Sunday 30 August 2015

DK. MAGUFULI: NITAENDESHA NCHI KISAYANSI, UFISADI HAPANA

 Mwenyekiti wa Shirikisho la vyama vya Watu wenye ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) Amon Anastaz Mpanju akisalimia wakazi wa Iwawa kwenye mkutano wa Kampeni za CCM uliofanyika stendi ya Mabehewani Makete
 Mgombea wa Urais kwa kupitia Chama Cha Mapinduzi Dk. John Pombe Magufuli akihutubia wakazi wa kijiji cha Kikondo kata ya Ilungu Mbeya vijijini akiwa njiani kuelekea mkoa wa Njombe
Umati wa wananchi waliohudhuria mkutano huo

Mgombea wa Urais kwa kupitia Chama Cha Mapinduzi Dk. John Pombe Magufuli akihutubia wakazi wa kijiji cha Ujuni Makete mkoani Njombe .


Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Mhe. Wiliam Lukuvi akihutubia wakazi wa njombe mjini kwenye uwanaja wa Saba Saba
Mgombea wa Urais kwa kupitia Chama Cha Mapinduzi Dk. John Pombe Magufuli akimkabidhi mgombea Ubunge wa Jimbo la Wanging'ombe  Eng.Gerson Lwenge ilani ya uchaguzi ya CCM
 Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara) Philip Mangula (kushoto) akiwa na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Njombe Ndugu Deo Sanga na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Mhe. Wiliam Lukuvi  wakimsikiliza Mgombea wa Urais kwa kupitia Chama Cha Mapinduzi Dk. John Pombe Magufuli kwenye mkutano wake katika wilaya ya Wanging'ombe
NA SELINA WILSON, NJOMBE

MGOMBEA Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, amesema akipata ridhaa ya wananchi, ataendesha nchi kisayansi na hatawapa nafasi mafisadi na wala rushwa wafanye watakavyo.

Amesema anajua mafisadi hawatampigia kura, lakini anawaomba wananchi nyingi za kutosha ili aweze kuwa Rais ashughulike nao kuhakikisha rasilimali za nchi zinawanufaisha Watanzania.

Dk. Magufuli alisema hayo jana kwa nyakati tofauti katika maeneo mbalimbali ya wilaya za mkoa wa Njombe kwenye mikutano ya kampeni za uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.

Alisema anatambua kero za wananchi kuwa huduma muhimu kama vile barabara, elimu, maji, afya na uchumi na kwamba, atahakikisha anazifikisha kwa wananchi kwa kuwa fedha zipo isipokuwa kuna watu wachache wanaofanya ufisadi.

“Kuna watu wanasema wanataka kuing’oa CCM madarakani, lakini niwape wosia kwamba kitanda chako kikiwa na kunguni huwezi kukitupa kitanda na badala yake unatakiwa kuwatafuta kunguni watatu waliopo unawaua unaendelea kulala na mkeo,”alisema.

Dk. Magufuli aliwataka wananchi wasiiadhibu CCM kwa ajili ya mafisadi na wala rushwa wachache ambao waliposikia ameteuliwa kuwania urais wamekimbia, hivyo ataendelea kusafisha na waliopo kama wanatakakubaki salama watubu na waendane na kasi ya kuleta maendeleo.

Aliwaambia wananchi kuwa atazingatia maslahi ya watu wote wakiwemo wafanyakazi, wafanyabiashara, wanafunzi, wakulima na watu wa makundi mengine.

“Kwanza nataka niwaambie mimi ni mwalimu, mke wangu ni mwalimu. Kwa hiyo kwa walimu mimi ni shemeji yenu kotekote,”alisema.

Dk. Magufuli alisema atafanya kazi kwa karibu na waandishi wa habari kutokana na kazi kubwa wanayofanya ya kuhabarisha wananchi.

“Ndugu zangu waandishi wa habari mnafanya kazi kubwa na ahadi yangu kwenu nikishinda uchaguzi nikiwa Rais nawaahidi nitakuwa pamoja nanyi,”alisema.

UVAMIZI VITUO VYA POLISI

Alionyeshwa kukerwa na kitendo cha uvamizi katika vituo vya polisi na kueleza akiingia Ikulu atahakikisha anaboresha maslahi ya polisi ili wafanye kazi zao kwa ufanisi.

“Askari polisi wanatulinda, nataka wafanye kazi zao vizuri. Wasikose hela ya chakula ili wasilale vituoni wakaja watu wakachukua SMG.
Nazungumza kwa upole nataka jeshi liheshimike, watu wanachukua silaha wakati na polisi wana silaha.

“Jambazi akija unatakiwa kumuwasha kwa kuwa yeye naye anakuja kukuwasha. Inawezekana maneno yangu ni makali, lakini ndio hivyo,” alisisitiza.

