Monday 4 April 2016

POLISI WAAGIZWA KUKOMESHA UJAMBAZI




JESHI la Polisi mkoani Mwanza limeagizwa kuwasaka na kuwakamata mara moja majambazi wanaofanya mauaji na uporaji kwa kutumia silaha.
Mbali na hilo, wameagizwa kuhakikisha wanavunja makundi ya mitandao saba ya uhalifu inayodaiwa kuwepo Mwanza.
Agizo hilo limetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, mjini Misungwi, jana, wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Kitwanga alitoa agizo hilo muda mfupi baada ya kukabidhi baiskeli 118, zenye thamani ya sh. milioni 21.2, kwa makatibu wa CCM wa matawi 118, ya jimbo lake, ikiwa ni utekelezaji wa ahadi yake ya kuimarisha Chama.
Agizo hilo alilitoa kufuatia uporaji wa fedha kwenye maduka ya miamala ya fedha (M-Pesa) na mauji mfululizo, yaliyotokea kuanzia mwezi uliopita hadi juzi, jijini hapa, na kusabaisha watu sita kupoteza maisha na zaidi ya 10, kujeruhiwa katika maeneo ya Shede, Nyegezi, Bugarika na Temeke Nyakato, wilayani Nyamagana.
“Polisi na serikali yetu chini ya Rais Dk John Magufuli, tunawahakikishia wananchi kuendelea kuwatumikia kwa vitendo na kukomesha uhalifu huo ili wananchi waendelee na shughuli za kujiletea maendeleo bila hofu. Tumebaini kuwepo mitandao saba ya uhalifu na tayari miwili tumeivunja, nawaagiza polisi mitano iliyosalia isambaratishwe haraka,”alisema
Alisema kuendelea kwa uhalifu na mauaji kunawapa hofu wananchi juu ya usalama wao na mali zao,  hivyo ni lazima jeshi hilo liendelee kupambana na watu wanaoendesha matukio na vitendo vya uhalifu vinavojitokeza ili wananchi waishi bila hofu.
Aliwaonya askari wachache wanaodaiwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu, ikiwemo kushirikiana na majambazi waache mara moja.
 “Sisi wananchi ni wengi, wahalifu ni wachache, tutashinda na nawambia ole wao,” alisisitiza.
Akizungumzia utekelezaji wa Ilani ya CCM na ahadi yake ya kuwawezesha usafiri makatibu hao, alisema alitoa ahadi hiyo mwaka jana, lakini kutokana na mchakato wa uchaguzi mkuu, alishindwa kuitekeleza kwa kuhofia kuwa ingeonekana ni moja ya kuwashawishi viongozi hao wampigie kura.
Alisema nyenzo hizo siyo mali ya mtu binafsi, ni mali ya Chama, hivyo viongozi hao wazitunze ili ziwawezesha kutekeleza majukumu yao, ikiwa ni pamoja na kuimarisha uhai wa CCM, kwa kuwatembelea mabalozi, wanachama na kutatua kero za wananchi.
Akimpongeza kwa hatua ya kuimarisha Chama na kutekeleza Ilani, Katibu wa CCM mkoani Mwanza, Miraji Mtaturu, alisema Kitwanga ni mfano wa kuigwa na wana-CCM wengine wenye uwezo, kwani ushindi wa CCM katika chaguzo zote hutokana na viongozi wa mashina na matawi.
Mtaturu aliahidi kuwa CCM mkoani Mwanza itaendelea kuwathamini viongozi wake wote, hususan wa ngazi hizo na kuhakikisha wanawawekea mazingira mazuri ya utendaji kazi, tofauti na vyama vingine vya msimu kama wa maembe.

No comments:

Post a Comment