda mapinduzi ya mwaka 1964.

Kwa mujibu wa Shaka, umefika wakati kwa wana-CCM kukilinda Chama kwa hatua mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kutoendelea kuwaficha wanachama wenye sumu ndani ya CCM, ambao kwa muda mrefu wameendelea kukihujumu.

"Wakati wa kuoneana aibu au muhali umepita, hatuwezi tena  kuendelea kuwachekea maadui wapya hatari, wakijificha ndani ya Chama chetu huku wakituhujumu, inasikitisha kuona waliofaidika na matunda ya mapinduzi ni washirika wa vibaraka na  mabeberu wapya, " alisema.

Kwa mujibu wa Shaka, viongozi na wanachama wa CCM wanapaswa kutambua  hata ndani ya Chama wako baadhi  ya viongozi wastaafu wa kisiasa ambao bila aibu wameamua kushirikiana na wapinga mapinduzi ili kuyasaliti, kuyafuja na ikibidi hata  wavunje misingi yake.

Akizungumzia uchaguzi mkuu uliofutwa kisheria na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), alisema iwapo mechi haijamalizika kutokana  aidha, kuingia  giza au mvua kubwa kunyesha kabla ya dakika 90  na mwamuzi kuamuru mchezo urudiwe, timu yenye  ubavu na stamina haiwezi kutia mpira kwapani, isipokuwa  itajipanga kucheza bila ulalamishi.

Katibu mkuu huyo alisema  baadhi ya vyama vya siasa, ambavyo vimeanza kugwaya  na kudai uchaguzi ukirudiwa havitashiriki, ni rahisi kwao  kuiaminisha jamii kwamba ni vyama vya  ubabaishaji, visivyojiamini na pia vinapenda hadaa na  hila ili kupata ushindi na madaraka ya dezo.

"Thamani ya utu na uhuru huu uliotokanana na mapinduzi yaliofanywa  na  wazee wetu, anapotokea jambazi mmoja mkorofi  kutaka kuubomoa ukuta uliohifadhi hazina ya urithi wetu, tusimuonee muhali, tukabiliane naye haraka," alieleza shaka huku akipigiwa makofi.
 
Alisema kuna kila sababu ya vijana wa CCM  kujifunza kutokana na kasoro, hitilafu au jambo  lolote dhaifu,  ambalo limetokea katika uchaguzi uliofutwa na sasa kutorudia makosa.

"Tumejipima vya kutosha sasa tumejijua, tumejitambua na  hatutakubali  kumvumilia yeyote asiye na nia njema. Ndani ya  jahazi la safari yetu atakayetukoroga , tutamdhibiti kisha  tutamtosa  mkondoni bila kumuhurumia.
“Huu si wakati wa kuendelea kucheka na nyani kwani kufanya hivyo tutavuna mabua. Tunawataka viongozi ambao wanajijua kwamba tunawajua wanatuhujumu, waache mara moja na wakishindwa kufanya hivyo tutawataja hadharani,” alisema. 
Alisema si busara, hekima wala fikra njema kwa kiongozi mmoja akawa anafikiri anaweza kufanya kila kitu peke yake bila msaada wa wenzake, hivyo amewataka vijana wa UVCCM kuhakikisha wanafanya kazi za kisiasa kwa ushirikiano kama wafanyavyo mchwa, nyuki au siafu.
Shaka yuko visiwani Zanzibar katika ziara ya kutembelea mikoa yote kumi ya kichama, Unguja na Pemba, akikutana na makundi ya vijana, wazee na wanawake katika mkutano ya ndani.

No comments:

Post a Comment