Tuesday 13 October 2015

KUWACHAGUA WAPINZANI NI SAWA NA KUJARIBU KIFO- MEMBE



Na Rashid Zahor, Lindi

CHAMA cha Mapinduzi (CCM), kimeonya kuwa kuwachagua viongozi wanaounda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu, ni sawa na kujaribu kifo.

Aidha, CCM imesema mabadiliko ya uongozi na serikali yanayohubiriwa na UKAWA hayana tija kwa nchi na kwamba mabadiliko ya kweli yanapatikana ndani ya Chama.

Hayo yamesemwa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM, Benard Membe, alipohutubia mkutano mkubwa wa kampeni wa mgombea urais, Dk. John Magufuli, uliofanyika kwenye uwanja wa Mpilipili mjini hapa.

Membe, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na pia mbunge jimbo la Mtama, aliyemaliza muda wake, amewataka Watanzania waepuke kuchezea amani au kujaribu kifo kwa vile madhara yake yatakuwa makubwa kuliko inavyofikiriwa.

Akitoa mfano, Membe alisema nchi ya Benin mwaka 1989 ilijaribu kufanya mabadiliko kwa kuanzisha kundi linalofanana na UKAWA, lakini baada ya kushinda uchaguzi mkuu, raia wake wakaanza kuuana wenyewe kwa wenyewe.

Membe pia alitoa mfano wa Burkina Faso, ambayo baada ya Thomas Sankara kufanya mapinduzi ya kijeshi, aliuawa baada ya kujitokeza muungano wa vyama vya siasa uliokusanya fisi, mende na hadi leo nchi hiyo inakabiliwa na mapigano.

"Mwaka 2008, wapinzani Kenya walianzisha muungano wa kundi la Rainbow Colliation, lakini badala ya kuleta mabadiliko, ulipofika wakati wa uchaguzi mkuu, wakaanza kupigana wenyewe kwa wenyewe na hatimaye viongozi wake kufunguliwa mashitaka kwenye Mahakama ya Uhalifu wa Kivita ya The Hague iliyoko Uholanzi.

Waziri huyo wa mambo ya nje alisema pia kuwa, katika nchi 18 za Afrika, watoto wamekuwa wakiishi kwenye mahandaki kutokana na baadhi ya viongozi wa serikali kukataa kukubali kushindwa katika uchaguzi mkuu.

Membe alikisifu Chama cha CHADEMA kwa kusema kuwa, kilipoanza harakati za siasa za vyama vingi, kilikuwa na viongozi wazuri na wanaokubalika, akiwepo Dk. Wilbroad Slaa na Zitto Kabwe, lakini hivi sasa kimeshapoteza mwelekeo.

"Leo hii CHADEMA imenunuliwa na mamluki na wasaliti wa CCM, katika hilo hawawezi kufanikiwa,"alisisitiza Membe.

AWASHANGAA SUMAYE LOWASSA

Membe alieleza kushangazwa kwake na uamuzi wa Waziri Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye na Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Kampuni ya Kufua Umeme ya Richmond, Edward Lowassa, kujitia CCM na kujiunga na UKAWA, ambapo amekiita kitendo hicho kuwa ni cha kisaliti.

Alisema Sumaye aliwahi kuwa waziri mkuu kwa miaka 10 huku Lowassa akishikilia wadhifa huo kwa miaka miwili na walikuwa na kawaida ya kuipongeza serikali bungeni kwa kazi nzuri inayofanya katika kuwaletea maendeleo wananchi, lakini sasa wamegeuka na kudai serikali haijafanya lolote.

"Hawa wote ni wasaliti na wasaliti wakipewa nchi, haitakuwa na amani, hakutakuwa na maendeleo, hakutakuwa na huduma nzuri za afya, maji na barabara,"alisema.

Membe pia alimponda Lowassa kutokana na kuwaahidi Watanzania kwamba atamrejesha Gavana wa zamani wa Benki Kuu ya Tanzania (B0T), Daudi Balal, ambaye alifariki dunia miaka kadhaa iliyopita, akidai kwamba bado yupo hai, isipokuwa amefichwa.

Alisema akiwa waziri mwenye dhamana ya kushughulikia mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa, anao ushahidi wa kutosha kwamba Balal alifariki dunia kwa ugonjwa Mei 16, 2008 na kuzikwa nchini Marekani, alikopelekwa kwa matibabu.

"Leo Lowassa anajigeuza kuwa YESU, ambaye alikuwa na uwezo wa kufufua wafu na baadhi ya watu wanamshangilia na kumuamini. Mwambieni yeye si YESU, aliyemfufua Lazaro. Kama ataweza kumleta Balal, tutampa urais, lakini hana uwezo huo. Sanasana ataleta mbwa wa zindiko,"alisema.

