Thursday 8 October 2015

SUMAYE NA NETGROUP SOLUTION, LOWASSA NA RICHMOND, KWELI MABADILIKO NI LAZIMA




MWENYEKITI wa Taifa wa CHADEMA, Freeman Mbowe, anataka kuleta machafuko nchini na hotuba zake za kichochezi na zinazoashiria hali ya kukata tamaa ndizo zinazonifanya kusema hivyo.
Tuirejee hotuba yake ya hivi karibuni ambayo aliitoa wakati akiwahutubia Waislamu kwenye Baraza la Idd la Mfungo Tatu jijini Dar es Salaam.
Hotuba yake ilipewa uzito mkubwa na gazeti moja litolewalo kila siku ambalo lilimnukuu Mbowe kwa  kuandika “Mbowe amuonya Kikwete.”  
Mbowe anasema Rais Kikwete asicheze na uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu, kwani akifanya hivyo ataliingiza Taifa kwenye matatizo makubwa.
Kwanza inabidi tuhoji mantiki ya Mbowe kwenda kusema masuala ya uchaguzi kwenye hafla ya kidini, Je, Mbowe alilenga nini kama sio kufanya kampeni kwa kutumia jukwaa la dini?
Mbowe anasema “ndugu zangu Waislamu, namuonya Rais Kikwete asicheze na uchaguzi wa mwaka huu.” Kulikuwa na ulazima gani wa Mbowe kumuonya Kikwete kwa kutumia mimbari ya dini?
Je, Mbowe hangeweza kuyasema akiwa kwenye mikutano ya kampeni za UKAWA? Ni wazi kwamba aliwalenga Waislamu kwa kusudi maalumu.
Hii ni safari ya pili kwa UKAWA kufanya kosa la kuzigeuza nyumba za ibada kuwa jukwaa la kampeni kwa lengo la kunasa kura za waumini.
Mara ya kwanza ni pale mgombea urais wa UKAWA, Edward Lowassa alipokuwa Tabora akiwa kanisani alinukuliwa kuomba Walutheri wamwombee kwa kuwa tangu nchi hii ipate uhuru imekuwa ikitawaliwa na marais Wakatoliki, Nyerere alikuwa Mkatoliki, Mkapa Mkatoliki, safari hii ni zamu ya Walutheri.
Wananchi wengi wenye kuitakia mema Tanzania waliilaani kauli hiyo inayoashiria ubaguzi wa itikadi za udhehebu wenye lengo la kuvuta kura za huruma kutoka kwa waumini wa dhehebu moja.
Hivyo kitendo cha Mbowe kuhubiri siasa kwenye  sherehe za Idd ya Mfungo Tatu hakikutokea kwa bahati mbaya, bali kilikusudiwa, kilipangwa tangu awali na kudhamiriwa kutekelezwa kwa lengo maalumu la kupata kura za huruma kutoka kwa Waislamu na papo hapo kumfitinisha Rais Kikwete na Waislamu.
Maana Mbowe anaposema ndugu zangu Waislamu namuonya Rais Kikwete asicheze na uchaguzi mkuu wa mwaka huu ni kama anamshitaki Rais Kikwete kwa Waislamu.
Kama kweli Mbowe hakukusudia kumshitaki Rais Kikwete kwa Waislamu, basi alidhamiria kuwadhihaki Waislamu kwasababu Kikwete ni Mwislamu, kwahiyo Mbowe ni kama alipeleka ujumbe kutoka kwa UKAWA yenye mgombea Mlutheri kwenda kwa Waislamu kuonya kwamba ‘angalieni Mwislamu mwenzenu anacheza na uchaguzi mkuu wa Oktoba 25 mwaka huu’.
Amebadilisha wakurugenzi wote katika Tume ya Uchaguzi, Tume iliyopo siyo ile ya mwaka uliopita na amefanya hivyo huku ukiwa umebaki mwezi mmoja tu uchaguzi ufanyike.
