Tuesday 20 December 2016

KINARA DAWA ZA KULEVYA MBARONI





KINARA wa mtandao wa biashara za dawa za kulevya, Kambi Zubeir Seif, maarufu kwa jina la Cambiasso, ametiwa mbaroni, kufuatia msako mkali uliofanywa na Polisi Kikosi Maalumu cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, katika nyumba yake ya kifahari aliyokuwa amejificha iliyoko Tuangoma, wilayani Kigamboni, Dar es Salaam.
Cambiasso, pia inadaiwa mwaka 2011, alikamatwa na kilo 179, za dawa za kulevya aina ya heroine, akiwa na wenzake watatu, Fredy Chonde, ambaye ni Mtanzania, Muhammad Shahbaz na Abdulghan Gulam, ambao ni raia wa Pakistan.
Mfanyabiashara huyo anayemiliki nyumba za kifahari pamoja na magari, anayedawa kuwa kinara muunganishaji wa mitandao ya dawa za kulevya, alikamatwa usiku wa kuamkia Desemba 10, mwaka huu, katika operesheni kali ya kuwasaka wafanyabiashara wa dawa za kulevya nchini.
Wengine waliokamatwa kwenye msako huo ni Marashi Zuberi Seif, ambaye ni dada wa mtuhumiwa namba moja na rafiki wa kike wa Cambiasso, Grace Aseasisye, ambaye alipangiwa nyumba eneo la Yombo Buza.
Imeelezwa kuwa polisi inaendelea na msako mkali baada ya watuhumiwa wengine kukimbia, ambapo kwa mujibu wa chanzo chetu, operesheni hiyo ni mwanzo wa operesheni kubwa zitakazoendeshwa na polisi kuumaliza mtandao huo unaohatarisha nguvu kazi ya vijana.
Akizungumzia kukamatwa kwa kinara huyo, Kamanda wa Polisi wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Dawa ya Kulevya Tanzania, Kamishna Mwandamizi Msaidizi wa Polisi (SACP),  Mihayo Msikhela, alisema Cambiasso alikamatwa Ijumaa, iliyopita na kufikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
“Huyu ni kiunganishi wa mitandao hiyo. Polisi walifanikiwa kumtia nguvuni baada ya kuweka mtego nyumbani kwake na Ijumaa alishafikishwa mahakamani kujibu moja ya kesi inayomkabili,” alisema Kamanda Msikhela.
Kwenye kesi hiyo, mtuhumiwa huyo aliunganishwa katika kesi namba PI 23/2016 ya raia wa Nigeria, Bede Eke, aliyekamatwa Juni, mwaka huu, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam, akiwa na kilo tano za dawa za kulevya.
Anakabiliwa na kosa la kula njama (conspiracy) na kusafirisha dawa za kulevya pamoja na raia huyo wa Nigeria.
Msako huo ni hatua za mapambano dhidi ya mtandao huo, ambao serikali ya awamu ya tano imeahidi kuutokomeza.
Katika mkesha wa kuliombea Taifa, Desemba 31, mwaka jana, Rais Dk. John Mafuguli, alisema Taifa kwa kipindi kirefu lilikabiliwa na vigogo wauza dawa za kulevya, watumishi na vigogo wakwepaji wa kodi pamoja na wizi wa dawa hospitalini, hivyo viongozi wa dini na Watanzania wote wanapaswa kumuombea ili aweze kutumbua majipu ya mafisadi hao.
Dk. Magufuli, ambaye aliwakilishwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba, Maendeleo na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, alisema viongozi wa dini wanapaswa kuendelea kuliombea Taifa na kuwaombea watu wabaya wasiopenda maendeleo waweze kubadilika ili nchi iweze kusonga mbele.
“Viongozi wa dini tunapaswa kuendelea kumuombea rais wetu (Dk.Magufuli), aendelee kutumbua majipu haya, ambayo yanasababisha maendeleo ya Taifa letu kurudi nyuma,” alisema Lukuvi.

No comments:

Post a Comment