Friday 14 October 2016

KIMITI: MWALIMU NYERERE HAKUPENDA MAJUNGU NA UMBEYA, ASEMA ALIWAHI KUMUULIZA ALIPATA WAPI PESA ZA KUJENGA NYUMBA DODOMA



NA MOHAMMED ISSA
OKTOBA 14, mwaka 1999, Tanzania ilipata pigo baada ya kutokea kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere kilichotokea Jijini London, Uingereza.
Msiba wa Mwalimu Nyerere licha ya kuacha simanzi na majonzi kwa familia yake, pia ulitikisa Tanzania na dunia kwa ujumla kutokana na mambo aliyoyafanya katika kipindi cha utawala wake.
Mwalimu Nyerere enzi za uhai wake, alitoa mchango mkubwa katika ukombozi wa baadhi ya nchi za bara la Afrika, hivyo alijipatia jina kutokana na mchango wake huo.
Akizungumzia msiba wa Mwalimu Nyerere, mwanasiasa mkongwe hapa nchini, Paulo Kimiti anasema mwaka 1999, baada ya Baba wa Taifa kufariki dunia, ilibidi yafanyike maandalizi ya aina mbili.
Kimiti, ambaye aliwahi kufanya kazi na Mwalimu Nyerere, akishika nafasi mbalimbali, ikiwemo uwaziri na ukuu wa mkoa kwenye mikoa mbalimbali nchini, anasema maandalizi ya kwanza yalikuwa ni ya kuupokea mwili wake kwa wakazi wa Dar es Salaam.
“Mipango hiyo ilikuwa inasimamiwa na Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, lakini utaratibu mwingine yalikuwa ni maandalizi ya mahali pa kumuhifadhi Baba wa Taifa na hapo ilikuwa lazima yafanyike nyumbani kwake alikozaliwa, Butiama,” anasimulia.
Anasema haikuwa rahisi kwa sababu mwanzoni watu wengi walikuwa wanapendekeza kuwepo utaratibu wa kuwa na mahali pamoja pa kuzikia viongozi wa taifa.
Anasema katika kutekeleza hilo, ikaamuliwa achaguliwe kiongozi mmoja na waziri mmoja, waende kwa Musoma na maandalizi yote yafanyike Butiama.
“Rais Benjamini Mkapa kipindi hicho aliniteua mimi kama Waziri wa Kazi na Vijana. Labda aliniteua kutokana na kazi yenyewe kwamba iwe wizara inayohusika na maandalizi, kwamba vijana watasaidia kuweka mambo yakawa mazuri kule,” anasema.
Anaongeza: “Mimi niliondoka mara tu baada ya mwili kuwasili Tanzania na nikaenda Butiama kushirikiana na viongozi wa kule.”
Anasema miongoni mwa viongozi alioshirikiana nao ni Chifu Japheti Wanzagi, ambaye ni mkuu wa familia ya Mwalimu Nyerere na pia kiongozi wa kabila la Wazanaki.
“Yeye ndiye aliyenisaidia sana kusimamia utaratibu mzima wa maandalizi ya mazishi. Wapo kina Jenerali Musuguri (David), anafahamika ni wazee wamekaa sana pale. Jenerali Musuguri ni kati ya majenerali wa mwanzo nchini, lakini anaishi Butiama akishirikiana na wazee wengine wa pale,” anasimulia.
Kimiti anasema kwa mkoa wa Dar es Salaam, walikuwa wakiwasiliana na Mzee Joseph Butiku, Mama Maria Nyerere na Jaji mstaafu Joseph Warioba ili wawe na uhakika wa mipango yote inayofanyika ili iwe inayokubalika na pande zote mbili.
Hata hivyo, anasema Butiama kulikuwa na matatizo ya aina tatu, kwanza ni eneo lipi azikwe Mwalimu na kwa sababu zipi tuchague eneo hilo.
