Monday 7 March 2016

RAIS WA VIETNAM KUTUA NCHINI KESHOKUTWA




Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi Dkt. Augustine Mahiga akizungumza na waandishiwa habari kuhusu ujio wa rais wa Vietnam hapa nchini kushoto ni Mindi Kasiga Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano cha Waziri wa Mambo ya Nje

Hussein Makame-MAELEZO

RAIS wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam Truong Tan Sang anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi nchini Tanzania Machi 9 mwaka huu ikiwa ni ziara yake ya kwanza Barani Afrika tangu aingie madarakani mwaka 2011.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa Balozi Dkt. Augustine Mahiga, amesema  lengo la ziara hiyo ni kukuza uhusiano baina ya Tanzania na Vietnam ambao umedumu kwa zaidi ya miaka 50 sasa.

Alisema Rais Sang atawasili siku ya Jumatano na ataanza shughuli mbalimbali Alhamisi kwa kufanya mazungumzo rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. John Pombe Joseph Magufuli Ikulu jijini Dar-es-Salaam.

Baada ya kukutana na Rais Dkt. Magufuli, Rais Sang atasaini mkataba kuhusu masuala ya ?kodi  na baadaye atafungua maeneo mapya ya Ushirikiano wa kiuchumi baina ya Tanzania na Vietnam.

Alisema lengo la mkataba huo ni kuchochea biashara baina ya Tanzania na Vietnam ambapo wafanyabiashara wa nchi hizo hawatatozwa kodi mara mbili kwa biashara na uwekezaji watakaoufanya.

Rais Sang pia atapata fursa ya kukutana na kuzungumza na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kabla ya kutembelea eneo la EPZ la Ubungo.

Akiwa EPZA Rais Sang atatembelea viwanda mbalimbali vinavyozalisha bidhaa zinazouzwa kuuza nje ya nchi kabla ya kuhudhuria mkutano wa biashara na uwekezaji katika ukumbi wa mikutano wa Julius Nyerere.

Waziri Balozi Mahiga alisema kuwa mkutano huo unatarajiwa kuhudhuriwa na taasisi za umma na sekta binafsi kutoka Tanzania na Vietnam

Katika ziara hiyo pia atapata fursa ya kuzungumza na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Ali Mohamed Shein.

Kwa mujibu wa ratiba ya ziara hiyo, Rais Sang pia atahudhuria dhifa ya Kitaifa itakayoandaliwa kwa heshima yake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk.John Pombe Joseph Magufuli.

Kabla ya kuondoka nchini Rais Sang atatembelea moja ya mbuga za wanyama zilizopo nchini ili kujionea vivutio vya kitalii vilivyopo kwenye mbuga hiyo na kuwashawishi raia wa Vietnam kuja kutalii nchini.

Rais Truong anatarajiwa kufuatana na mke wake Bi Mai Thi Hahn, mawaziri 4 wanaoshughulika na sekta za  Kilimo, Mawasiliano Uwekezaji, Afya Viwanda na Biashara.  Aidha mgeni huyo atafuatana na ujumbe wa wafanyabiashara 30 kutoka Vietnam. 

Baada ya kuondoka nchini siku ya Ijumaa, Rais Sang anatarajiwa kwenda nchini Msumbiji kwa ziara ya kikazi.

Rais Sang wa Vietnam amezaliwa tarehe 21 January 1949 katika Jimbo la Long An nchini Vietnam na 25 Julai 2011 apochaguliwa na Bunge la Vietnam kuwa Rais wa Vietnam.

No comments:

Post a Comment