Je, utendaji wa Rais Kikwete kama kiongozi mkuu wa serikali unahusikaje na dini yake hadi mabadiliko ya kiserikali yajadiliwe kwenye Baraza la Idd?
Mbowe alikuwa na maana gani kukosoa utendaji wa serikali kwenye hafla ya kidini? Ni ujumbe wa aina gani ambao kiongozi huyo  alikusudia kuwafikishia Waislamu wakati wanasherehekea Idd?
Mbowe aliendelea kusema “hivi karibuni watu wa usalama walifika ofisi za tume hiyo na kumbeba mkurugenzi aliyebaki wakakaa naye kwa siku tatu aliporudi wakamwamrisha akabidhi ofisi, sasa tume inaongozwa na vyombo vya dola”.
Je, maneno ya aina hii ndiyo yanayostahili kwenye mkutano wa dini? Kwanini Mbowe hakuitisha mkutano na wanahabari ili atoe dukuduku lake?
Yawezekana aliogopa maswali kutoka kwa wanahabari, akaona ayaongelee hayo kwenye Baraza la Idd kwa kuwa hatahojiwa chochote, waislamu wataishia kuwa wasikilizaji.
Mbowe anaendelea kumshitaki Kikwete kwa Waislamu akisema Rais Kikwete ajue kuwa usalama wa nchi hii umo mikononi mwa wananchi hivyo, wakiamua wanaweza kufanya lolote. 
Hii ni lugha ya uchochezi inayotufanya tuamini kwamba Mbowe alidhamiria kuwashirikisha baadhi ya waislamu wajumuike kwenye uamuzi wao yaani wajumuike kuunga hicho walichokiamua kwa siri viongozi wa UKAWA.
Yaelekea viongozi wa UKAWA wamekwishaamua kwamba wasipoingia madarakani mwaka huu lazima vurugu itokee. Nasi watanzania wenye nia njema tunawaeleza na tunawaonya kwamba uongozi wa nchi hii umo mikononi mwa wananchi, ni wananchi ndio wanaoamua nani awe Rais wao.
Kwahiyo, wao UKAWA hawana haki ya kuamua kwamba iwe isiwe lazima mwaka huu waingie Ikulu, wanaoamua nani aingie Ikulu ni wananchi na uamuzi wao ni wa mwisho.
Mbowe aliendelea kusema “Rais Kikwete anapaswa kuwaacha watanzania waamue wenyewe kwa kumchagua mtu wanayempenda akishinda apewe haki na si kumnyima.”
Hapa kuna swali, Mbowe anajua wananchi wanampenda nani na kumchukia nani? Ana kipimo gani cha kujua wananchi wanampenda fulani na kumchukia fulani wakati haijawahi kuitishwa kura ya maoni nani anachukiwa na nani anapendwa?
Mbowe aliendelea kuwaambia waislamu akisema “kwa muda mrefu watanzania wamekuwa wakionewa kwa kukosa haki,  wakinyonywa, sasa wamesema basi, muda umefika wa kulikomboa Taifa la Tanzania kwa njia ya sanduku la kura”.
Mbowe anawakumbusha waislamu uonezi na mauaji ya Mwembechai ya mwaka 1998 ambapo Sumaye alikuwa waziri Mkuu. Askari waliingia msikitini na viatu. Je, akina Sumaye na Lowassa ndio wa kuwakomboa watanzania na uonezi?
Lowasa akiwa Waziri wa Nchi katika ofisi ya waziri mkuu ndiye aliyesaini makubaliano ya MOU (Memorandum of Understanding) ambayo baadhi ya waislamu wanayalalamikia, leo Mbowe anataka kuwahadaa Waislamu kwamba Lowassa atakuwa mkombozi wao.
Mbowe anazungumzia ukombozi kupitia sanduku la kura kwani ni lini watanzania walipata uongozi nje ya sanduku la kura?