Dk. Magufuli alisema askari wanalinda benki wanatoka hawana hela ya kununua mboga na ndio maana anakuja jambazi askari yuko na silaha anaogopa hata kumpiga risasi kwa kuogopa kushitakiwa.

“Wakati wangu jambazi akija chapa chapa, nataka watu wafanye kazi, watu wafungue maduka usiku na afungue pale anapotaka,”alisema.

Alisema kinachotakiwa ni kuzingatia sheria lakini Jeshi la Polisi linapaswa kuheshimika.

Pia Dk. Magufuli alimpongeza Rais Kikwete kwa kuanzisha mkoa mpya wa Njombe na ilikuwa ni mapenzi makubwa ya CCM kusogeza maendeleo karibu na wananchi.

Alisema Rais Kikwete ameshaanzisha mkoa na kinachotakiwa ni kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo na Njombe inajengwa na kufunguka kibiashara.

Dk. Magufuli alimnadi mgombea ubunge wa Wanging`ombe, Naibu Waziri wa Ujenzi, Gerson Lwenge na kuwaeleza wananchi kwamba ni mchapakazi hodari.

“Nimefanya kazi na Lwenge namfahamu. Naomba mniletee ili nifanye kazi naye akamilishe ujenzi wa barabara kutoka Njombe, Makete hadi Mbeya ili wafanyabiashara waweze kusafirisha mazao yao na wapate maendeleo,”alisema.

Akiwa Makete alimnadi, Dk. Noman Sigala na kuwaomba wananchi wamchague ili apate mtu wa kufanya naye kazi na kuibadilisha Makete ambayo bado ipo nyuma kimaendeleo.

MANGULA AWAKOSHA WALIMU

Katika hatua nyingine, Makamu Mwenyekiti wa CCM Taifa (Bara), Philip Mangula, akizungumza katika Uwanja wa Sabasaba mjini Njombe, alisema Rais Jakaya Kikwete anaondoka madarakani na kuwaachia mwalimu mwenzao.

“Walimu mpoo. Nakumbuka Rais Kikwete akiwa kwenye sherehe za walimu jijini Mwanza kwenye sherehe za Siku ya Wafanyakazi Mei mosi, mwaka huu, walimu mlimtania mkaamuliza ‘shemeji unatuachaje’,” alisema.

Mangula alisema sasa Rais Kikwete, amewapa majibu kwamba anawaachia mwalimu mwenzeo.

Alisema CCM imemleta Dk. Magufuli ambaye ni mwalimu aliyesoma masomo ya hesabu na sayansi na anayeaminika kwa kuwa mchapa kazi.

AWANANGA WAZUSHI

Katika hatua nyingine, Dk. Magufuli aliwazodoa waliomzushia kwenye mitandao ya jamii kwamba amelazwa ICU na kwamba, taarifa hizo hazina ukweli.

Alisema uzushi huo hauna tija kwa kuwa amekamilisha mikutano yake Mbeya na amepokelewa na wananchi wa vyama vyote, hivyo wenye lengo kumchafua wameshindwa.

Mgombea huyo aliesema ni mzima wa afya na kilichotokea ni kwamba alikwenda Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa Mbeya kumuona Meya mstaafu wa Jiji la Mbeya, Atanad Kapunga, aliyelazwa baada ya kujeruhiwa ajalini.

Dk.Magufuli alisema hayo jana wakati akizungumza na viongozi wa mkoa huo baada ya kuhitimisha ziara yake, ambapo aliwashukuru kwa mapokezi na mikutano ya kampeni kwa mafanikio makubwa.

Alisema ameshangazwa na taarifa zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kwamba ameugua na amelazwa ICU.

“Nawapa pole viongozi na wananchi kwa tukio la ajali iliyotokea siku nne zilizopita wakati viongozi walipokuja kunipokea nikitoka Nzoka. Gari moja alilopanda meya huyo likapata ajali.

Katika ajali hiyo mwanachama mmoja wa CCM alifariki dunia na wengine watatu walijeruhiwa. Niliacha shughuli zangu nikaenda hospitali kumuona meya na hali yake inaendelea vizuri,"alisema.

Dk.Magufuli alisema kwa ubinadamu wa kawaida na kwa watu wanaomjua Mungu ilikuwa ni lazima kwenda kumuona mgonjwa huyo.

Alisema yeye ni mzima wa afya na anaendelea kupiga kazi na lengo lake ni kuwaletea maendeleo Watanzania na kuleta mabadiliko ya kweli.

Dk.Magufuli akiwatubia wananchi wa jimbo la Makete katika  uwanja wa Iwawa aliwaahidi wananchi kwamba serikali yake itajenga barabara ya lami ya Njombe/Makete hadi Mbeya.

Aliwaomba wananchi wamchague kwa kura nyingi ili aweze kutekeleza azma yake ya kuwaletea Watanzania maendeleo bila kujali itikadi zao za vyama.

No comments:

Post a Comment