Tuesday 22 March 2016

CCM MORO YAKUNJUA MAKUCHA, 29 WAVULIWA UANACHAMA, 21 WASIMAMISHWA UONGOZI




CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Morogoro, kimewavua uanachama wanachama 29 na kuwaondoa kwenye uongozi  wengine  21, katika ngazi mbalimbali mkoani hapa, baada ya kubainika walikisaliti Chama wakati wa uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana. 
Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro, Rojas Romuli, alisema hayo jana, wakati akitoa taarifa ya kikao cha kamati ya siasa ya mkoa kilichoketi Machi 13, mwaka huu, mjini hapa.
Alisema  adhabu hiyo ni miongoni mwa zilizotolewa kwa wanachama mbalimbali wakati wa kikao hicho, baada ya kamati ya siasa ya CCM mkoa, kupokea na kujadili tathmini ya uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani.
Romuli alisema kikao hicho kiliamua kuwaondoa kwenye uongozi baadhi ya wanachama na wengine kuwavua uanachama huku baadhi yao wakipewa onyo kali.
Alisema viongozi waliokumbwa na kadhia hiyo ni pamoja na waliokuwa makatibu wa kata, wenyeviti wa kata, wenyeviti serikali za vijiji, makatibu uenezi wa kata na wenyeviti wa vitongoji.
Wengine ni wajumbe wa halmashauri za vijiji, wajumbe wa serikali za vijiji, mabalozi wa shina, wajumbe wa kamati za siasa za kata na wanachama wa kawaida.
Alisema  wanachama na viongozi hao walikiuka taratibu za CCM na kufanya makosa mbalimbali, ikiwemo usaliti, uzembe na kutowajibika.
Aidha, alisema kikao hicho pia kilijadili na kubaini mapungufu kadhaa kwa baadhi ya wanachama na kuwavua uanachama wanachama 29 na wengine 42 kupewa onyo kali wakati wengine 13 walipewa onyo la mdomo.
Katibu huyo alisema kamati hiyo ya siasa pia imewafutia adhabu wanachama watano, kutokana na tuhuma zao kutothibitika.
Hata hivyo, alisema vikao vya mkoa na  taifa vinatarajia kufanya maamuzi ya mwisho kwa viongozi 11 wanaotuhumiwa kwa makosa mbalimbali, baada ya kujiridhisha juu ya ukweli wa tuhuma zinazowakabili.

No comments:

Post a Comment