Monday 4 April 2016

KIAMA CHA WAKOPAJI ELIMU YA JUU CHAJA



TAARIFA za watu wanaodaiwa na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), zitawasilishwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), hivyo kuwanyima fursa ya kupata mikopo katika taasisi za fedha.
Hatua hiyo inatokana na HESLB kutia saini mkataba na Kampuni ya CreditInfo Tanzania, utakaowezesha taarifa za wadaiwa wa mikopo ya elimu ya juu kufikishwa katika Kitengo cha Uratibu wa Taarifa za Mikopo kilichoko BoT.
Kampuni ya CreditInfo ina leseni iliyotolewa na BOT kwa ajili ya kufanya kazi hiyo. 
Hivyo, mnufaika wa mikopo ya elimu ya juu, ambaye ataomba mkopo kutoka taasisi yoyote ya fedha hapa nchini, taasisi husika itakuwa na uwezo wa kuhakiki kama mwombaji huyo ni mnufaika wa mkopo wa elimu ya juu na kama ana nidhamu ya kurejesha mikopo. 
Kwa mujibu wa mkataba huo, HESLB itawasilisha orodha ya wadaiwa wa mikopo ya elimu ya juu kwa CreditInfo, ambayo itahakikisha taarifa za wakopaji kwa taasisi zote za kifedha, zikiwemo benki, ili taasisi hizo zijiridhishe kabla ya kutoa mikopo mipya kwa wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu. 
“HESLB ina furaha kufanya kazi na CreditInfo kama mdau mpya. Tunawasihi wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu waanze kulipa madeni yao ili wawe na hadhi ya kukopesheka na taasisi za kifedha,” alisema Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Jerry Sabi, wakati wa hafla fupi ya kutia saini mkataba huo.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Davith Kahwa, alisema lengo la kampuni hiyo ni kuhakikisha fursa za ukopaji zinaongezeka na wakopaji wanakuwa na nidhamu kwa mikopo waliyopata.  
“Wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu, ambao wamekuwa wakilipa, watapata fursa ya kipekee ya kujadiliana na taasisi za kifedha kuhusu viwango vya riba kwa sababu ya nidhamu wanayoionyesha kwa mikopo yao,” alisema.
Aliongeza: ”Tumedhamiria kuiunga mkopo HESLB katika kutekeleza majukumu yake, hususan yale ya ukusanyaji mikopo iliyoiva.”
Hadi sasa, zaidi ya sh. trilioni 2.1 zimetolewa kwa Watanzania na kati ya hizo, sh bilioni 258, zimeiva, hivyo kutakiwa kukusanywa kutoka kwa wanufaika.

No comments:

Post a Comment