Sunday 29 October 2017

UMEME WAMTOKEA PUANI KIGOGO TANESCO


WAZIRI wa Nishati, Dk. Medard Kalemani ameagiza kuhamishwa kwa Meneja wa kituo cha kuzalisha umeme cha Kidatu, Manfred Ndyalu kwa kushindwa kutoa taarifa mapema, baada ya kuchomoka kwa waya na kusababisha mitambo iliyobaki kuzidiwa.
Pia, amemtaka Meneja Mkuu wa Usimamizi na Uzalishaji Umeme, Abdallah Ikwassa, kuhakikisha kuwa mashine zote  zinafanyakazi, vinginevyo aachie ngazi kutokana na kutokufanya majukumu yake ipasavyo.
Vilevile, amemuagiza Naibu Mkurugenzi wa Usafirishaji, Kahitwa Bishaija, kuhakikisha mfumo wa kusambaza umeme wa Ubungo, unaanza kufanyakazi mara moja, vinginevyo ajitafakari na kuchukua hatua mara moja.
Kauli hiyo aliitoa jana, alipotembelea mitambo ya Umeme ya Ubungo na ule wa Kinyerezi 1, baada ya kutokea kwa hitilafu ya umeme, iliyosababisha kukatika kwa umeme nchi nzima.
Dk. Kalemani alisema, wanamuhamisha meneja wa kituo hicho, kutokana na uzembe alioufanya wa kushindwa kutoa taarifa mapema ya kuchomoka kwa waya na kusababisha hitilafu kwenye gridi ya taifa.
"Tumemuelekeza mkuu wake amuondoe kwenye kituo hicho mara moja ili hali hiyo isijirudie tena na ili tuwe na wafanyakazi wachache wenye uweledi," alisema.
Kuhusu Naibu Mkurugenzi wa Usafirishaji, alisema anatakiwa kujitathmini mwenyewe kutokana na kushindwa kusimamia  mfumo wa Ubungo, kuhakikisha unafanyakazi.
Pia, alisema Meneja wa Usimamizi na Uzalishaji Umeme, anatakiwa ajitafakari mwenyewe kutokana na mitambo mingi ya umeme kutofanyakazi.
"Kutokana na hali hiyo, mitambo mingi ya kuzalisha umeme na vyanzo vingi vimeshindwa kufanyakazi, lakini nashukuru Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), walitoa taarifa ya kuwaomba radhi wananchi," alisema.
Hata hivyo, alisema wanaendelea kufuatilia chanzo cha tatizo hilo ili kuweza kulitatua mara moja.
"Tumefuatilia maeneo yote ambayo tumehisi yana tatizo, tumeenda kwenye mfumo wenyewe Ubungo ili kuweza kugundua chanzo cha tatizo, lakini tumekuta mfumo bado unafanyiwa marekebisho ya kuongezewa nguvu, taratibu zinaendelea.
"Pia, tukaenda Kinyerezi 1, ambako sasa kuna mashine haifanyikazi, nayo itafanyiwa matengenezo, lakini kubwa ni valvu moja, ambayo imesababisha mtambo wa Kinyerezi ushindwe kufanyakazi, jitihada zinaendelea," alisema.
Alisema marekebisho yanaendelea na kwa sasa umeme unapatikana nchi nzima, baada ya gridi ya taifa kurejea, ambayo imerudi tangu usiku.
"Lakini hata hivyo, yapo maeneo machache ambayo hayapati umeme wa kutosha kwa sababu mtambo mmoja wa Ubungo 11, wenye uwezo wa kuzalisha umeme megawati 129, haujaanza kufanyakazi.
"Nimewaelekeza wataalamu wafanyekazi usiku na mchana leo (jana), mpaka mtambo wa Ubungo wenye megawati 129, nao uweze kufanyakazi. Wamenihakikishia kwamba, mpaka leo saa nne asubuhi, mtambo wa Ubungo 11 nao utakuwa unafanya kazi," alisema.
Kutokana na hali hiyo, alisema Wizara na TANESCO watahakikisha leo, saa 5 asubuhi, maeneo yote yaliyobaki yanapata umeme wa uhakika.
"Yale matengenezo yaliyokuwa yanaendelea ya kurekebisha mashine, nazo zitaendelea na utaratibu wake kama kawaida. Tunawaomba radhi wananchi kwa matatizo yalitokea," alisema.

No comments:

Post a Comment