“Sasa katika kuchagua sehemu yenyewe, kwanza watu walipendekeza pale ambapo wazazi wa Baba wa Taifa, yaani baba yake na mama yake Mwalimu Nyerere walipozikwa, ambako ni mbele ya nyumba yao,” anasema
Anaongeza: “Hiyo ikawa ngumu kuikubali kwa sababu huyo ni kiongozi wa taifa, lazima apate nafasi azikwe pekee yake. Huwezi kumchanganya na familia nyingine, ingawa ukweli ni baba na mama, lakini katika taratibu, lazima kiongozi huyu awe na eneo la pekee yake katika mazishi.”
Kimiti anasema eneo jingine, ambalo lilipendekezwa ni mahali ambapo yeye mwenyewe alishaweka picha yake ya kuchonga na alitaka azikwe sehemu hiyo.
“Ni kweli tulitaka tupatumie mahali hapo, lakini tukaja kugundua kwamba, sehemu hiyo makosa yalifanyika wakati wanamjengea nyumba yake. Vijana wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), walipitisha mfereji wa maji machafu sehemu hiyo, ingawaje huwezi kuuona kwa sababu uko kwa chini. Sasa tukasema hatuwezi kufanya makosa, ingawaje mzee mwenyewe alitaka sehemu kama hiyo, lakini isingewezekana kwa sababu ya hila ya mfereji huo,” amesema.
Anasema wazo la tatu, ambalo waliona ni vizuri walitumie  baada ya kushindikana sehemu mbili, wawasiliane na viongozi walioko Dar es Salaam kwa lengo la kufikia mwafaka.
Kimiti anasema walimshirikisha Mama Maria, Mzee Butiku na Jaji Warioba ili wakubaliane kuhusu jambo hilo.
 “Tulichofanya kwa kushirikiana na viongozi wa pale, tuliona Mwalimu Nyerere alikuwa na bustani yake pale pale karibu na nyumba yake, ilikuwa bustani mzuri tu. Tukaomba kibali, ikiwezekana tumzike katika eneo hilo,” anasema.
Anaongeza: “Kulikuwa na utata mkubwa, baadhi ya viongozi walisema hapana, tutakuwa tumemtupa, yuko nje ya himaya yake, lakini tukasema huwezi kusema nje ya himaya maana eneo lake limezungukwa na fensi, hivyo eneo lote lile ni lake.”
Kimiti anasema uamuzi waliofikia ni kutengeneza kaburi lake  sawa kabisa na mlango wa kuingilia,  baada ya kukubaliana na wazee wote.
“Na mimi kama kiongozi wa serikali, nikamuomba Chifu Wanzagi atusaidie kusimika fimbo mahali pale, ambalo anataka Baba  wa Taifa azikwe, ili iwe ushahidi, isionekane ni mtu mmoja ameamua azikwe wapi. Alichomeka mkuki na papo hapo tukaanza kuchimba kaburi bila kuchelewa,” anasimulia.
Anasema kuwa kaburi hilo lilianza kuchimbwa na vijana wa JKT na kwamba ndio walioshiriki kuanzia mwanzo, ikiwa ni pamoja na kulijengea.
Kimiti anasema wakati akiwa Butiama, alipewa majukumu ya kukaimu nafasi ya mkuu wa mkoa wa Mara kwa muda ili awe Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa huo.
Anasema huwezi kufanya kazi hiyo bila ya kuwa na kibali maalumu na ndipo alipopewa barua hiyo ikieleza kuwa, pamoja kwamba alikuwa waziri, pia awe mkuu wa mkoa wa Mara kwa kipindi hicho.
Kimiti amemtaja Mkuu wa Mkoa wa Mara, aliyekuwepo wakati huo kuwa ni Lugoye, ambaye hali yake ya afya haikuwa nzuri na kwamba, asingeweza kusimamia majukumu hayo ipasavyo.
Anasema aliendelea kuchukua madaraka ya ukuu wa mkoa kwa kipindi chote hicho na kwamba, alifanya mikutano ya hadhara wilayani Musoma ili kuwaeleza wananchi ratiba mzima itakayotumika katika kumuhifadhi Baba wa Taifa.
“Tulifanya mikutano, wazee waliuliza maswali na baadhi ya wazee walitaka mwili wa Baba wa Taifa ukifika Musoma Mjini, wapewe heshima ya kumuona pale pale uwanjani. Lakini niliwakatalia, nikasema huwezi kuufanya mwili wa Baba wa Taifa kama Mwenge wa Uhuru, kuzunguka huku na huko,” anasema.
