Monday 21 August 2017

SHAKA: UPYA WA CCM NI MAGEUZI YA SERA ZAKE



KAIMU Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM  (UVCCM), Shaka Hamdu Shaka amesema dhana ya upya wa CCM inatokana na kufanya kwake mageuzi ya sera zake, upitiaji mipango na uboreshaji wa oganaizehani ya Chama na jumuiya zake kulingana na mahitaji ya wakati.

Shaka pia amesema kazi inayofanywa na serikali za CCM ni uhodari wa kuyatazama mabadiliko ya dunia ili kwenda na matakwa au mahitaji ya wakati.

Shaka alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita, alipozumgumza na wanachama wa CCM na jumuia zake, katika ukumbi wa Jamhuri, mjini Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba. 

Alisema siri kubwa na upya wa CCM, sio miaka ya kuzaliwa au kuanzishwa kwake, bali ni umahiri na uhodari mkubwa wa viongozi wake katika kufanya mageuzi ya kisera, mipango mkakati na uundaji dira za maendeleo, ikiwemo kuwashirikisha wananchi. 

Alisema vyama vya upinzani havina uthubutu wala uwezo na maarifa ya kujibadili kimtazamo na kisera kulingana na mageuzi ya wakati, hivyo licha ya upya wao, huonekana ni vijuukuu, jambo linalofanya vipuuzwe na wananchi.

"Siri ya upya wa CCM  ni uhodari wa viongozi na serikali zake kuwa na uthubutu katika mageuzi ya sera juu ya masuala nyeti ya kisiasa, kiuchumi na kidiplomasia, kulingana dhamira ya wakati, "alisema.

Alisema CCM na serikali zake imejielekeza katika dhana ya kuwatumikia watu bila kuwabagua, huku kikijali na kushughulikia shida na kusikiliza kero au matatizo ya wananchi na hatimaye kuyafanyiakazi na kupata utatuzi.

Alisema hata hatua ya kufanya mabadiliko makubwa katika kuweka muundo mpya wa kakanuni na utaratibu mpya wa kiuendeshaji, usimamizi wa uchaguzi ndani ya chama pia ni katika kuheshimu dhana ya mageuzi.

Aliwataka wakuu wa mikoa, wilaya, wakurugenzi wa halamshauri za wilaya na wataalamu walio kwenye ngazi hizo, kuwa wabunifu wa mipango ili kuwaondolea dhana vijana kwamba, kusoma na kufikia elimu ya juu tafsiri yake ni kupata ajira serikalini.

"Wataalamu wetu tusaidieni kuibua mipango itakayowahimiza vijana kujitambua na kuona uzalishaji mali ni jambo muhimu na lenye tija kuliko kusubiri mshahara mwisho wa mwezi kwa kufanyakazi katika sekta ya umma,"alisisitiza Shaka 

Aliwataka vijana wa Wete na Mkoa wa Kaskazini Pemba, kutambua kuwa, hakuna serikali hata moja duniani yenye uwezo wa kuajiri vijana wote na kuwalipa mishahara kila mwezi, badala yake makundi ya vijana hujikusanya ili kuwa katika mazingira mazuri ya kuwezeshwa ili hatimaye waweze kujitegemea kiuchumi. 

"Tunao wataalamu waliosomea masuala ya uvuvi, kilimo, ufugaji, bustani, ufundi, michezo na sanaa, maeneo hayo yote ni ajira zinazoleta maisha bora kuliko kuajiriwa,"alisema. 

No comments:

Post a Comment