Tangu 1958 wananchi wa nchi hii wameshiriki kwenye uchaguzi mkuu uliowawezesha kuwapata viongozi wao, kwa mara ya mwisho 2010 ambapo wamempata Rais Kikwete kupitia sanduku la kura.
Kwa hiyo, uchaguzi wa mwaka huu (2015) una tofauti gani na chaguzi zilizopita? Watanzania hawachagui kiongozi wa dini, bali wanamchagua Rais ambaye ataunda serikali itakayotawala katika misingi ya Katiba na Sheria.
Kisiasa Rais ataongoza serikali inayotekeleza ilani ya uchaguzi na sera zilizonadiwa wakati wa kampeni na zilizoiwezesha kushinda na kuingia madarakani.
Kwahiyo, kama kweli Mbowe amedhamiria kuwaletea Waislamu ukombozi, angenadi sera za UKAWA na kuthibitisha jinsi zitakavyowakomboa Waislamu.
Kwakuwa hakufanya hivyo akaishia kukosoa utendaji wa serikali naweza kusema Mbowe aliwauzia Waislamu bidhaa iliyofichwa ndani ya gunia, haijulikani UKAWA ikiingia madarakani watawafanyia nini Waislamu wa nchi hii?
Turejee kwenye hoja yake kuhusu uhamisho na mabadiliko ya wakurugenzi wa Tume.Ilivyo Tume ni asasi ya dola inayojiendesha kwa uhuru.
Lakini tume haijiundi yenyewe, wala haijiendeshi nje ya misingi na taratibu za utumishi wa umma yaani (Public Services na Civil Services). Kwahiyo, serikali inayo haki ya kuwahamisha na kuwabadilisha.
Serikali siyo mgombea, wala serikali siyo chama kilichoko kwenye ushindani wa kisiasa kwahiyo inapotokea serikali imemhamisha mkuu wa mkoa kutoka eneo moja la nchi kwenda eneo jingine ama inapombadilisha kazi ikampa kazi zingine au kumstaafisha hayo ni mambo ya kawaida kwenye utumishi (Civil service).
Yanaweza kufanywa wakati wowote pasipo kujali mazingira ya kisiasa kwa sababu serikali haiongozwi wala kusukumwa na mazingira ya kisiasa.
Kwa ajili hiyo wako akina Mbowe na timu ya UKAWA waishie kumvaa Magufuli, kama wameishiwa na hoja za kushindana na mgombea huyo wa CCM wasitafute upenyo kwa kuivaa serikali.
Waiache serikali  iendelee na utendaji wake kwani duniani kote haitokei serikali ikaacha kufanya kazi zake kwa kuwahofia wanasiasa. Serikali kubadilisha Wakurugenzi ni masuala ya ndani sawa na wao CHADEMA walivyo na masuala yao ya ndani.
Mnamo mwezi Februari na Aprili 2015 walimpitisha Dk. Wilbroad Slaa kama mgombea wao wa baadaye lakini ulipofika mwezi Julai 27 ghafla wakabadilisha na kumweka Lowassa waliyemuorodhesha kama fisadi namba 9 kwenye orodha yao ya Mwembe Yanga waliyoiita “List of shame”.
Je, hayo si mabadiliko yao ya mambo ya ndani? Kwani serikali haina haki ya kufanya mabadiliko kwa kadri inavyoona? Hofu ya Mbowe ni nini kuhusiana na mabadiliko hayo? Je, yeye alitaka mambo yaweje au yafanyike vipi ili aweze kukubali na kufurahi?
Inavyoelekea Mbowe na timu nzima ya UKAWA wana hofu ya kushindwa kwenye uchaguzi mkuu unaotazamiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu, kwahiyo wanatafuta upenyo wa kutokea.
Nasema haya kwa kuzingatia kauli ya Mbowe aliyoitoa siku za nyuma na kujiapisha kwamba safari hii kama CHADEMA isipochukua nchi atajiuzulu uenyekiti.
Kwahiyo, inawezekana Mbowe na timu nzima ya UKAWA wamejiona hawana hoja za kupiku hoja za Magufuli kwahiyo wanataka kuandaa mazingira yatakayohalalisha kushindwa kwao.