Anaongeza: “Watu wengi walikuwa wameomba mwili wa Baba wa Taifa uende katika mikoa mingine. Dodoma waliomba, Tabora waliomba,  Mwanza waliomba mwili upelekwe wakamuone, lakini nikasema hapana, mwenye shida atakwenda Butiama.”
Kimiti anasema baada ya kuelewana na wazee wa Musoma na kukamilika kwa maandalizi yote muhimu, walikuwa wanajiandaa kwa ajili ya kuupokea mwili wake.
Anasema mambo ya usafiri yalikuwa tayari na hapo aliwaeleza wananchi kwamba, watatoa nafasi ya kuuaga mwili nyumbani kwa Baba wa Taifa.
“Mwili wake uliletwa jioni kwa ndege, ukiwa na viongozi wengi sana, lakini tulikuwa tumejiandaa vizuri, tulikuwa na usafiri wa kutosha, hivyo tukauchukua mwili mpaka nyumbani kwake,” anasema.
Anaongeza: “Siku hiyo ilikuwa ngumu, kulikuwa na manyunyu, mtikisiko ambapo watu wengi walishangaa, kwani kipindi chote walichokuwa wamekaa Butiama, mambo hayo hayakutokea, lakini walimuachia Mwenyezi Mungu kwani yeye ndiye anayejua kila kitu.”
Anasema mipango iliendelea na kwamba waliamua kwa kipindi chote watoe nafasi ya siku mbili ili wananchi wapate fursa ya kutoa heshima za mwisho.
Kimiti anasema wananchi wa mikoa ya karibu walifika wilayani Butiama kwa ajili ya kutoa heshima zao za mwisho.
Akizungumzia siku ya mazishi, Kimiti anasema maandalizi yalianza asubuhi na waliohusika na askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na kwamba, upande wa ibada ulisimamiwa na Kanisa Katoliki, ambapo Muadhama Policapy Kardinali Pengo, alisimamia shughuli zote za misa, kuanzia kanisani Butiama hadi kaburini.
Kimiti anasema siku hiyo yeye alikuwa mshereheshaji, kuanzia kanisani mpaka kaburini na kwamba, aliwaanda viongozi wakuu na familia kuweka mashada ya maua.
“Suala hilo lilichukua muda wa kutosha kuanzia asubuhi mpaka mchana, karibuni saa nane na ilipofika saa tisa au kumi hivi, tulikuwa tumemaliza kwani viongozi wengi walirudi siku hiyo hiyo na tukabaki kama familia tu,” anasema.
Anasema baada ya siku mbili, nao walirudi na kuwaacha wanajeshi kulinda kaburi hilo mpaka wakati walipolijengea upya kwani lilikuwa la muda.
Kimiti anasema baada ya miezi miwili, ilipofika Desemba, 1999, Rais wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, alitembelea Tanzania na kwamba Rais Mkapa alimteua kusafiri naye hadi Butiama.
Anasema Baba wa Taifa alikuwa na mvuto kwa wananchi wengi kwa sababu alikuwa na haiba mbele ya jamii na alikuwa akipenda watu.
“Baba wa Taifa alikuwa mtu wa watu, alikuwa anapenda watu na siku zote ukipenda watu nao watakupenda. Hakutaka mtu mwingine aonewe ama aonekane anadharauliwa mbele ya wengine bila sababu ya msingi,” anasema.
Anaongeza: “Mwalimu alikuwa mcha Mungu kila wakati, sasa tabia hiyo iliwafanya watoto kwa wakubwa, kila mmoja kumpenda.”
Kimiti anasema atamkumbuka Mwalimu Nyerere kwa sababu ya mapenzi yake kwa taifa, ambapo hakutaka kuliona taifa linakuwa masikini, kwani alitaka watu wote wawe na hali mzuri ya maisha.
Anataja sababu ya pili kwamba, Mwalimu Nyerere hakupenda kusikia maneno bila ya kufuatilia yeye mwenyewe.
