Sunday 29 October 2017

MVUA YALETA KIZAAZAA DAR, MMOJA AFA





MVUA kubwa iliyonyesha jijini Dar es Salaam, jana, ilisababisha mafuriko makubwa na kuua mtu mmoja, huku miundombinu nayo ikiharibika.
Maeneo yaliyoathirika zaidi ni Bonde la Mto Msimbazi, maeneo ya Jangwani na Mto Kenge, Tabata wilayani Ilala, ambako maiti ya mtu mmoja mwanaume iliopolewa.
Katika maeneo ya Tegeta, Basihaya na  Mbezi Beach,  maji yamezingira makazi ya watu na kufanya  wananchi kuzikimbia nyumba zao.
Maeneo mengi yaliyokumbwa na mafuriko hayo, nyumba zimezama kabisa na zingine maji yamefikia usawa wa paa.
Mvua hizo, zilisababisha wanafunzi 12 wa Shule ya Msingi Atlas Kampasi ya Madale, Dar es Salaam kuokolewa baada ya basi walilokuwa wamepanda kuzama katika Mto Tegeta, ulioko Goba Mtaa wa Muungano.
Hali  hiyo, imesababisha adha kubwa kwa usafiri kutokana na barabara nyingi kutopitika, ambapo Kampuni  ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART ), ililazimika  kusimamisha huduma baada ya maji kupita juu ya barabara eneo la Jangwani na mawasiliano kukatika kati ya Magomeni na Kariakoo.
Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema, ambaye alikagua maeneo yaliyoathirika na mafuriko hayo, alithibitisha mvua hiyo kuleta madhara na kutoa tahadhari kwa wananchi waishio mabondeni na maeneo hatarishi kuondoka mara moja.
“Hali sio nzuri. Serikali imekuwa ikitahadharisha wananchi kuondoka maeneo ya mabondeni mara kwa mara, lakini wananchi wamekuwa wazito kutii.
“Natoa agizo wote waondoke kwa sababu bado mvua inaendelea kunyesha, huenda kukawa na madhara makubwa,” alisema Mjema akiwa Jangwani.
Mbunge wa Ilala, Mussa Zungu, alisema mvua hiyo imesababisha uharibifu mkubwa wa mali, nyumba kuzama na miundombinu ya barabara kuharibika.
“Hatua moja tunayofanya ni kuhamasisha watu kuondoka katika maeneo hatarishi. Maji ni mengi na yanaendelea kuongezeka. Chanzo ni madaraja katika mito mingi kujaa uchafu unaozuia maji kupita kwa urahisi. Tumeomba msaada wa kuzibua mifereji na madaraja hayo,”alisema Zungu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Ilala, Salum Hamduni, alithibitisha mtu mmoja kufa maji.
“Maiti ya kijana wa umri wa miaka kati  ya 25 na 30,  iliopolewa bonde la Mto Kenge Tabata. Umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti Hospitali ya Amana,” alisema Kamanda Hamduni.
Alisema kuhusu madhara mengine yaliyopatikana, bado  polisi wanaendelea kufuatilia na watatoa taarifa zaidi.
Hata hivyo, alitahadharisha wananchi kutii maagizo ya serikali ya kuondoka katika maeneo hatarishi.
Waathirika wengi  walionekana wakitoa  mali zao katika nyumba zilizojaa maji huku wengine wakiwa wamejikusanya katika nyumba za jirani, ambazo hazikuathirika wakiwa na mizigo yao.
“Hatufahamu hatima yetu. Tumepoteza kila kitu hapa,”alisema Zainabu Omari, mkazi wa Jangwani.
WANAFUNZI WAOKOLEWA
Wanafunzi 12 wa Shule ya Msingi Atlas, Kampasi ya Madale, Dar es Salaam, waliokolewa baada ya basi walilokuwa wamepanda kuzama katika Mto Tegeta, ulioko Goba, Mtaa wa Muungano.
Basi hilo dogo aina ya Hiace, lilizama jana, saa tano asubuhi, baada ya mvua kubwa iliyonyesha maeneo mbalimbali, kusababisha baadhi ya mito, ukiwemo Mto Tegeta, kujaa na kufurika maji.
Wanafunzi hao, walikuwa wakirejeshwa nyumbani kutoka shule na walipofika eneo hilo, basi hilo lilizama kutokana na wingi wa maji katika mto huo.
Kelele za watoto hao kuomba msaada, zilisikika baada ya kukwama katikati ya mto huo huku maji yakiingia ndani ya gari kupitia madirishani.
Mashahidi wa tukio hilo, walisema dereva wa basi hilo, alionekana akiendesha kwa umakini, lakini alipofika eneo hilo, alishindwa kupita kutokana na maji ya mto huo  kukimbia kwa kasi.
“Tulianza kusikia kelele za watoto za kuomba msaada, tulijikusanya na kwenda kuwaokoa, watoto ni wadogo, ambao kwa kukisikia wana umri wa miaka mitatu
“Tunashukuru kwa umoja wetu, tumefanikiwa kuwaokoa ingawa hadi sasa gari lao halijatoka kutokana na maji yaliyojaa katika eneo hilo,”alisema Maimuna Ally.
MABASI YA DART YASIMAMA
Wakati huo huo, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (UDART), Deus Bugaywa, alitangaza kusitishwa kwa huduma ya usafiri wa mabasi hayo baada ya kufungwa kwa barabara ya Morogoro, kwa sababu ya daraja la Mto Msimbazi kujaa maji.
Hata hivyo, alisema huduma hiyo itarejeshwa baada ya hali hiyo kutengamaa.
“Tunawaomba radhi abiria wetu kwa usumbufu uliojitokeza kwani huduma hiyo ni muhimu kwa jamii na itarudi baada ya hali kukaa sawa,”alisema Bugaywa.
Mvua hizo pia zilisababisha barabara ya Morogoro, eneo la Mbezi Kibanda cha Mkaa, maji yalijaa na kusababisha magari kushindwa kupita.
Baadhi ya magari, likiwemo lori lililobeba mbao, lilionekana katikati ya daraja wakati maji yakiendelea kuongezeka.
Mbali na madhara hayo, mvua hizo pia ziliharibu daraja la Kiluvya, ambalo lilikatika na kusababisha magari yanayotumia barabara ya Morogoro, yakiwemo ya abiria, kusababisha usumbufu mkubwa ambapo baadhi yalilazimika kuzunguuka na kupitia barabara ya Msata-Bagamoyo.
NDEGE YAPATA AJALI SERENGETI
Katika tukio jingine, mvua hizo zilisababisha ndege ndogo ya abiria ya Kampuni ya Coastal Aviation, kupata ajali ilipokuwa ikijaribu kutua katika uwanja wa ndege wa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Taarifa ya kampuni hiyo ilisema, ndege hiyo ilipata ajali saa 8.30 mchana, ilipokuwa ikitaka kutua, ambapo kutokana na hali mbaya ya hewa iliyosababishwa na mvua, ilishindwa kufaya hivyo.
Iliongeza kuwa, abiria wawili na rubani ndio waliopata majeraha machache na kulazimika kupelekwa hospitali.
Chanzo cha habari kilisema majeruhi hao walipelekwa Nairobi, Kenya kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

No comments:

Post a Comment