Saturday 10 October 2015

HAMAD: NITATEKELEZA AHADI HATA KAMA NITASHINDWA



Na  Masanja Mabula, Pemba
MGOMBEA wa Urais wa Zanzibar kupitia ADC, Hamad Rashid Mohammed, amesema  hata kama hatachaguliwa kuwa Rais atahakikisha anatekeleza ahadi zake kwani zinatekelezeka na kuwatupia lawama wanasiasa wanaodai mamlaka kamili ili watimize ahadi zao .
Amesema chama cha ADC  na viongozi wake kiko kwa  ajili ya kuwasaidia wananchi na si kutaka  umaarufu  na kuwashauri  wananchi kuacha ushabiki wa vyama bali wabadilike na kuwachagua viongozi mwenye lengo la kuwaetea maendeleo.
Kauli hiyo aliitoa wakati akihutubia wananchi wa wilaya ya Micheweni,  mkoa wa Kaskazini Pemba kwenye mkutano wa kampeni  akiomba ridhaa ya wananchi wamchague ili awe Rais wa Zanzibar, uliofanyika katika viwanja vya Shehia ya Maziwang’ombe.
Aliwataka wananchi kuwapima uwezo wagombea kwa kuwa wako walioshindwa kuwatumikia wananchi licha ya kwamba baadhi yao ni mawaziri ndani ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,  yenye mfumo wa Umoja wa Kitaifa .
“ADC hata kama haitapata nafasi ya kuongoza dola, ni lazima itekeleze ahadi zake kwani lengo letu ni kuwaletea  wananchi  maendeleo na hatusubiri kuingia Ikulu kama ilivyo kwa CUF,” alisema.
Aidha, mgombea  huyo alisema  baadhi ya wizara zinazoongozwa na mawaziri kutoka CUF zimeanza kupoteza hadhi  na kuitolea mfano Wizara ya Biashara , Viwanda na Masoko .
Alisema wakati Mazurui  anakabidhiwa wizara hiyo, kiwanda cha Makonyo Wawi kilikuwa na mashine nane ambazo zilikuwa zinafanya kazi lakini kwa sasa mashine nne zimahabirika na kudhoofisha utendaji wa kazi wa kiwanda hicho .
Akizungumzia muundo wa serikali atakayoiongoza pindi akichaguliwa, alisema itakuwa na mawaziri wasiozidi  12 huku akisema ataheshimu katiba kwa kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa .
Pia alisema atalazimika kurejea kwa wananchi kutaka kufanyike kura ya maoni ili kuifanyia marejebisho Katiba hiyo na  kufanya vyama vyote vyenye usajiliwa kudumu kushiriki katika kuunda serikali .

No comments:

Post a Comment