Tuesday 31 May 2016

MUME ASHIKILIWA NA POLISI KWA TUHUMA ZA MAUAJI YA DADA WA BILIONEA MSUYA


POLISI Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, inamshikilia mume wa Aneth Msuya, kwa tuhuma za kuhusika na mauaji  ya mkewe yaliyotokea wiki iliyopita, eneo la Kibada, Temeke.

Pia, inamtafuta mfanyakazi wa ndani, ambaye aliondoka siku moja kabla ya mauaji hayo ili kubaini sababu iliyomuondoa nyumbani kwa Aneth.

Kamanda wa kanda hiyo, Simon Sirro, alisema jana kuwa, kutokana na mauaji  hayo, wameandaa timu ya upelelezi na wataalamu kwa lengo la kubaini waliohusika katika mauaji hayo.

“Tumeandaa timu  ya upelelezi  na watalaamu  kwa ajili  ya kuwabaini watu waliojihusisha na  mauaji hayo,  ambapo hadi sasa  tumefanikiwa  kumkamata  mume wake  na  jitihada bado zinaendelea  kwa ajili ya  kumpata dada  wa kazi  ili  kubaini kitu gani  kilichomuondoa  siku moja kabla ya  mauaji,’’  alisema.
 
Sirro  aliwataka  wananchi wawape  muda  wa  kufuatilia  mauaji hayo  kwa lengo la kufahamu tatizo au chanzo chake.

Aneth (30), alikuwa ni mtumishi  wa Wizara ya  Fedha na Mipango, ambaye aliuawa  Mei 25, mwaka huu,  kwa kuchinjwa  na watu wasiojulikana, Kigamboni  jijini Dar es Salaam.

Wakati huo huo, polisi wanawashikilia watu wanne, maarufu kwa jina la Panya Road, wakiwa na marungu na mapanga, baada ya kuvamia nyumbani kwa mfanyabiashara Thomas John.

Alisema watu hao walikamatwa Mei 25, mwaka huu, saa 5.15 asubuhi, maeneo ya Vingunguti  Mtakuja, Dar es Salaam.

Watuhumiwa hao ni   Stephen  Antony (21),  Selemani  Abdallah (30), Nassoro  Anuary (21) na  Yussuf  Abballah (22) .

Katika tukio  lingine, polisi inawashilia watuhumiwa 11 wakiwa na mapanga, visu na marungu,  ambao walikamatwa Mei 21, mwaka huu, saa  1.00  usiku,  maeneo ya  Kivule  Nyang’andu.

Watuhumiwa hao ni  Lilo  Meng’anyi (18),  Abas  omarty(19), Sambulu  Odickson (18),  Ayub Mohamed(21),  Samwel  Milaba(20),  Emannulel Nyangi(18),  Moses Antony (19),  Falijara Salehe(27),  Adam  Mohamed(23),  Ally  Said (35) na  Sylivester  Gideon (22).

Aidha, Sirro alisema wanawashikilia wamiliki sita wa madanguro, wanaouza miili  na kaka poa katika maeneo mbalimbali  wilayani Temeke.

Wamiliki hao ni  Chiku Msafiri,  Diula  Victor,  Ally  Mwinyimvua, Helen  Newe, Mrisho  Khalifan  na Zaina  Mussa.
 

No comments:

Post a Comment