Tuesday 26 January 2016

MGOGORO WA ZANZIBAR UTAMALIZWA NA WANANCHI-DK. MPANGO



SERIKALI imesema itabaki kama mshauri katika mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar kwa sababu wananchi wenyewe ndiyo wenye uwezo wa kuutatua.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, alisema hayo jana, alipokuwa akijibu hoja za wabunge, baada ya kumaliza kuchangia mjadala wa mapendekezo ya  mwelekeo wa mpango wa pili wa maendeleo wa miaka mitano.
Dk. Mpango alitoa ufafanuzi huo, baada ya mbunge wa Hai, Freeman Mbowe, kueleza namna mpango huo unavyozungumzia amani, usalama, umoja, haki na demokrasia, mambo ambayo amedai hayapo kiuhalisia kutokana na serikali kushindwa kumaliza mgogoro wa Zanzibar.
Mbowe alidai kuwa mipango hiyo haitekelezeki kwa sababu ya serikali inataka kutumia nguvu ya kupora ushindi wa rais aliyepatikana.
Hata hivyo, Dk. Mpango alisema mgogoro wa Zanzibar, utamalizwa na wananchi na Serikali ya Zanzibar na Tanzania Bara itabaki kuwa mshauri.
Akizungumzia mpango huo wa mwaka 2016/2017, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashantu Kijaji, alisema unakusudia kuwa na viapaumbele vinne, ambavyo ni viwanda vya kuimarisha kasi ya uchumi na miradi mikubwa ya kielelezo ya kuwezesha uchumi kupaa.
Vipaumbele vingine ni miradi inayoendelea hususan ya maeneo wezeshi, ikiwemo barabara, reli, bandari, maji na mawasiliano kwa maendeleo ya viwanda na maeneo yatakayolenga kufungamanisha maendeleo ya viwanda na maendeleo ya watu.
Wakichangia kuhusu mpango huo, baadhi ya wabunge walidai hauwezi kutekelezeka kutokana na kuwa hauna uhalisia kwani mambo mengi yaliyoandikwa, likiwemo suala la maji vijijini, limetajwa kuwa yanapatikana kwa asilimia 68 mijini na kudai kuwa si kweli kutokana na maeneo mengi hayana maji.
Waliitaka serikali kuorodhesha kwa kutaja maeneo, ambayo maji yanapatikana na kwa kiasi gani.
Mbunge wa Kaliua, Magdalena Sakaya, alisema katika jimbo lake, hakuna maji hata kidogo na anashangazwa kusikia maji yanapatikana kwa asilimia 68.
Aliishauri serikali kutafuta namna ya kukusanya maji ya mvua ili yaweze kuwasaidia wananchi waweze kushiriki katika kilimo cha umwagiliaji na pia zijengwe reli nyingi ili kusaidia barabara nyingi zisiharibike.
Mbunge wa Babati, Jitu Son alisema taifa halifanikiwi kwenye mipango linayopanga, hususan kwenye sekta ya kukua kwa viwanda, kutokana na kuwepo kwa tozo nyingi na kodi.
Alisema asilimia 78 ya mbegu zinatoka nje ya nchi na wanazichukua kutokana na wanaozalisha mbegu wanatozwa tozo 26, hivyo ameomba tozo hizo zipunguzwe na wapandishe kodi za watakaoagiza kutoka nje ili wafanyabiashara waweze kutumia zinazozalishwa nchini.
Husein Bashe, mbunge wa Nzega Mjini, alisema kilimo kinaporomoka nchini na kushauri Benki ya Kilimo, iwezeshwe na kuwasaidia wakulima ili waweze kulima zaidi na kwamba asilimia 10 ya bajeti ipelekwe kwenye kilimo.
Akijibu hoja hizo, Dk. Mpango alisema wamepokea mapendekezo yote na kuyafanyia kazi kadri itakavyowezekana.
Alisema takwimu zote hususan za maji, ambazo wabunge wamezilalamikia kuwa hazina uhalisia kutokana na maeneo mengi kukosa maji, wanazipata kutoka ngazi za chini.

No comments:

Post a Comment