Membe alisema alipojitokeza kuomba kuteuliwa kugombea urais kwa tiketi ya CCM, aliahidi iwapo hatapitishwa, atamuunga mkono yeyote atakayechaguliwa na ndivyo alivyofanya kwa Magufuli.

Aidha, alisema hakuamua kuhama CCM na kujiunga na chama kingine cha siasa kwa vile kufanya hivyo ni usaliti kwa taifa. Aliwataka watanzania kumpa kura kwa wingi Dk. Magufuli ili aweze kuwaletea maendeleo wanayoyahitaji.

Alisema Dk. Magufuli amefanya mambo mengi ya maendeleo akiwa Waziri wa Ujenzi na zinginezo alizowahi kuziongoza, hivyo atakapochaguliwa kuwa rais, atakuwa na uwezo wa kufanya mambo makubwa zaidi.

MAMA SALMA: MAGUFULI AMESHAKUWA RAIS

MKE wa Rais Jakaya Kikwete, Mama Salma Kikwete, amewataka Watanzania kumpitisha Dk. Magufuli kuwa Rais wa awamu ya Tano wa Tanzania kwa vile tayari CCM imeshampitisha.

Akihutubia mkutano huo jana, Mama Salma aliyekuwa akiwachangamsha wananchi waliofurika kwenye uwanja huo kwa kuzungumza lugha ya kimachinga, alisema hakuna chama chenye uwezo wa kuleta maendeleo nchini zaidi ya CCM.

"Maendeleo ya kweli yataletwa na CCM, wapinzani bado hawajampata mtu anayeweza kuitwa rais,"alisema Mama Salma huku akishangiliwa kwa mayowe mengi na wananchi.

Alisema kama mgombea urais wa UKAWA, Edward Lowassa, alikatwa CCM kwa kukosa sifa, hawezi kufaa kushika wadhifa huo mahali kwingine kokote.

"Tunataka kumpeleka Ikulu mtu mwenye sifa na uwezo,"alisisitiza Mama Salma, ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), kupitia mkoa wa Lindi.

Alisema iwapo Watanzania watampitisha Dk. Magufuli kuwa rais, Tanzania itaweka historia ya kuwa na makamu wa rais mwanamke kwa mara ya kwanza, kupitia kwa mgombea mwenza, Samia Suluhu Hassan.

Aliwataka Watanzania kukamilisha falasafa ya mafiga matatu kwa kumchagua mgombea urais, wabunge na madiwani wa CCM ili waweze kuwaletea maendeleo kwa kushirikiana.

NAPE: LOWASSA AMEANZA KUWEWESEKA

Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, amesema mgombea urais wa UKAWA, Edward Lowassa, ameanza kuweweseka kutokana na kuwaombea kura wagombea wa CCM.

Nape alisema Lowassa alifanya hivyo katika mkutano wa kampeni wa UKAWA uliofanyika hivi karibuni katika mji wa Tarime mkoani Mara, hali inayodhihirisha kwamba ameshakubali matokeo.

Kwa mujibu wa Nape, kauli hiyo ya Lowassa, pia imedhihirisha wazi kwamba ameshaanza kupatwa na ugonjwa wa kusahau na kwamba iwapo Watanzania watampa ridhaa ya kuwaongoza, atawasahau na kuwaacha kwenye mataa.

Nape aliwataka Watanzania kuwa macho na UKAWA kutokana na kampeni yao ya kutaka kuwagawa wananchi kwa itikadi za udini na ukabila na kusisitiza kuwa hawatakuwa tayari kuona hayo yanatokea.

Alisema ujio wa CHADEMA katika mikoa ya Lindi na Mtwara, umewafanya wananchi waanze kugawanyika, ikiwa ni pamoja na wafuasi wa chama hicho kufanya vitendo vya uharibifu wa mali za viongozi wa CCM.

"Lindi sasa kumeanza kujitokeza habari ya watu kutozikana, baba na mama kutoelewana, tusiruhu siasa za aina hiyo. Tuondokane na UKAWA Oktoba 25, mwaka huu,"alisisitiza.

Nape alisema yanapotokea machafuko katika nchi yoyote, wanaokufa ni watu wa kawaida, hakuna hata ndugu wa viongozi, hivyo aliwataka Watanzania kuwa macho na watu wa aina hiyo.

"Hata kule Pemba ilitokea hivyo mwaka 1995, nendeni mkatazame orodha ya waliokufa wakati wa vurugu za uchaguzi, hakuna ndugu hata mmoja wa kiongozi wa CUF,"alisema.

Alisema vyama vya upinzani  vimeanza kufanya hujuma mkoani Lindi kwa kununua shahada za kupigia kura na kuonya kuwa, anayenunua kura kwa pesa, ipo siku anaweza kuwauza wananchi bila kujitambua.



No comments:

Post a Comment