Monday 24 October 2016

MFALME WA MOROCCO ATUA NCHINI




MFALME wa Morocco, Mohammed VI, amewasili nchini kwa ziara ya kiserikali.

Mfalme huyo aliwasili jana, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa JK Nyerere, jijini Dar es Salaam, akiongoza msafara wenye watu zaidi ya 150.

Uwanjani hapo, Mfalme Mohamed VI, alilakiwa na mwenyeji wake, Rais Dk. John Magufuli, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na viongozi wengine mbalimbali.

Baada ya ndege iliyombeba kutua uwanjani hapo, alipigiwa miziga 21, iliyoambatana na upigwaji wa nyimbo za mataifa hayo na baadae kukagua vikundi vya ngoma vilivyokuwa vikitumbuiza kwenye mapokezi yake.

Akiwa nchini, Mfalme Mohamed VI anatarajiwa kushiriki shughuli mbalimbali, ikiwemo mazungumzo na mwenyeji wake Rais Dk. John Magufuli kisha kutembelea maeneo mbalimbali ya kitalii.

Aidha, akiwa nchini, atatiliana saini mikataba 11, ikiwemo ya kilimo, siasa,  nishati na madini, uvuvi na utalii.

Pia, ataweka jiwe la msingi la ujenzi wa msikiti mkubwa wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), unaoambatana na jengo pacha kwa ajili ya madrasa.

No comments:

Post a Comment