Maana Wakurugenzi sio ndio wanaomfanya mgombea yeyote ashinde, kwanini Mbowe aguswe na mabadiliko yao?
Mbowe anadai kwa muda mrefu watanzania wamenyonywa, je, wamenyonywa na nani? Wamenyonywa na watawala?
Yeye Mbowe ambavyo amekuwa mbunge wa Hai kwa miaka kumi na mitano amewanyonya kiasi gani wananchi wa Hai?
Mbowe amemaliza hotuba yake kwa kudai kwamba CCM wamekuwa wakiendesha nchi kwa kufanya ufisadi mkubwa baada ya kulifilisi shirika la umeme na kusababisha nchi kuingia kwenye mgawo wa umeme.
Ni kweli enzi za utawala wa Mwalimu Nyerere Tanzania haikuwahi kuonja mgawo wa umeme licha ya kutokea mazingira magumu kama ya ukame wa 1974.
Tanzania kwa wakati huo ilikuwa na viwanda vingi vilivyotumia umeme, lakini watanzania hawakuumizwa na bili kubwa za umeme kwa matumizi ya nyumbani.
Matatizo ya umeme tumeanza kuyaonja mara baada ya ujio wa Netgroup Solutions iliyoletwa kama dili ya wakubwa enzi Sumaye akiwa Waziri Mkuu.
Makali ya umeme tumeyaonja baada ya ujio wa Richmond ambayo haikuwa na sifa za kuzalisha umeme, lakini bado Lowassa kama Waziri mkuu aliingilia mchakato wa TANESCO wa kutoa zabuni, hakusikiliza ushauri wa wataalamu  wa TANESCO walioiona Richmond haina sifa sawa na waombaji wengine, ikaamua itangaze upya zabuni ili kuwapata wenye uwezo.
Lowassa aliitisha orodha ya wazabuni wote ofisini kwake kama Waziri mkuu na ndipo Richmond ilipoibuka kidedea wakati wataalamu waliikataa.
Mbowe anakiri ukweli kwamba baada ya utawala wa Nyerere (1960-1985) watanzania hatukuonja matatizo ya umeme, bali tumeanza kuwa na umeme wa kuungaunga baada ya ujio wa kampuni mbili za Netgroup Solution na Richmond ambazo zimeifilisi TANESCO.
Hapa ndipo linaibuka swali ‘Sumaye kampeni’ meneja wa UKAWA na Netgroup Solution na Lowassa aliye mgombea wa UKAWA na Richmond, kweli hawa ndio wa kuleta ukombozi nchini?
Kweli hawa ndio wa kuwakomboa watanzania na kuwaondolea madhara ya kunyonywa na kufukarishwa? Watawakomboa watanzania kwa mbinu gani na kwa msukumo upi?
Walipokuwa madarakani kwenye nafasi ya Uwaziri Mkuu walisukumwa kujitajirisha zaidi ndio maana walibuni miradi hewa kama ya “Speed governor”, Netgroup Solution, na Richmond. Leo hawawezi kuwashawishi watanzania wenye kumbukumbu zao wawaamini na kuwakabidhi nchi.
Walipokuwa madarakani hawakuwasikiliza wananchi, watakapoingia tena hawatamsikiliza yeyote.
Sumaye hakuwasikiliza wafanyakazi wa TANESCO ambao waliomba kwamba ikiwa TANESCO inawekwa chini ya menejimeti mpya, basi wao walipwe mafao yao.
Lowassa naye hakuwasikiliza wataalamu wa TANESCO walioiona kampuni ya Richmond haina sifa ya kupewa tenda ya kuwapatia watanzania umeme.
Je, hawa kweli ndio wanastahili kuitwa wakombozi kwasababutu ya kuhubiri mabadiliko? Ni kweli mabadiliko tunayataka lakini hayataletwa na Lowassa.
0754  425371

No comments:

Post a Comment