“Mwalimu Nyerere hakupenda umbea. Alipokuwa anasikia kitu, alikuwa anakuita na kukuliza ili umpe uthibitisho. Mimi yaliwahi kunitokea. Aliposikia ninajenga nyumba Dodoma, nikaitwa na kuulizwa unajenga nyumba, umepata wapi hela. Wewe ni waziri wangu, najua mshahara wako, hizi hela umepata wapi, hebu niambie,” anasimulia.
Anaongeza: “Kwa bahati nzuri nilikuwa nimepata mkopo kutoka Benki ya Nyumba wakati huo, ikawa ndio ponyaponya yangu.”
“Usipokuwa na kiongozi, ambaye anafuatilia mambo, majungu yanaweza kuharibu na watu wakashindwa kufanya kazi kwa sababu ya majungu. Ndio maana watu wengi walikuwa wanaogopa kumpelekea uongo Mwalimu kwani ukimpelekea uongo atajua tu na atamwita muhusika ili amueleze ukweli,” anasema Kimiti.
Anasema pia kuwa alikuwa anampenda Mwalimu kwa sababu mara nyingi alikuwa anawaonya kwamba, wachezee mshahara wao, kamwe wasichezee kazi.
“Watu wanaweza kuchukulia jambo rahisi, lakini maneno hayo yalikuwa na maana, kwani ukichezea mshahara, unaweza ukaupata siku nyingine, lakini kazi ukiichezea, hata huo mshahara huutaupata,” anasema.
Kimiti anasema ilikuwa vigumu kumfananisha Mwalimu Nyerere na kiongozi mwingine yeyote kwani alikuwa na uwezo mkubwa wa kufanya kazi.
Mwanasiasa huyo mkongwe amewataka viongozi mbalimbali nchini, kuwa watumishi wa watu kwani wakitekeleza hilo, watafanikiwa zaidi.
Akizungumzia utendaji wa mawaziri wa serikali ya awamu ya tano, amewataka wafanye kazi kwa bidii kubwa bila ya kuwa na wasiwasi wa kuogopa kufukuzwa.
“Mawaziri lazima watambue kwamba, Rais Dk. John Magufuli amewaamini, hivyo jukumu lao ni kufanya kazi bila ya wasiwasi wa kuogopa kufukuzwa, badala yake wazingatie kiapo walichoapa,” anasema.
Anasema mawaziri hao kupewa dhamana na Rais Magufuli siyo kwamba amewajaribu, bali amewaamini, hivyo wajibu wao ni kutekeleza na kufanya kazi kwa misingi na falsafa ya serikali ya awamu ya tano ya ‘Hapa Kazi Tu’.
Kuhusu utendaji wa Rais Magufuli, Kimiti amesema anafanya kazi kubwa na nzuri na kwamba, anatanguliza upendo katika kutekeleza majukumu yake.
Anasema Rais Magufuli anafanya kazi bila ya kujali kabila, dini, rangi, chama na muda wote anataka watu waishi kama familia moja.
AMETOKEA WAPI?
Akizungumzia historia yake kwa ufupi, Kimiti anasema alizaliwa mjini Sumbawanga, mwaka 1940 na alipata elimu yake ya msingi wilayani humo mkoani Rukwa.
Kimiti anasema elimu ya sekondari aliipata Mzumbe na kwamba, shahada ya kwanza alichukua nchini Uholanzi, ambapo shahada ya pili aliipata nchini Marekani.
Anasema kitaaluma ni mtaalamu wa kilimo, ambapo mwaka 1980, alichaguliwa kuwa mbunge wa taifa na miaka miwili badaye, alichaguliwa kuwa Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu.
Kimiti anasema mwaka 1984, aliteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro na mwaka 1989 hadi 1991, alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera.
Mwaka 1991 hadi 1995, alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya na  mwaka 1995 hadi 1998, alikuwa Waziri wa Kilimo na Ushirika.
Kuanzia mwaka 1998 hadi 2000, alikuwa Waziri wa Kazi na Vijana na kuanzia mwaka 2000 hadi 2004, alikuwa Mwenyekiti wa Kamisheni ya Idadi ya Watu ya Umoja wa Afrika (AU), ambapo alistaafu rasmi kwa hiari yake mwaka 2010.
0000000

No comments:

Post a Comment